Thursday, February 12, 2026

"WATOTO WANAOPATA LISHE WANAFABYA VIZURI DARASANI" MWL. DULENGA

Wazazi na walimu wameaswa kudumisha ushirikiano wa karibu ili kuhakikisha elimu bora inaendelea kutolewa shuleni na kuleta matokeo chanya kitaaluma. Rai hiyo imetolewa leo tarehe 12 Februari 2026 na Afisa Elimu Mkoa wa Singida, Bw. Makwasa Dulenga, wakati akishiriki mahafali ya kidato cha sita yaliyofanyika katika Shule ya Sekondari Ndago mkoani Singida.

Mwl. Makwasa Dulenga akitoa hotuba kwa wahitimu Shule ya Sekondari Dago wilayani Mkalama.

Akizungumza katika hafla hiyo, Bw. Makwasa amesema mafanikio ya kitaaluma shuleni yanategemea mshikamano wa wadau wote wa elimu, hususan wazazi na walimu wenyewe. Amefafanua kuwa ushirikiano huo hujidhihirisha kupitia hatua mbalimbali ikiwemo uhamasishaji wa utoaji wa chakula shuleni, ufuatiliaji wa maendeleo ya wanafunzi na michango ya hiari inayowawezesha walimu wanaojitolea kuendelea kutoa huduma bora ya ufundishaji.

Aidha, amewataka wazazi na walezi kuhakikisha watoto wao wanapata lishe bora wakiwa shuleni, kwa kuwahimiza kuchangia chakula shuleni akisisitiza kuwa kuna uhusiano wa moja kwa moja kati ya lishe bora na ufaulu mzuri darasani. Amesema mwanafunzi anayepata chakula chenye virutubisho muhimu shuleni huwa na uwezo mkubwa wa kuzingatia masomo na kufanya vizuri katika mitihani.

Vilevile, Afisa Elimu amewahimiza wanafunzi kuendelea kuthamini fursa ya elimu kwa kujituma zaidi katika masomo yao, akibainisha kuwa wazazi na walezi wao wanajitoa kwa hali na mali kuhakikisha wanawapatia mahitaji muhimu ya shule ikiwemo sare na vifaa vya kujifunzia ili kuwajengea msingi bora wa maisha ya baadaye.


Awali akiwasilisha taarifa fupi ya shule hiyo, Mkuu wa Shule ya Sekondari Ndago, Bi. Prisca T. Msemo, amesema wanafunzi wa kidato cha sita wanaohitimu wameonyesha kiwango kizuri cha maandalizi kitaaluma kupitia mitihani mbalimbali ya majaribio waliyoifanya, ikiwemo mtihani wa utimilifu (Mock) wa Mkoa wa Singida. Ameeleza kuwa katika matokeo ya mtihani huo, shule ilishika nafasi ya tano kati ya shule 27 za mkoa, ambapo wanafunzi 54 walipata daraja la kwanza, wanafunzi 13 daraja la pili na mwanafunzi mmoja daraja la tatu, matokeo ambayo yanaonesha juhudi za walimu na wanafunzi pamoja na mazingira mazuri ya ufundishaji na ujifunzaji yaliyopo shuleni hapo.



Kwa upande wa baadhi ya wazazi waliohudhuria mahafali hayo wameipongeza hotuba ya mgeni rasmi na kuahidi kuendeleza ushirikiano katika malezi na elimu ya watoto wao. Wamesema wataendelea kuhakikisha wanafunzi wanapata mazingira mazuri ya kusoma ili waweze kufikia ndoto zao za kuendelea na masomo ya ngazi za juu. "Mgeni rasmi umesema maneno mazuri sana, umewahusia vijana wetu na sisi wazazi umetuhusia, basi tutashirikiana na walimu wetu. Pia nawashukuru walimu kwa kuwalea watoto wetu na ninyi watoto wetu bado kuna hatua huko mbele hivyo jitahidini katika masomo yenu sisi tuko pamoja na walimu wenu." Amesema mmoja katika wazazi.


Nao wanafunzi wa kidato cha sita wa Shule hiyo wamewashukuru walimu wao kwa malezi bora ya kitaaluma na kimaadili waliyoyapata katika kipindi chote cha masomo yao shuleni hapo. Wamesema juhudi, moyo wa kujitolea na ufuatiliaji wa karibu kutoka kwa walimu wao umekuwa chachu ya maendeleo yao darasani na nje ya darasa. Aidha, wameahidi kuwa watajituma kwa bidii katika mitihani yao ya mwisho ili kufanya vizuri zaidi na kuendeleza rekodi ya ufaulu wa shule hiyo, huku wakisisitiza kuwa wataendelea kuitunza heshima ya shule yao kwa matokeo mazuri yatakayodhihirisha ubora wa elimu waliyoipata.

  
















Sunday, February 08, 2026

DINI NI NYENZO YA MAADILI, UMOJA NA UTIIFU WA SHERIA – DKT. FATUMA MGANGA

 Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida, Dkt. Fatuma Mganga, amesema taasisi za dini ni nguzo muhimu katika kujenga maadili, kuimarisha umoja wa kitaifa na kukuza utii wa sheria miongoni mwa wananchi, akisisitiza kuwa maendeleo ya taifa yanahitaji jamii yenye hofu ya Mungu.

Dkt. Mganga alitoa kauli hiyo alipokuwa mgeni rasmi katika harambee ya kuchangia ununuzi wa vyombo vya muziki vya Kanisa la EAGT Nduguti, Wilaya ya Mkalama, yenye lengo la kukusanya Shilingi milioni 15. Alieleza kuwa vyombo hivyo vitatumika kuimarisha ibada, mafundisho ya kiroho na semina zitakazochangia mabadiliko chanya ya kijamii.

Alifafanua kuwa hofu ya Mungu hujengwa kupitia malezi na mafundisho yanayotolewa na taasisi za dini, hali inayosaidia kupata raia watiifu, wanaozingatia sheria na kuepuka vitendo vya rushwa, ufisadi na uhalifu. Alisisitiza kuwa jamii yenye misingi imara ya kiroho ni msingi wa utawala bora na amani ya kudumu.


Aidha, Dkt. Mganga alisema shughuli hiyo imeonesha mshikamano wa kijamii kwa kuwakutanisha wananchi wa imani tofauti kushiriki lengo moja la maendeleo. Alieleza kuwa ushiriki wa viongozi wa Serikali, viongozi wa dini na wananchi kwa pamoja unaimarisha umoja na ushirikiano unaohitajika katika kujenga taifa lenye maadili.



Kwa upande wake, Katibu Tawala wa Wilaya ya Mkalama, Bi. Happyness Sulle, alisema taasisi za dini zimekuwa washirika wakuu wa Serikali katika kuhubiri amani, maadili na mshikamano, hususan kwa vijana, jambo linalochangia utulivu na maendeleo ya wilaya hiyo.


Naye Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama, Bi. Asia Messos, alisema Serikali itaendelea kushirikiana na taasisi za dini katika utekelezaji wa mipango ya maendeleo, akibainisha kuwa maendeleo ya jamii yanahitaji ushirikiano wa karibu kati ya Serikali na taasisi za dini.




Akizungumza kwa niaba ya Kanisa la EAGT Nduguti, Mchungaji wa Kanisa hilo alisema taasisi za dini zitaendelea kuwa mstari wa mbele katika kukuza maadili mema, kupunguza vitendo vya uhalifu na kuijenga jamii yenye hofu ya Mungu kwa kushirikiana na Serikali.


Harambee hiyo ni sehemu ya jitihada za kuimarisha ibada, malezi ya kiroho na mshikamano wa kijamii, kwa lengo la kujenga taifa lenye maadili, umoja na utii wa sheria.









https://www.youtube.com/watch?v=M7aatIDpxbI&pp=ygUJU2luZ2lkYXJz 

 

Wednesday, January 28, 2026

KILA MMOJA ALINDE ENEO LAKE NA KUFUATA SHERIA - RC DENDEGO

 Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mhe. Halima Dendego, ametoa uhakika wa utatuzi wa mgogoro wa ardhi unaohusisha wananchi wa Wilaya ya Manyoni na Serikali, akiwataka wananchi kuwa wavumilivu na wenye subira wakati zoezi la usuluhishi na uhakiki wa maeneo ya makazi likiendelea kufanyika.


Mhe. Dendego alitoa kauli hiyo alipokuwa akizungumza na wananchi katika eneo la mradi wa ujenzi wa Chuo cha Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA), eneo ambalo limekuwa na mgogoro wa ardhi kati ya Serikali na wananchi wanaoishi katika maeneo yanayokusudiwa kutumika kwa utekelezaji wa miradi ya maendeleo.


Akizungumza katika mkutano huo, Mkuu wa Mkoa alisema Serikali imejipanga kusikiliza hoja na malalamiko ya wananchi kwa kina, na kutatua mgogoro huo kwa hatua, kwa kuanza na kaya zote zilizopo katika maeneo yanayoguswa na miradi hiyo, yakiwemo maeneo ya shule za msingi na sekondari, afya, viwanda pamoja na VETA.

Alisisitiza kuwa mchakato wa utatuzi wa mgogoro huo utafanyika kwa kuzingatia misingi ya haki, uwazi na kwa kufuata sheria na taratibu zilizopo, akibainisha kuwa Serikali haina dhamira ya kuwaonea wananchi bali kuhakikisha miradi ya umma inatekelezwa sambamba na kulinda haki za wananchi.
Aidha, Mhe. Dendego aliwaondoa hofu wananchi ambao nyumba zao zimewekewa alama ya “X”, akieleza kuwa alama hiyo haimaanishi kubomolewa kwa nyumba husika bali ni ishara ya kuwa nyumba hizo zimepitiwa katika hatua ya awali ya uhakiki, huku kamati maalum ikiendelea na tathmini ya kina kwa kuwafuata wananchi katika makazi yao.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Manyoni, Mhe. Dkt. Vincent Mashinji, amesema Wilaya ya Manyoni ni salama na imejengwa katika misingi ya kusikilizana hata panapokuwepo mitazamo tofauti, bila migogoro kugeuka kuwa fujo. Amesema mgogoro huo uliwahi kufikishwa katika ofisi yake na kamati iliundwa, ambayo ilibaini kuwa zaidi ya wananchi 400 wanahusishwa na migogoro ya ardhi katika maeneo ya miradi ya umma ya maendeleo ikiwemo viwanda, shule, huduma za afya na VETA.
Dkt. Mashinji ameongeza kuwa Wilaya imefanya juhudi kubwa katika kushughulikia suala hilo, hatua iliyosababisha kumualika Mkuu wa Mkoa kuja kusaidia kusuluhisha changamoto hiyo kwa kiwango cha juu zaidi, akisisitiza kuwa kila mwananchi atapata haki yake kwa mujibu wa sheria na taratibu.


Katika mkutano huo, wananchi wameeleza furaha na matumaini makubwa baada ya kusikia kauli ya Mkuu wa Mkoa aliyewahakikishia kuwa ndani ya siku 14 mgogoro huo utakuwa umesuluhishwa, wakisema ahadi hiyo imewajengea imani mpya na kuwapa nafuu ya moyo kwamba changamoto yao ya muda mrefu sasa inaelekea kufikia tamati, huku wakiahidi kushirikiana na Serikali hadi suluhu ya kudumu ipatikane.

Kwa mujibu wa taarifa za Wilaya ya Manyoni, mgogoro wa ardhi katika maeneo ya miradi ya umma umedumu kwa muda mrefu kutokana na kukosekana kwa uhakiki wa kina wa umiliki wa ardhi kabla ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo, hali iliyosababisha sintofahamu kati ya wananchi na Serikali, na hivyo kuilazimu Serikali ya Mkoa kuingilia kati ili kuhakikisha haki za wananchi zinalindwa sambamba na utekelezaji wa miradi ya kimkakati ya maendeleo.



Thursday, January 22, 2026

MALIGHAFI ZAIDI ZAHITAJIKA ILI KUINUA VIWANDA MKOANI SINGIDA

 

Posted on: January 22nd, 2026

Mkoa wa Singida umetajwa kuwa na fursa kubwa ya kukuza uchumi wa viwanda, lakini bado unakabiliwa na changamoto ya uhaba wa malighafi unaosababisha baadhi ya viwanda kusimamisha uzalishaji. Kauli hiyo imetolewa na Brigedia Jenerali Charles  Ndiege wakati wa ziara ya mafunzo kwa vitendo ya washiriki wa kozi ya Chuo cha Taifa cha Ulinzi waliotembelea viwanda mbalimbali mkoani humo.

Akizungumza baada ya kutembelea viwanda vya kuchakata alizeti na pamba, leo Januari 22,2025 Brigedia Jenerali Ndiege amesema changamoto kubwa iliyojitokeza ni viwanda kushindwa kufanya kazi kwa msimu mzima kutokana na utegemezi wa malighafi zinazotokana na kilimo cha mvua. Amesema hali hiyo huathiri mnyororo mzima wa maendeleo ya kiuchumi, kuanzia wakulima hadi wafanyakazi wa viwandani.

Amefafanua kuwa viwanda vinaposimama, ajira hupungua na mapato ya wananchi hushuka, hali inayodhoofisha mchango wa sekta ya viwanda katika pato la taifa. Kwa mtazamo wake, uzalishaji wa viwanda hauwezi kuwa endelevu bila sera madhubuti zitakazohakikisha upatikanaji wa malighafi kwa uhakika na kwa wingi.

Brigedia Jenerali Ndiege amesisitiza kuwa kuongeza uzalishaji wa mazao ya viwandani ni ajenda ya kimkakati kwa taifa, akibainisha kuwa masuala ya chakula na viwanda yanagusa moja kwa moja usalama wa taifa. Ameshauri kuimarishwa kwa kilimo cha tija, matumizi ya teknolojia na ushirikiano wa karibu kati ya serikali, wakulima na wawekezaji wa viwanda.

Kwa upande wa washiriki wa kozi hiyo, Hawa Adam kutoka Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo amesema ziara hiyo imewapa uelewa wa kina kuhusu mchango wa viwanda vya Singida katika kukuza uchumi wa taifa. Amesema viwanda hivyo vinatoa soko la uhakika kwa wakulima na hivyo kuboresha maisha yao kupitia kipato na upatikanaji wa huduma za kijamii.

Ameongeza kuwa changamoto ya uzalishaji mdogo inaweza kutatuliwa kwa kutoa elimu zaidi kwa wakulima juu ya mbinu bora za kilimo ili kuongeza mavuno ya mazao yanayotumika kama malighafi viwandani, hatua itakayosaidia viwanda kufanya kazi kwa ufanisi zaidi.

Aidha, Wawakilishi wa viwanda vya Biosustain Tanzania Limited na Mount Meru Millers Limited wameeleza kuwa uzalishaji mdogo wa pamba na alizeti bado ni changamoto kubwa, wakisisitiza umuhimu wa kuendelea kuhamasisha wakulima kuongeza uzalishaji. Wamesema kupitia elimu, motisha na ushirikiano na serikali, uzalishaji unaweza kuongezeka na kuwezesha viwanda kufanya kazi kwa muda mrefu zaidi.

Ziara ya washiriki wa kozi ya Chuo cha Taifa cha Ulinzi mkoani Singida ni sehemu ya mafunzo kwa vitendo yanayolenga kuoanisha nadharia za darasani na utekelezaji wa sera, mipango na mikakati ya serikali katika mazingira halisi. Kupitia ziara hiyo, washiriki wanapata fursa ya kutathmini maendeleo ya viwanda, kilimo na uchumi kwa ujumla, pamoja na kubaini changamoto na fursa zilizopo kwa maendeleo endelevu ya taifa.