Thursday, January 22, 2026

MALIGHAFI ZAIDI ZAHITAJIKA ILI KUINUA VIWANDA MKOANI SINGIDA

 

Posted on: January 22nd, 2026

Mkoa wa Singida umetajwa kuwa na fursa kubwa ya kukuza uchumi wa viwanda, lakini bado unakabiliwa na changamoto ya uhaba wa malighafi unaosababisha baadhi ya viwanda kusimamisha uzalishaji. Kauli hiyo imetolewa na Brigedia Jenerali Charles  Ndiege wakati wa ziara ya mafunzo kwa vitendo ya washiriki wa kozi ya Chuo cha Taifa cha Ulinzi waliotembelea viwanda mbalimbali mkoani humo.

Akizungumza baada ya kutembelea viwanda vya kuchakata alizeti na pamba, leo Januari 22,2025 Brigedia Jenerali Ndiege amesema changamoto kubwa iliyojitokeza ni viwanda kushindwa kufanya kazi kwa msimu mzima kutokana na utegemezi wa malighafi zinazotokana na kilimo cha mvua. Amesema hali hiyo huathiri mnyororo mzima wa maendeleo ya kiuchumi, kuanzia wakulima hadi wafanyakazi wa viwandani.

Amefafanua kuwa viwanda vinaposimama, ajira hupungua na mapato ya wananchi hushuka, hali inayodhoofisha mchango wa sekta ya viwanda katika pato la taifa. Kwa mtazamo wake, uzalishaji wa viwanda hauwezi kuwa endelevu bila sera madhubuti zitakazohakikisha upatikanaji wa malighafi kwa uhakika na kwa wingi.

Brigedia Jenerali Ndiege amesisitiza kuwa kuongeza uzalishaji wa mazao ya viwandani ni ajenda ya kimkakati kwa taifa, akibainisha kuwa masuala ya chakula na viwanda yanagusa moja kwa moja usalama wa taifa. Ameshauri kuimarishwa kwa kilimo cha tija, matumizi ya teknolojia na ushirikiano wa karibu kati ya serikali, wakulima na wawekezaji wa viwanda.

Kwa upande wa washiriki wa kozi hiyo, Hawa Adam kutoka Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo amesema ziara hiyo imewapa uelewa wa kina kuhusu mchango wa viwanda vya Singida katika kukuza uchumi wa taifa. Amesema viwanda hivyo vinatoa soko la uhakika kwa wakulima na hivyo kuboresha maisha yao kupitia kipato na upatikanaji wa huduma za kijamii.

Ameongeza kuwa changamoto ya uzalishaji mdogo inaweza kutatuliwa kwa kutoa elimu zaidi kwa wakulima juu ya mbinu bora za kilimo ili kuongeza mavuno ya mazao yanayotumika kama malighafi viwandani, hatua itakayosaidia viwanda kufanya kazi kwa ufanisi zaidi.

Aidha, Wawakilishi wa viwanda vya Biosustain Tanzania Limited na Mount Meru Millers Limited wameeleza kuwa uzalishaji mdogo wa pamba na alizeti bado ni changamoto kubwa, wakisisitiza umuhimu wa kuendelea kuhamasisha wakulima kuongeza uzalishaji. Wamesema kupitia elimu, motisha na ushirikiano na serikali, uzalishaji unaweza kuongezeka na kuwezesha viwanda kufanya kazi kwa muda mrefu zaidi.

Ziara ya washiriki wa kozi ya Chuo cha Taifa cha Ulinzi mkoani Singida ni sehemu ya mafunzo kwa vitendo yanayolenga kuoanisha nadharia za darasani na utekelezaji wa sera, mipango na mikakati ya serikali katika mazingira halisi. Kupitia ziara hiyo, washiriki wanapata fursa ya kutathmini maendeleo ya viwanda, kilimo na uchumi kwa ujumla, pamoja na kubaini changamoto na fursa zilizopo kwa maendeleo endelevu ya taifa.


Wednesday, January 21, 2026

DKT.MGANGA AWAPIGA MSASA MAAFISA ELIMU KATA NAMNA YA KUBORESHA UFAULU MASHULENI

 Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida, Dkt. Fatuma Mganga, amewaagiza Maafisa Elimu Kata kuimarisha uwajibikaji, ubunifu na ufuatiliaji wa karibu katika usimamizi wa elimu ili kuongeza ufaulu wa wanafunzi katika mitihani ya kitaifa. Ameyasema hayo wakati wa kikao kazi cha Maafisa Elimu Kata wa Mkoa wa Singida kilichofanyika katika Ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa.


Akizungumza katika kikao hicho, Dkt. Mganga amesema takwimu za ufaulu kwa miaka ya karibuni zimekuwa zikionesha mabadiliko ya kupanda na kushuka, hali inayoashiria changamoto katika utekelezaji wa majukumu ya usimamizi wa ufundishaji na ujifunzaji. Ameeleza kuwa masomo ya Hisabati, Kiingereza na Sayansi yameendelea kuonesha ufaulu wa chini, jambo linalohitaji mikakati madhubuti, mbinu bunifu za ufundishaji na ufuatiliaji wa mara kwa mara katika shule.

Ameeleza kuwa lengo la Mkoa wa Singida ni kuongeza kiwango cha ufaulu kutoka asilimia 81.21 mwaka 2025 hadi kufikia asilimia 95, akisisitiza kuwa mafanikio hayo yanategemea kwa kiasi kikubwa uwajibikaji wa Maafisa Elimu Kata. Amesema viongozi hao wako karibu zaidi na shule, hivyo wana nafasi ya kubaini changamoto mapema na kuchukua hatua stahiki kabla hazijaathiri matokeo ya wanafunzi.

Dkt. Mganga ameongeza kuwa jukumu la Maafisa Elimu Kata si kufundisha moja kwa moja, bali ni kuhakikisha walimu wanafundisha kwa ufanisi, wanazingatia mitaala, wanapata stahili zao kwa wakati na wanahamasishwa kufanya kazi kwa nidhamu na ari. Amesisitiza pia utekelezaji wa maazimio ya kikao hicho kwa vitendo na kuendeleza utamaduni wa tathmini ya mara kwa mara ili kuleta maboresho endelevu katika shule za msingi na sekondari.

Aidha, Afisa Elimu mstaafu, Ndg. Hamisi Maulidi, amesema kikao kazi hicho kinalenga kuwajengea uwezo Maafisa Elimu Kata ili kuimarisha usimamizi wa elimu mkoani Singida. Amebainisha kuwa mafanikio ya Mkoa katika mitihani ya kitaifa yanategemea moja kwa moja weledi na ufanisi wa usimamizi wao katika ngazi ya kata.

Nao Maafisa hawakusita kueleza furaha yao kutokana na kikao kazi hicho, Bw. Benjamini Nikodemas, Afisa Elimu Kata ya Miganga amesema maelekezo yaliyotolewa yameongeza hamasa ya kufanya kazi kwa weledi zaidi, huku Afisa Elimu Kata ya Muhalala, Mwl. Fatina Rajabu, akieleza kuwa kikao hicho kimewapa motisha ya kuimarisha mbinu za usimamizi na kujifunza uzoefu bora ili kuongeza ufaulu mwaka 2026.

Kwa ujumla, kikao kazi hicho kimefanyika katika kipindi muhimu kufuatia kutangazwa kwa matokeo ya mitihani ya Darasa la Nne, Darasa la Saba na Kidato cha Pili pamoja na tathmini ya Mtihani wa Kidato cha Nne, kikitoa fursa ya kufanya tathmini ya kina ya mafanikio na changamoto katika sekta ya elimu. Hatua hiyo ni sehemu ya mkakati wa Mkoa wa Singida wa kuimarisha uwajibikaji na kuongeza ufaulu wa mitihani ya kitaifa kwa kuweka mkazo katika usimamizi wa karibu na utendaji unaozingatia matokeo.







KWA KUTAZAMA VIDEO YA KIKAO, TAZAMA VIDEO HAPA CHINI:




 



Saturday, January 10, 2026

CHANGAMOTO ZA WAFUGAJI NA WAVUVI SINGIDA ZAANZA KUPATIWA UFUMBUZI

 


Posted on: January 10th, 2026

Wananchi wa Wilaya za Iramba na 
Mkalama mkoani Singida wameeleza matumaini mapya baada ya ziara ya kikazi ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Balozi Bashiru Kakurwa (Mb), iliyofanyika leo tarehe 10 Januari 2025, wakisema imefungua fursa ya kusikilizwa na kushughulikiwa changamoto zinazowakabili katika sekta ya mifugo na uvuvi.

Katika Wilaya ya Iramba, wananchi na viongozi wa wilaya walieleza kuwa uchumi wa eneo hilo unategemea kwa kiasi kikubwa ufugaji na uvuvi katika Ziwa Kitangiri. Mkuu wa Wilaya alibainisha kuwa wilaya ina idadi kubwa ya mifugo lakini bado inakabiliwa na upungufu wa miundombinu ya kisasa kama machinjio, minada na majosho, pamoja na uhaba wa watumishi wa mifugo na uvuvi. Alisema hali hiyo imekuwa ikiwalazimu wananchi kutumia gharama kubwa kupata huduma na wakati mwingine kushindwa kufikia masoko yenye tija.

Afisa Uvuvi wa wilaya alieleza kuwa shughuli za uvuvi zinaendelea kufanyika licha ya changamoto za vifaa na rasilimali, akibainisha kuwa wilaya ina wavuvi hai 204, mitumbwi 34 iliyosajiliwa na boti moja pekee. Alisema bado kuna hitaji kubwa la kuimarisha usimamizi wa rasilimali za uvuvi, kutoa elimu ya uvuvi endelevu kwa wananchi na kuboresha miundombinu ya uvuvi ili kuongeza tija na kipato cha wavuvi.

Katika Wilaya ya Mkalama, Mkuu wa Wilaya Mhe.Moses Machali alisema migogoro ya wakulima na wafugaji imekuwa changamoto ya muda mrefu, hasa katika maeneo ya mipakani, akisisitiza kuwa kuwekwa kwa mipaka rasmi kati ya Wilaya ya Mkalama na Meatu ni hatua muhimu ya kudhibiti migogoro hiyo. Aliongeza kuwa kuna haja ya kulifufua shamba la mifugo la Serikali lililotelekezwa na kuvamiwa, ili kulinda mali ya umma na kutoa mfano wa ufugaji wa kisasa kwa wananchi.

Wananchi wa Kijiji cha Nyahaa walieleza kero zao kuhusu uvamizi wa mifugo, wizi na migogoro iliyosababisha majeruhi na hasara za mali, wakisisitiza umuhimu wa Serikali kuchukua hatua hatua za haraka kurejesha amani na kuimarisha ulinzi wa mifugo.

Kwa ujumla, wananchi walisema ziara hiyo imeongeza uwazi na matumaini mapya, huku viongozi wa wilaya na wataalamu wa sekta wakisisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya Serikali na wananchi ili kuboresha huduma za mifugo na uvuvi na kuchochea maendeleo ya kiuchumi katika mkoa wa Singida.





Friday, January 09, 2026

WANANCHI WAGUSWA NA KLINIKI YA HUDUMA ZA KISHERIA MKOANI SINGIDA

 


Posted on: January 9th, 2026

Wananchi Mkoani Singida,wamepongeza uzinduzi wa Kliniki ya Huduma za Msaada wa Kisheria uliofanyika Singida, wakisema hatua hiyo itarahisisha upatikanaji wa haki, kupunguza gharama za kufuata huduma za kisheria na kuongeza uelewa wa masuala ya sheria, haki za binadamu na utawala bora kwa jamii.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti, wananchi walisema kliniki hiyo imewapa fursa ya kupata msaada wa kisheria karibu na walipo, hususan kwa wananchi wa kipato cha chini ambao kwa muda mrefu wamekuwa wakishindwa kufikia huduma hizo kutokana na umbali na gharama. Walisema huduma hiyo itasaidia kutatua migogoro ya ardhi, ndoa, mirathi na masuala mengine ya kisheria yanayowakabili.

Katika uzinduzi huo, Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe.Dk. Juma Homera, alisema Wizara ina mpango wa kuandaa sera ya kitaifa ya msaada wa kisheria itakayoweka misingi ya kuboresha na kuimarisha utoaji wa huduma hiyo nchini, hatua itakayoongeza upatikanaji wa haki kwa wananchi wengi zaidi.

Dkt. Homera alisema maeneo yatakayoboreshwa ni pamoja na matumizi ya mifumo ya Tehama katika utoaji wa huduma za msaada wa kisheria, kuimarisha utatuzi wa migogoro kwa njia mbadala na kuweka mifumo madhubuti ya usimamizi ili huduma hizo zipatikane kwa urahisi na kwa wakati.

Alisema utekelezaji wa kampeni ya msaada wa kisheria umeleta mafanikio makubwa, ambapo tangu kuanza kwake wananchi 3,734,157 wamepatiwa elimu kuhusu masuala ya kisheria, haki za binadamu na utawala bora, jambo alilosema linaonesha umuhimu wa kuendelea na huduma hiyo kwa mwendelezo endelevu.

“Huduma ya msaada wa kisheria imekuwa endelevu na itaendelea kutolewa katika halmashauri zote. Serikali itaendelea kuimarisha huduma hizi ili wananchi wajitokeze na changamoto zao zipate ufumbuzi,” alisema Dk. Homera.

Aliongeza kuwa Serikali itaendelea kuanzisha na kuimarisha madawati ya msaada wa kisheria katika ngazi ya halmashauri zote nchini, akibainisha kuwa maafisa wa madawati hayo ni kiungo muhimu kati ya Serikali na wananchi katika kuhakikisha haki inapatikana kwa wakati.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe.Zainab Katimba, alisema halmashauri za wilaya zinapaswa kuweka utaratibu wa kuwawezesha maafisa wa madawati ya msaada wa kisheria ili waweze kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi zaidi, ikiwemo kuwapatia rasilimali na ushirikiano unaohitajika.

Alisema kwa sasa wapo maafisa 446 wa madawati ya msaada wa kisheria katika halmashauri mbalimbali nchini wanaoendelea kutoa huduma hizo, huku akisisitiza kuwa kuimarishwa kwa ushirikiano kati ya halmashauri, wizara na wadau wa huduma za kisheria kutapanua zaidi wigo wa upatikanaji wa haki kwa wananchi.
















Thursday, December 18, 2025

RC DENDEGO: "ARDHI NI DHAHABU YA MAENDELEO YA WANANCHI"


Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mhe. Halima Dendego, amewataka wananchi kutumia ardhi kama rasilimali ya kimkakati kwa maendeleo ya kiuchumi na kijamii, akisisitiza umuhimu wa kuitunza na kuitumia kwa tija. Kauli hiyo ameitoa wakati wa hafla ya kukabidhi hati zaidi ya 800 za umiliki wa ardhi kwa wananchi wa Kijiji cha Makunda, Wilaya ya Iramba, ikiwa ni sehemu ya mpango wa Serikali wa kuimarisha usalama wa ardhi na kupunguza migogoro ya umiliki.

Akizungumza katika hafla hiyo iliyofanyika Makunda, Mhe. Dendego amesema Serikali imeendelea kuweka mifumo ya kumuwezesha mwananchi kumiliki ardhi kihalali ili aweze kuitumia kama mtaji wa maendeleo. Ameeleza kuwa umilikishaji wa ardhi unalenga kuwawezesha wananchi kupata mikopo, kuongeza uzalishaji wa kilimo na kuimarisha ustawi wa familia, huku akisisitiza nidhamu ya matumizi sahihi ya ardhi.

“Ninawaomba wananchi, hati hizi ni heshima, ni haki na ni uchumi. Ardhi kila mwaka inaongezeka thamani; ardhi ndio dhahabu tuliyonayo mkononi. Msipate haraka ya kuuza ardhi yenu, itumieni kujijenga kiuchumi na kuboresha maisha ya familia zenu,” amesema Mhe. Dendego, akionya dhidi ya matumizi yasiyo ya maendeleo yanayoweza kuleta migogoro ya kifamilia na kijamii.

Aidha, Mkuu wa Mkoa amesisitiza kuwa Serikali itaendelea kusimamia matumizi bora ya ardhi kwa kushirikiana na viongozi wa vijiji, huku akihimiza wananchi kutumia hati kama dhamana ya mikopo ya maendeleo, kuwekeza katika kilimo cha mazao ya kimkakati ikiwemo alizeti, na kuhakikisha watoto wanapata elimu kwa wakati kama msingi wa maendeleo ya muda mrefu.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Mkalama, Mhe. Moses Machali, aliyekuwa Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Iramba, amesema kukabidhiwa kwa hati hizo ni hatua muhimu katika kumuwezesha mwananchi kushiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi. Amewataka wananchi kuzihifadhi hati zao sehemu salama na kuzitumia kuongeza uzalishaji katika kilimo na biashara ndogondogo.

Naye Kamishna Msaidizi wa Ardhi Mkoa wa Singida, Bi. Shamim S. Hoza, amesema Kijiji cha Makunda ni miongoni mwa vijiji 241 vilivyopo kwenye mpango wa matumizi bora ya ardhi katika Mkoa wa Singida. Amesema wanakijiji 899 wamenufaika na zoezi hilo, akibainisha kuwa lengo ni kupunguza migogoro ya ardhi na kuongeza thamani ya ardhi kama rasilimali ya uzalishaji.

Mwenyekiti wa Kijiji cha Makunda, Bw. Yesaya Daudi Seti, amesema umilikishaji wa ardhi utasaidia kuimarisha amani na mshikamano kwa kupunguza migogoro ya mipaka na kumwezesha mwananchi kuwekeza kwa uhakika. Ameishukuru Serikali kwa kuleta mpango huo na kuahidi usimamizi mzuri wa kumbukumbu za ardhi ngazi ya kijiji.

Baadhi ya wananchi waliopokea hati hizo wamesema hatua hiyo imewapa uhakika wa kisheria wa kumiliki ardhi na kuwapa fursa ya kupata mikopo ya maendeleo. Wamesema kupitia umilikishaji huo, wanatarajia kuongeza uzalishaji wa kilimo na kuboresha maisha ya familia zao.

Kwa ujumla, zoezi la kukabidhi hati za ardhi Makunda ni sehemu ya mkakati wa Serikali wa kuhakikisha ardhi inatumika kama nyenzo ya maendeleo, kupunguza migogoro ya umiliki na kuchochea uchumi wa wananchi wa Wilaya ya Iramba na Mkoa wa Singida kwa ujumla.



Wednesday, December 17, 2025

"MTEJA NI MFALME” — DKT. FATUMA MGANGA

 

Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida, Dkt. Fatuma Mganga, amewataka wahudumu wa afya mkoani Singida kuzingatia maadili, utu na kuwajali wananchi wanapotoa huduma za afya, akisisitiza kuwa mteja ndiye mhimili mkuu wa mafanikio ya utekelezaji wa Bima ya Afya kwa Wote. Ameyasema hayo wakati wa ufunguzi wa kikao kazi cha kujadili utekelezaji wa Bima ya Afya kwa Wote kilichofanyika katika Ukumbi wa Chuo cha Uhasibu Tanzania (TIA) mkoani Singida.

Akizungumza katika kikao hicho kilichowakutanisha waganga wafawidhi wa vituo vya afya mkoa wa Singida, Dkt. Mganga amesema Serikali inaanza utekelezaji wa bima hiyo kwa majaribio kwa makundi maalum, hivyo ni muhimu wahudumu wa afya kuwahudumia wananchi kwa weledi ili kila mmoja anufaike na mpango huo. Amesema huduma duni au lugha isiyofaa inaweza kuwakatisha tamaa wananchi na kudhoofisha lengo la Serikali la kuhakikisha huduma za afya zinapatikana kwa wote.

Dkt. Mganga amewataka pia wasimamizi wa huduma za afya kufanya marekebisho na kuboresha utoaji wa huduma katika vituo vya afya ili wananchi wasijutie kujiunga na mfuko wa bima ya afya, hususan kwa makundi maalum ambayo Serikali itayalipia gharama. Amesisitiza kuwa mazingira ya vituo vya afya yanapaswa kuboreshwa ili mwananchi anapofika ajisikie kuthaminiwa na kupata huduma stahiki.

Aidha, amezitaka taasisi za afya kuhakikisha zinalipa madeni yanayodaiwa na Bohari ya Dawa (MSD) kwa wakati, ili kuwezesha upatikanaji wa dawa, vifaa tiba na huduma muhimu zinazokidhi mahitaji ya wananchi. Amesema upatikanaji wa dawa na vifaa ni msingi wa utoaji huduma bora na mafanikio ya bima ya afya kwa wote.

Kwa upande wake, Mganga Mkuu wa Mkoa wa Singida amewataka wahudumu wa afya kuvaa mavazi rasmi yanayotambulika ili kuongeza uaminifu kwa wagonjwa na kuimarisha taswira ya sekta ya afya. Ameongeza kuwa matumizi ya lugha nzuri na yenye staha kwa wagonjwa ni msingi muhimu wa kudumisha uhusiano mzuri kati ya wahudumu wa afya na wananchi.

Kwa niaba ya waganga wafawidhi wote wa mkoa wa Singida, viongozi wa vituo vya afya wameahidi kutekeleza maagizo yaliyotolewa na Katibu Tawala wa Mkoa kwa kuboresha huduma za afya, kuongeza uwajibikaji na kuhakikisha vituo vinaingiza mapato yatakayosaidia kuendeleza huduma. Wamesema dhamira yao ni kuufanya Mkoa wa Singida kuwa mfano wa utoaji huduma bora za afya nchini Tanzania.

Kikao kazi hicho pia kimewakutanisha wadau mbalimbali wa sekta ya afya, wakiwemo wawakilishi wa NHIF, TIRA, MSD na taasisi nyingine, ambao waliwasilisha mada na maelezo kuhusu mwelekeo wa utekelezaji wa Bima ya Afya kwa Wote, hatua inayotarajiwa kuboresha upatikanaji na ubora wa huduma za afya kwa wananchi wote.