Sunday, February 08, 2026

DINI NI NYENZO YA MAADILI, UMOJA NA UTIIFU WA SHERIA – DKT. FATUMA MGANGA

 Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida, Dkt. Fatuma Mganga, amesema taasisi za dini ni nguzo muhimu katika kujenga maadili, kuimarisha umoja wa kitaifa na kukuza utii wa sheria miongoni mwa wananchi, akisisitiza kuwa maendeleo ya taifa yanahitaji jamii yenye hofu ya Mungu.

Dkt. Mganga alitoa kauli hiyo alipokuwa mgeni rasmi katika harambee ya kuchangia ununuzi wa vyombo vya muziki vya Kanisa la EAGT Nduguti, Wilaya ya Mkalama, yenye lengo la kukusanya Shilingi milioni 15. Alieleza kuwa vyombo hivyo vitatumika kuimarisha ibada, mafundisho ya kiroho na semina zitakazochangia mabadiliko chanya ya kijamii.

Alifafanua kuwa hofu ya Mungu hujengwa kupitia malezi na mafundisho yanayotolewa na taasisi za dini, hali inayosaidia kupata raia watiifu, wanaozingatia sheria na kuepuka vitendo vya rushwa, ufisadi na uhalifu. Alisisitiza kuwa jamii yenye misingi imara ya kiroho ni msingi wa utawala bora na amani ya kudumu.


Aidha, Dkt. Mganga alisema shughuli hiyo imeonesha mshikamano wa kijamii kwa kuwakutanisha wananchi wa imani tofauti kushiriki lengo moja la maendeleo. Alieleza kuwa ushiriki wa viongozi wa Serikali, viongozi wa dini na wananchi kwa pamoja unaimarisha umoja na ushirikiano unaohitajika katika kujenga taifa lenye maadili.



Kwa upande wake, Katibu Tawala wa Wilaya ya Mkalama, Bi. Happyness Sulle, alisema taasisi za dini zimekuwa washirika wakuu wa Serikali katika kuhubiri amani, maadili na mshikamano, hususan kwa vijana, jambo linalochangia utulivu na maendeleo ya wilaya hiyo.


Naye Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama, Bi. Asia Messos, alisema Serikali itaendelea kushirikiana na taasisi za dini katika utekelezaji wa mipango ya maendeleo, akibainisha kuwa maendeleo ya jamii yanahitaji ushirikiano wa karibu kati ya Serikali na taasisi za dini.




Akizungumza kwa niaba ya Kanisa la EAGT Nduguti, Mchungaji wa Kanisa hilo alisema taasisi za dini zitaendelea kuwa mstari wa mbele katika kukuza maadili mema, kupunguza vitendo vya uhalifu na kuijenga jamii yenye hofu ya Mungu kwa kushirikiana na Serikali.


Harambee hiyo ni sehemu ya jitihada za kuimarisha ibada, malezi ya kiroho na mshikamano wa kijamii, kwa lengo la kujenga taifa lenye maadili, umoja na utii wa sheria.









https://www.youtube.com/watch?v=M7aatIDpxbI&pp=ygUJU2luZ2lkYXJz 

 

Wednesday, January 28, 2026

KILA MMOJA ALINDE ENEO LAKE NA KUFUATA SHERIA - RC DENDEGO

 Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mhe. Halima Dendego, ametoa uhakika wa utatuzi wa mgogoro wa ardhi unaohusisha wananchi wa Wilaya ya Manyoni na Serikali, akiwataka wananchi kuwa wavumilivu na wenye subira wakati zoezi la usuluhishi na uhakiki wa maeneo ya makazi likiendelea kufanyika.


Mhe. Dendego alitoa kauli hiyo alipokuwa akizungumza na wananchi katika eneo la mradi wa ujenzi wa Chuo cha Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA), eneo ambalo limekuwa na mgogoro wa ardhi kati ya Serikali na wananchi wanaoishi katika maeneo yanayokusudiwa kutumika kwa utekelezaji wa miradi ya maendeleo.


Akizungumza katika mkutano huo, Mkuu wa Mkoa alisema Serikali imejipanga kusikiliza hoja na malalamiko ya wananchi kwa kina, na kutatua mgogoro huo kwa hatua, kwa kuanza na kaya zote zilizopo katika maeneo yanayoguswa na miradi hiyo, yakiwemo maeneo ya shule za msingi na sekondari, afya, viwanda pamoja na VETA.

Alisisitiza kuwa mchakato wa utatuzi wa mgogoro huo utafanyika kwa kuzingatia misingi ya haki, uwazi na kwa kufuata sheria na taratibu zilizopo, akibainisha kuwa Serikali haina dhamira ya kuwaonea wananchi bali kuhakikisha miradi ya umma inatekelezwa sambamba na kulinda haki za wananchi.
Aidha, Mhe. Dendego aliwaondoa hofu wananchi ambao nyumba zao zimewekewa alama ya “X”, akieleza kuwa alama hiyo haimaanishi kubomolewa kwa nyumba husika bali ni ishara ya kuwa nyumba hizo zimepitiwa katika hatua ya awali ya uhakiki, huku kamati maalum ikiendelea na tathmini ya kina kwa kuwafuata wananchi katika makazi yao.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Manyoni, Mhe. Dkt. Vincent Mashinji, amesema Wilaya ya Manyoni ni salama na imejengwa katika misingi ya kusikilizana hata panapokuwepo mitazamo tofauti, bila migogoro kugeuka kuwa fujo. Amesema mgogoro huo uliwahi kufikishwa katika ofisi yake na kamati iliundwa, ambayo ilibaini kuwa zaidi ya wananchi 400 wanahusishwa na migogoro ya ardhi katika maeneo ya miradi ya umma ya maendeleo ikiwemo viwanda, shule, huduma za afya na VETA.
Dkt. Mashinji ameongeza kuwa Wilaya imefanya juhudi kubwa katika kushughulikia suala hilo, hatua iliyosababisha kumualika Mkuu wa Mkoa kuja kusaidia kusuluhisha changamoto hiyo kwa kiwango cha juu zaidi, akisisitiza kuwa kila mwananchi atapata haki yake kwa mujibu wa sheria na taratibu.


Katika mkutano huo, wananchi wameeleza furaha na matumaini makubwa baada ya kusikia kauli ya Mkuu wa Mkoa aliyewahakikishia kuwa ndani ya siku 14 mgogoro huo utakuwa umesuluhishwa, wakisema ahadi hiyo imewajengea imani mpya na kuwapa nafuu ya moyo kwamba changamoto yao ya muda mrefu sasa inaelekea kufikia tamati, huku wakiahidi kushirikiana na Serikali hadi suluhu ya kudumu ipatikane.

Kwa mujibu wa taarifa za Wilaya ya Manyoni, mgogoro wa ardhi katika maeneo ya miradi ya umma umedumu kwa muda mrefu kutokana na kukosekana kwa uhakiki wa kina wa umiliki wa ardhi kabla ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo, hali iliyosababisha sintofahamu kati ya wananchi na Serikali, na hivyo kuilazimu Serikali ya Mkoa kuingilia kati ili kuhakikisha haki za wananchi zinalindwa sambamba na utekelezaji wa miradi ya kimkakati ya maendeleo.



Thursday, January 22, 2026

MALIGHAFI ZAIDI ZAHITAJIKA ILI KUINUA VIWANDA MKOANI SINGIDA

 

Posted on: January 22nd, 2026

Mkoa wa Singida umetajwa kuwa na fursa kubwa ya kukuza uchumi wa viwanda, lakini bado unakabiliwa na changamoto ya uhaba wa malighafi unaosababisha baadhi ya viwanda kusimamisha uzalishaji. Kauli hiyo imetolewa na Brigedia Jenerali Charles  Ndiege wakati wa ziara ya mafunzo kwa vitendo ya washiriki wa kozi ya Chuo cha Taifa cha Ulinzi waliotembelea viwanda mbalimbali mkoani humo.

Akizungumza baada ya kutembelea viwanda vya kuchakata alizeti na pamba, leo Januari 22,2025 Brigedia Jenerali Ndiege amesema changamoto kubwa iliyojitokeza ni viwanda kushindwa kufanya kazi kwa msimu mzima kutokana na utegemezi wa malighafi zinazotokana na kilimo cha mvua. Amesema hali hiyo huathiri mnyororo mzima wa maendeleo ya kiuchumi, kuanzia wakulima hadi wafanyakazi wa viwandani.

Amefafanua kuwa viwanda vinaposimama, ajira hupungua na mapato ya wananchi hushuka, hali inayodhoofisha mchango wa sekta ya viwanda katika pato la taifa. Kwa mtazamo wake, uzalishaji wa viwanda hauwezi kuwa endelevu bila sera madhubuti zitakazohakikisha upatikanaji wa malighafi kwa uhakika na kwa wingi.

Brigedia Jenerali Ndiege amesisitiza kuwa kuongeza uzalishaji wa mazao ya viwandani ni ajenda ya kimkakati kwa taifa, akibainisha kuwa masuala ya chakula na viwanda yanagusa moja kwa moja usalama wa taifa. Ameshauri kuimarishwa kwa kilimo cha tija, matumizi ya teknolojia na ushirikiano wa karibu kati ya serikali, wakulima na wawekezaji wa viwanda.

Kwa upande wa washiriki wa kozi hiyo, Hawa Adam kutoka Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo amesema ziara hiyo imewapa uelewa wa kina kuhusu mchango wa viwanda vya Singida katika kukuza uchumi wa taifa. Amesema viwanda hivyo vinatoa soko la uhakika kwa wakulima na hivyo kuboresha maisha yao kupitia kipato na upatikanaji wa huduma za kijamii.

Ameongeza kuwa changamoto ya uzalishaji mdogo inaweza kutatuliwa kwa kutoa elimu zaidi kwa wakulima juu ya mbinu bora za kilimo ili kuongeza mavuno ya mazao yanayotumika kama malighafi viwandani, hatua itakayosaidia viwanda kufanya kazi kwa ufanisi zaidi.

Aidha, Wawakilishi wa viwanda vya Biosustain Tanzania Limited na Mount Meru Millers Limited wameeleza kuwa uzalishaji mdogo wa pamba na alizeti bado ni changamoto kubwa, wakisisitiza umuhimu wa kuendelea kuhamasisha wakulima kuongeza uzalishaji. Wamesema kupitia elimu, motisha na ushirikiano na serikali, uzalishaji unaweza kuongezeka na kuwezesha viwanda kufanya kazi kwa muda mrefu zaidi.

Ziara ya washiriki wa kozi ya Chuo cha Taifa cha Ulinzi mkoani Singida ni sehemu ya mafunzo kwa vitendo yanayolenga kuoanisha nadharia za darasani na utekelezaji wa sera, mipango na mikakati ya serikali katika mazingira halisi. Kupitia ziara hiyo, washiriki wanapata fursa ya kutathmini maendeleo ya viwanda, kilimo na uchumi kwa ujumla, pamoja na kubaini changamoto na fursa zilizopo kwa maendeleo endelevu ya taifa.


Wednesday, January 21, 2026

DKT.MGANGA AWAPIGA MSASA MAAFISA ELIMU KATA NAMNA YA KUBORESHA UFAULU MASHULENI

 Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida, Dkt. Fatuma Mganga, amewaagiza Maafisa Elimu Kata kuimarisha uwajibikaji, ubunifu na ufuatiliaji wa karibu katika usimamizi wa elimu ili kuongeza ufaulu wa wanafunzi katika mitihani ya kitaifa. Ameyasema hayo wakati wa kikao kazi cha Maafisa Elimu Kata wa Mkoa wa Singida kilichofanyika katika Ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa.


Akizungumza katika kikao hicho, Dkt. Mganga amesema takwimu za ufaulu kwa miaka ya karibuni zimekuwa zikionesha mabadiliko ya kupanda na kushuka, hali inayoashiria changamoto katika utekelezaji wa majukumu ya usimamizi wa ufundishaji na ujifunzaji. Ameeleza kuwa masomo ya Hisabati, Kiingereza na Sayansi yameendelea kuonesha ufaulu wa chini, jambo linalohitaji mikakati madhubuti, mbinu bunifu za ufundishaji na ufuatiliaji wa mara kwa mara katika shule.

Ameeleza kuwa lengo la Mkoa wa Singida ni kuongeza kiwango cha ufaulu kutoka asilimia 81.21 mwaka 2025 hadi kufikia asilimia 95, akisisitiza kuwa mafanikio hayo yanategemea kwa kiasi kikubwa uwajibikaji wa Maafisa Elimu Kata. Amesema viongozi hao wako karibu zaidi na shule, hivyo wana nafasi ya kubaini changamoto mapema na kuchukua hatua stahiki kabla hazijaathiri matokeo ya wanafunzi.

Dkt. Mganga ameongeza kuwa jukumu la Maafisa Elimu Kata si kufundisha moja kwa moja, bali ni kuhakikisha walimu wanafundisha kwa ufanisi, wanazingatia mitaala, wanapata stahili zao kwa wakati na wanahamasishwa kufanya kazi kwa nidhamu na ari. Amesisitiza pia utekelezaji wa maazimio ya kikao hicho kwa vitendo na kuendeleza utamaduni wa tathmini ya mara kwa mara ili kuleta maboresho endelevu katika shule za msingi na sekondari.

Aidha, Afisa Elimu mstaafu, Ndg. Hamisi Maulidi, amesema kikao kazi hicho kinalenga kuwajengea uwezo Maafisa Elimu Kata ili kuimarisha usimamizi wa elimu mkoani Singida. Amebainisha kuwa mafanikio ya Mkoa katika mitihani ya kitaifa yanategemea moja kwa moja weledi na ufanisi wa usimamizi wao katika ngazi ya kata.

Nao Maafisa hawakusita kueleza furaha yao kutokana na kikao kazi hicho, Bw. Benjamini Nikodemas, Afisa Elimu Kata ya Miganga amesema maelekezo yaliyotolewa yameongeza hamasa ya kufanya kazi kwa weledi zaidi, huku Afisa Elimu Kata ya Muhalala, Mwl. Fatina Rajabu, akieleza kuwa kikao hicho kimewapa motisha ya kuimarisha mbinu za usimamizi na kujifunza uzoefu bora ili kuongeza ufaulu mwaka 2026.

Kwa ujumla, kikao kazi hicho kimefanyika katika kipindi muhimu kufuatia kutangazwa kwa matokeo ya mitihani ya Darasa la Nne, Darasa la Saba na Kidato cha Pili pamoja na tathmini ya Mtihani wa Kidato cha Nne, kikitoa fursa ya kufanya tathmini ya kina ya mafanikio na changamoto katika sekta ya elimu. Hatua hiyo ni sehemu ya mkakati wa Mkoa wa Singida wa kuimarisha uwajibikaji na kuongeza ufaulu wa mitihani ya kitaifa kwa kuweka mkazo katika usimamizi wa karibu na utendaji unaozingatia matokeo.







KWA KUTAZAMA VIDEO YA KIKAO, TAZAMA VIDEO HAPA CHINI:




 



Saturday, January 10, 2026

CHANGAMOTO ZA WAFUGAJI NA WAVUVI SINGIDA ZAANZA KUPATIWA UFUMBUZI

 


Posted on: January 10th, 2026

Wananchi wa Wilaya za Iramba na 
Mkalama mkoani Singida wameeleza matumaini mapya baada ya ziara ya kikazi ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Balozi Bashiru Kakurwa (Mb), iliyofanyika leo tarehe 10 Januari 2025, wakisema imefungua fursa ya kusikilizwa na kushughulikiwa changamoto zinazowakabili katika sekta ya mifugo na uvuvi.

Katika Wilaya ya Iramba, wananchi na viongozi wa wilaya walieleza kuwa uchumi wa eneo hilo unategemea kwa kiasi kikubwa ufugaji na uvuvi katika Ziwa Kitangiri. Mkuu wa Wilaya alibainisha kuwa wilaya ina idadi kubwa ya mifugo lakini bado inakabiliwa na upungufu wa miundombinu ya kisasa kama machinjio, minada na majosho, pamoja na uhaba wa watumishi wa mifugo na uvuvi. Alisema hali hiyo imekuwa ikiwalazimu wananchi kutumia gharama kubwa kupata huduma na wakati mwingine kushindwa kufikia masoko yenye tija.

Afisa Uvuvi wa wilaya alieleza kuwa shughuli za uvuvi zinaendelea kufanyika licha ya changamoto za vifaa na rasilimali, akibainisha kuwa wilaya ina wavuvi hai 204, mitumbwi 34 iliyosajiliwa na boti moja pekee. Alisema bado kuna hitaji kubwa la kuimarisha usimamizi wa rasilimali za uvuvi, kutoa elimu ya uvuvi endelevu kwa wananchi na kuboresha miundombinu ya uvuvi ili kuongeza tija na kipato cha wavuvi.

Katika Wilaya ya Mkalama, Mkuu wa Wilaya Mhe.Moses Machali alisema migogoro ya wakulima na wafugaji imekuwa changamoto ya muda mrefu, hasa katika maeneo ya mipakani, akisisitiza kuwa kuwekwa kwa mipaka rasmi kati ya Wilaya ya Mkalama na Meatu ni hatua muhimu ya kudhibiti migogoro hiyo. Aliongeza kuwa kuna haja ya kulifufua shamba la mifugo la Serikali lililotelekezwa na kuvamiwa, ili kulinda mali ya umma na kutoa mfano wa ufugaji wa kisasa kwa wananchi.

Wananchi wa Kijiji cha Nyahaa walieleza kero zao kuhusu uvamizi wa mifugo, wizi na migogoro iliyosababisha majeruhi na hasara za mali, wakisisitiza umuhimu wa Serikali kuchukua hatua hatua za haraka kurejesha amani na kuimarisha ulinzi wa mifugo.

Kwa ujumla, wananchi walisema ziara hiyo imeongeza uwazi na matumaini mapya, huku viongozi wa wilaya na wataalamu wa sekta wakisisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya Serikali na wananchi ili kuboresha huduma za mifugo na uvuvi na kuchochea maendeleo ya kiuchumi katika mkoa wa Singida.