Mkuu wa Mkoa wa Singida Peter Serukamba jana 27.01.2023 ameweka rasmi jiwe la msingi katika ujenzi wa
Ofisi ya madereva Mkoani hapo
linalotarajiwa kugharimu zaidi ya Tsh. Milioni 79.6.
Akiongea na Watumishi baada ya kuweka jiwe hilo RC Serukamba amempongeza Katibu Tawala wa Mkoa huo Dorothy Mwaluko kwa kuleta wazo la kuwajengea Ofisi madereva ili waweze kujikinga na mvua jua na baridi jambo ambalo ameeleza kwamba litaleta ufanisi katika kazi yao.
RC amesema maamuzi hayo ni ya kijasiri kwakuwa Ofisi nyingi
za Serikali hazina Ofisi maalum za
madereva hivyo akawataka madereva hao kutunza Ofisi hiyo na kuhakikisha kwamba
wanafanya kazi kwa ufanisi mkubwa.
Katika hatua nyingine ameupongeza mpango wa kuwa na sare
maalumu inayovaliwa siku ya Ijumaa huku akiueleza kwamba inaonesha umoja katika kazi.
Amesema umoja huo utumike katika ufanyaji kazi kwa umahiri
juhudi na maarifa na kila Mtumishi ahakikishe kwa nafasi yake anatatua
changamoto za wananchi.
"Utanashati huu nilio uona usiwe wa siku ya Ijumaa
pekee bali tujitahidi siku zote tupendeze, mtu mtanashati hata kazi zake
anazifanya vizuri" Serukamba.
Kwa upande wake Katibu Tawala wa Mkoa huo Dorothy Mwaluko
amemueleza RC Serukamba kwamba ujenzi wa ofisi hiyo ni sehemu ya majengo
mbalimbali yanayoendelea kujengwa na ofisi hiyo yakihusisha nyumba za Maafisa
Tarafa ambazo nazo atakaribishwa kuzizindua siku chache zijazo.
Aidha akiongea na Watumishi hao Mwaluko amewataka kuongeza juhudi katika kufanya kazi na kuacha
mazoea katika kazi ili kuwasaidia
wananchi wa Singida huku akikemea swala la utoro kazini.
Awali akitoa taarifa ya awali Mhandisi wa Mkoa Domicianus
Kirina amesema ujenzi wa ofisi hiyo ulianza tarehe 19 Desemba, 2022 ambapo
inategemewa kukamilika tarehe 1 Machi,
2023.
Ameleeza kwamba katika kufanikisha zoezi hilo ziliundwa
kamati nne ambazo ni kamati ya manunuzi, mapokezi, ulinzi na kamati ya
ufuatiliaji.
Mhandisi Domicianus
amesema fedha ambazo zimekwisha tumika zilikuwa ni Tsh. Milioni 56.04
kwa ajili ya ununuzi wa vifaa mbalimbali na malipo ya fundi.
Mwisho.
No comments:
Post a Comment