Friday, December 01, 2023

WATENDAJI KATA, VIJIJI NA MAAFISA UGANI, SIMAMIENI KILIMO BORA - RC SERUKAMBA

Mkuu wa Mkoa wa Singida Peter Serukamba, amewataka Watendaji wa Kata, Vijiji na Maafisa Ugani wawaelekeze Wakulima umuhimu wa kanuni na taratibu za Kilimo bora ili waongeze uzalishaji wa mazao ya chakula na biashara kwa lengo la kuwakwamua kiuchumi wananchi wa Singida na Taifa kwa ujumla.

Serukamba ametoa maelekezo hayo leo Ijumaa Disemba Mosi, alipokutana nao kwenye ukumbi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama, pamoja na mambo mengine kuandaa kwa pamoja mikakati ya kilimo itakayoongeza eneo la Kilimo, kupitia mazao ya chakula na biashara mkoani Singida.

“Nataka niwaambieni, kwenye hili hatutanii Watendaji wa Kata!, naomba niwaambieni, hili jambo kwangu ni la kufa na kupona…mkitoka hapa, muende mkakutane na Serikali za kijiji, mkafanye mikutano, hakikisheni tunalima eneo jipya, ambalo mwaka jana halikulimwa, mkahakikishe vijana wote wanaozurura bila kazi kwenye maeneo yenu wanashiriki katika kilimo ili kuongeza uzalishaji wa mazao ya chakula na biashara…,” alisisitiza Serukamba.

Aidha Serukamba, ameeleza kuwa Serikali imekubali ombi la Wakulima la kupatiwa aina mpya ya mbegu ya zao la Alizeti badala ya ile ya msimu uliopita ili waongeze uzalishaji wa mafuta ya kula nchini ambayo kwa msimu uliopita Mkoa wa Singida ulichangia zaidi ya asilimia 50 ya alizeti yote inayozalishwa hapa nchini.

Katika makubaliano ya Watendaji hao wa Wilayani Mkalama na Mkuu wa Mkoa iliazimiwa kwamba eneo la kilimo msimu huu wa 2023/2024, liongezwe ekari 9,940 zaidi ili kuongeza wingi wa mazao ya chakula na biashara wakati msimu wa 2022/2023 Wilaya ya Mkalama ililima eneo lenye ukubwa wa ekari 354,230.

Kwa upande wake Katibu Tawala Msaidizi Uchumi na Uzalishaji Sekretarieti ya Mkoa Singida Stanslaus Choaji, amewataka Watendaji hao wa Kata na Vijiji, wakasimamie zoezi hilo sambamba na kurejesha fedha za ruzuku ya mbegu ya Alizeti waliyokopeshwa wakulima msimu uliopita, lakini baadhi yao wamegoma kurejesha kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo mashaka juu ya ubora wake.

“Kimsingi ni majukumu yetu hapa sote, Watendaji wa Kata na Vijiji kufanikisha suala hili kwa hiyo tunampongeza sana Mkuu wetu wa Mkoa kutukumbusha leo, na naamini kutokana na Kikao hichi sasa tunakwenda kusimamia vyema zoezi hili ili Wakulima wetu waweze kunyanyuka zaidi Kiuchumi,” alisema Choaji.

Hata hivyo kwa kuonyesha kwamba maagizo ya Serukamba yamewaingia vyema, Mtendaji wa Kata ya Mwanga, Hamisi Soya, aliwasimamisha Watendaji wa Vijiji vya Kata yake mbele ya Mkuu wa Mkoa na kuwataka hadi kufikia siku ya Jumatatu Novemba 4, 2023, wawe wameitisha mikutano ya hadhara ili kwa makubaliano na Wananchi waongeze ekari 700, kukidhi matakwa ya Serikali ya Mkoa.

“Mimi kwenye Kata yangu ya Mwanga, ninao uwezo wa kuongeza ekari 700, nitazitoa wapi!, Watendaji wa Vijiji vyangu naomba msimame wote, nawaagiza Jumatatu mfanye mikutano mtoe tatizo hili la vijana kuzurula badala kufanya kazi, walazimisheni waende kutafuta mashamba kila mmoja angalau alime ekari mbili, kama tulivyokubaliana. Naomba mkae…kwa hiyo Mkuu wa Mkoa hii siyo lelemama, tunaenda kupambana kweli kweli, na tunahakukikishia zoezi hili litakamilika, kwa asilimia mia,” alimaliza Soya.

Kutokana na Kata ya Mwanga kuwa na eneo pana kwa ajili ya shughuli za kilimo, hata hivyo wajumbe wa Kikao hicho walikubaliana Kata hiyo iongezewe eneo la kilimo hadi kufikia ekari 2,000, badala ya 700, na Afisa Mtendaji wa Kata ya Mwanga (Soya), alikubali na kuahidi kutekeleza msimu huu wa kilimo 2023/2024.

Mkuu wa Mkoa wa Singida Peter Serukamba akisisitiza jambo kwa Watendaji wa Kata, Vijiji na Maafisa Ugani wakati wa kikao hicho kilichofanyika kwenye ukumbi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama

Mkuu wa Wilaya ya Mkalama Moses Machali akizungumza na Watendaji wa Kata, Vijiji na Maafisa Ugani wakati wa kikao hicho kilichofanyika kwenye ukumbi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama



Baadhi ya Watendaji wa Kata, Vijiji na Maafisa Ugani wakimuahidi Mkuu wa Mkoa huyo utekelezaji wa maazimio ya kikao hicho kilichofanyika kwenye ukumbi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama


Katibu Tawala Msaidizi Sehemu ya Uchumi na Uzalishaji Sekretarieti ya Mkoa Beatus Choaji, akizungumza katika kikao hicho.


Kikao kikiendelea

RAS SINGIDA AKEMEA TABIA YA UKATILI, WANAWAKE NA WATOTO.

Wakati Dunia ikipiga vita tabia ya ukatili dhidi ya binadamu, takwimu zinaonesha kuwa wanawake wenye umri miaka 15 hadi 49 waliofanyiwa ukatili wa kingono kimwili na kihisia na wenza wao Mkoani Singida ni asilimia 45.

Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida, Dkt. Fatuma Mganga amesema hayo hivi karibuni wakati wa uzinduzi wa ‘Siku 16 za Kupinga Ukatili wa Kijinsia’, kwa wajumbe wa mpango kazi wa Taifa juu ya kutokomeza ukatili dhidi ya Wanawake na Watoto waliokutana ukumbi wa jengo la Mkuu wa Mkoa wa Singida wenye kauli mbiu ya “Wekeza: Kuzuia Ukatili wa Kijinsia’’.

“Mpango kazi huu ulitengenezwa kwa njia shirikishi na ninayo imani kubwa kuwa kupitia mpango huu kila mdau atatambua wajibu wake na kuutekeleza ili tufikie malengo tuliyojiwekea ya kutokomeza ukatili dhidi wa wanawake na watoto kwa asilimia 50, ifikapo 2028,” alisema.

Aidha Dkt. Mganga alibainisha kuwa utafiti uliofanywa nchini na (The 2009 National Survey on Violence against Children), unaonesha asilimia 28 ya wasichana na wavulana asilimia 13, wamefanyiwa ukatili wa kingono katika mazingira ya nyumbani.

Aidha Dkt. Mganga alisema asilimia 73 ya wasichana na asilimia 72 ya wavulana wamefanyiwa ukatili wa kimwili na zaidi ya asilimia 60, wakibainika kufanyiwa na ndugu wa karibu huku wengine asilimia 40, hufanyika wakiwa shuleni.

“Hata hivyo utafiti huu unaonesha kuwa robo ya watoto wa kitanzania wakiwemo wavulana na wasichana wamefanyiwa ukatili wa kihisia au kisai   kolojia…,” alifafanua Dk. Mganga.

Katibu Tawala huyo alisema kuwa, kupitia siku 16 za kupinga Ukatili wa Kinjinsia kwa mwaka 2023,  iwe chachu kwa jamii kubadili sura  ya vitendo vya ukatili, katika nchi na hasa Mkoa wa Singida, ambao upo kati ya Mikoa ambayo   Mimba, ndoa za utotoni na ukeketaji bado ni changamaoto kubwa.

Katika kuhakikisha mapambano dhidi ya vitendo vya ukatili yanafanikiwa, Dk. Mganga aliwataka wajumbe wa kamati ya….., wakatoe elimu kwenye taasisi na makundi mbalimbali, na kuwasilisha taarifa siku ya kilele, novemba 10, 2023, juu ya namna wajumbe walivyotekeza kampeni hii.

Kampeni ya siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia, ni kampeni kabambe ya kimataifa, inayosimamiwa na kituo cha kimataifa cha Wanawake, tangu mwaka 1991, katika kuhakikisha suala hilo linafanikiwa na kuleta matokeombora kwa jamii.

Wednesday, November 29, 2023

SERUKAMBA ATOA NENO LA POLE KWA NDUGU JAMAA NA MARAFIKI KWA AJALI ILIYOT...

BASI LA KAMPUNI YA ALLY'S STAR LAGONGA INJINI YA TRENI NA KUUA ABIRIA 13 WILAYANI MANYONI SINGIDA

Watu 13 wamefariki Dunia katika ajali iliyohusisha basi la kampuni ya Ally’s Star kugonga Injini ya Treni katika makutano ya barabara kuu ya Manyoni - Singida, kwenye eneo la Manyoni mjini, mkoani Singida, leo Jumatano Novemba 29, 2023.

Baada ya ajali hiyo Mkuu wa Mkoa wa Singida Peter Serukamba, akiongozana na kamati ya ulinzi na usalama ya mkoa alifika kwenye eneo la tukio ambako alishuhudia na kupata nafasi ya kuzungumzia tukio hilo.

Akiwa kwenye eneo la tukio Serukamba, alieleza kusikitishwa na ajali hiyo alipofika kwa ajili ya kuwatembelea na kuwapa pole kwa ndugu wa marehemu na majeruhi waliolazwa hospitali ya Wilaya ya Manyoni na waliopata rufaa kwenda hospiatli ya St. Gaspar Itigi na kuwaombea wapate nafuu majeruhi waweze kuendelea na shughuli za kujenga taifa..

Hata hivyo Serukamba, ametoa rai kwa watumiaji wa vyombo vya moto hususani madereva wa mabasi kuzingatia sheria alama na taratibu za barabarani hasa kipindi hiki cha kuelekea sikukuu za mwisho wa mwaka.

Aidha Serukamba alitumia fursa hiyo kuwashukuru Wauguzi na Madaktari wa hospitali ya Wilaya ya Manyoni na Itigi, kwa kujitoa kwa kila hali katika kuwahudumia majeruhi walionusurika kwenye ajali hiyo.

Akizungumzia ajali hiyo, Kamanda wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Singida, Stella Mutabihirwa, alisema tukio hilo limetokea majira ya saa 10 alfajiri, wakati basi hilo lenye namba za usajili T 178 DVB likijaribu kukatiza njia ya reli eneo la Manyoni mjini kisha kugongana na Injini ya Treni.

Alisema kuwa basi hilo likiwa katikati ya njia ya reli ghafla liligongwa na Injini ya Treni kilichokuwa kikirudi Manyoni mjini kutokea kituo cha Aghondi na hivyo kusababisha vifo na majeruhi waliokuwemo kwenye basi la Ally’s.

Kamanda Mutabihirwa amesema kuwa basi hilo lilikuwa na jumla ya abiria 57 na waliopoteza maisha ni abiria 13 (wanawake 6, wanaume 7) huku majeruhi wakiwa 32 na wengine waliobakia walinusurika na kuendelea na safari.   


















Tuesday, November 28, 2023

SERUKAMBA AAGIZA KUKAMILIKA KWA VYUMBA VYA MADARASA ILI YATUMIKE KWA WANAFUNZI IFIKAPO JANUARI 2024

 

Mkuu wa Mkoa wa Singida Peter Serukamba, amezitaka Halmashauri za Wilaya Mkoani Singida kukamilisha miradi ya maendeleo kwa wakati ikiwemo ya elimu ili wanafunzi wenye sifa ya elimu ya awali na msingi wapate nafasi na watakaofaulu waendelee na elimu ya Sekondari ifikapo Januari 2024.

Serukamba amesema hayo leo Novemba 28, 2023 alipoongea na Wazazi Walezi na Viongozi wa Halmashauri ya Wilaya ya Ikungi katika shule ya msingi Kintandaa muda mfupi baada ya kukagua miradi ya maendeleo kwenye kijiji cha Irisya, Msimii, Kipunda na Kintandaa ikiwa ni mwendelezo wa ziara ya kusikiliza na kutatua kero za wananchi katika kila kijiji Mkoani humo.

Mkuu huyo wa Mkoa alilazimika kutoa maelekezo hayo baada ya kujionea ujenzi wa vyumba vya madarasa ya shule ya msingi Kintandaa na ambayo yapo kwenye hatua mbalimbali za ujenzi wakati umebakia mwezi mmoja pekee wanafunzi waanze muhula mpya wa masomo kote nchini.

“Mkurugenzi, lijulishe baraza lako la Madiwani juu ya ujenzi wa vyumba vya madarasa…hakikisha mnakamilisha mapema kabla ya Disemba 31 mwaka huu, ili ifikapo mwezi wa kwanza mwakani, wanafunzi waweze kuyatumia katika masomo yao,”alisema Serukamba.

Aidha katika kituo cha afya Irisya, Serukamba, alimtaka Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo, Alli Mwanga, kulielekeza Baraza la Madiwani liidhinishe fedha za kukamilisha miradi ya Zahanati na vituo vya afya ili wananchi waanze kunufaika na matunda ya Serikali yao ya awamu ya sita.

“Kwenye miradi hii yote, hakikisheni mnaisimamia vizuri na kuifuatilia mwanzo hadi mwisho, ili iweze kuendana na kasi, ubora, thamani ya fedha na kiwango kinachostahili, kwa lengo la kuleta tija kwa jamii yetu tunayoitumikia,” alisisitiza Serukamba.

Mapema katika mkutano huo Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Ikungi, Alli Mwanga, aliipogeza Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuwaletea wananchi maendeleo kupitia miradi ya afya elimu maji na miundombinu ya barabara.

“Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa, sisi wananchi wa Halmashauri ya Wilaya ya Ikungi, pamoja na mambo mengi ya maendeleo yanayoendelea hivi sasa, tunamshuru sana Rais wetu, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kutupatia fedha za kutosha kwa ajili ya miradi mbalimbali inayotekelezwa” alisema.

Mwenyekiti huyo, alitumia muda huo pia kuwaomba wananchi waendelee kumuunga mkono Rais, kutokana na kazi kubwa ya maendeleo anayoifanya lengo likiwa ni kwa ajili ya kuwajali Watanzania, na bila kuwabagua kwa misingi ya dini na kabila lake la asili.

Ziara hiyo ni mahususi kwa Mkuu huyo wa Mkoa, kutembelea vijiji vyote 441 vya Mkoa wa Singida, huku katika awamu ya kwanza akiwa amekamilisha kukutana na wananchi wa vijiji zaidi ya 61, kwa ajili ya kusikiliza na kutatua kero mbalimbali zinazoikabili jamii.


Moja ya mwananchi wa Kijiji cha Kipunda akiuliza swali wakati wa ziara hiyo.






Mkuu wa Wilaya ya Ikingu Thomas Apson akizungumza wakati wa ziara hiyo.

Ziara ikiendelea.

Thursday, November 23, 2023

SERUKAMBA AAGIZA MCHAKATO KUANZISHA KITONGOJI KIPYA KIJIJI CHA RUNGWA

Mkuu wa Mkoa wa Singida, Peter Serukamba ameuelekeza Uongozi wa Halmashauri ya Wilaya ya Itigi Wilayani Manyoni kuitafutia ufumbuzi changamoto ya wananchi zaidi ya 2,978 walioomba kumilikishwa kipande cha ardhi, katika kijiji cha Rungwa baada ya kuishi kwenye eneo hilo kwa miaka 14.

Katika mkutano wa hadhara na wananchi wa kitongoji cha Mauki, kijiji na Kata ya Rungwa, Halmashauri ya Itigi Wilaya ya Manyoni alipokutana nao tarehe (21/11/2023) kwa ajili ya kusikiliza kero Serukamba ametaka mchakato huo mapema ili kuwezesha wananchi hao kuwa sehemu ya walinzi wa hifadhi ya Rungwa.

Awali wananchi hao, ambao wengi wao wanatoka katika jamii ya wafugaji, walimweleza Mkuu wa Mkoa kuwa wamekuwa wakiishi kwenye eneo hilo kwa miaka 14 lakini pamoja na juhudi zao katika shughuli za uzalishaji mali Serikali haiwatambui hali inayokwamisha maendeleo yao kiuchumi.

“Hatuna jinsi, Mkurugenzi na Mkuu wa Wilaya naomba muanze mchakato wa kuifanya sehemu hii kuwa Kitongoji…hawa ndio watakaokuwa walinzi wa msitu huu..,” alisisitiza Serukamba.

Baadhi ya wananchi hao waliolazimika kuomba eneo lao kutambuliwa na Serikali ni Paulina Shija, Uzenza Ndaki na Machia Machembe, na walisisitiza kuwa changamoto hiyo imekuwa kikwazo katika kujenga makazi ya kudumu na hivyo kuzorotesha maendeleo.  

Hata hivyo alipotakiwa kujibu hoja hiyo Afisa Maliasili na Uhifadhi wa Mazingira wa Halmashauri ya Wilaya ya Itigi, John Makotta, alisema eneo hilo lipo chini ya kitalu cha mwekezaji wa shughuli za uwindaji.

Makotta alifafanua kuwa, sehemu hiyo ni Kitalu cha uwindaji kinachojulikana kwa jina la ‘North Rungwa open area, huku mwekezaji akitarajiwa kuanza shughuli zake hivi karibuni baada ya kuingia mkataba na Serikali.

Pamoja na maelezo hayo, Mkuu wa Mkoa wa Singida Serukamba, amesisitiza kuanza kwa mchakato wa kuwamilikisha wananchi hao, kutokana na uzembe uliofanywa katika kuwatoa wananchi hao kwa miaka yote 14, hivyo ni lazima liwe sehemu ya Kitongoji cha Kijiji cha Rungwa.

Kwa mujibu wa hifadhi ya Rungwa, wananchi hao walivamia eneo la Mwauki miaka 14 iliyopita lakini pamoja na kuwatoa kwa nguvu mara kadhaa, wamekuwa wakirejea hivyo kusababisha usumbufu kwa mamlaka husika.