Monday, June 29, 2026

BAJETI YA 2026/2027 NI SILAHA YA KUPAMBANA NA UTAPIAMLO SINGIDA



  Katika kuhakikisha Mkoa wa Singida unaendelea kupiga hatua katika kupunguza utapiamlo na kuimarisha afya ya jamii kama msingi wa maendeleo endelevu, Kamati ya Lishe ya Mkoa imeelekeza kuwa bajeti ya mwaka wa fedha 2026/2027 iwe chombo cha msingi cha kuimarisha utekelezaji wa afua za lishe kwa matokeo yanayopimika.



Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida na Mwenyekiti wa Kamati ya Lishe ya Mkoa, Dkt. Fatuma Mganga, ameitaka Serikali na wadau wote wa maendeleo kuhakikisha bajeti ya mwaka wa fedha 2026/2027 inatoa kipaumbele kwa afua za lishe, akisisitiza kuwa vita dhidi ya utapiamlo haviwezi kushindwa bila uwekezaji wa makusudi katika mipango na matumizi ya fedha.



Akifungua kikao cha Kamati ya Lishe ya Mkoa wa Singida cha robo ya Januari–Machi 2026 kilichofanyika Juni 30, 2026 katika Ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Dkt. Mganga amesema lishe si suala la sekta ya afya pekee, bali ni agenda ya maendeleo inayohitaji ushiriki wa sekta zote ili kujenga jamii yenye afya, nguvu kazi yenye tija na uchumi imara.



Amesema Mkoa wa Singida umeendelea kupata mafanikio katika kupunguza udumavu kwa watoto kutoka asilimia 29 hadi asilimia 25.7, lakini akasisitiza kuwa kiwango hicho bado ni kikubwa na kinahitaji hatua za haraka kupitia utekelezaji wa bajeti yenye matokeo. "Bila uwekezaji wa makusudi kwenye lishe, hatutafikia jamii yenye tija inayotarajiwa katika Dira ya Taifa ya Maendeleo," amesema.



Dkt. Mganga ameelekeza kuwa bajeti ya mwaka 2026/2027 izingatie utekelezaji wa Mpango Jumuishi wa Lishe kwa kuongeza fedha za ufuatiliaji wa watoto wenye utapiamlo, upatikanaji wa virutubisho, elimu ya lishe kwa jamii, huduma za lishe kwa mama na mtoto pamoja na kuimarisha huduma hizo katika ngazi ya kata na vijiji.



Aidha, amesisitiza kuwa kila sekta inapaswa kuwa na mchango unaopimika katika kuboresha hali ya lishe, huku akiitaka Serikali za Mitaa kutenga bajeti mahsusi kwa ajili ya kampeni za lishe shuleni, afya ya mama na mtoto pamoja na kuimarisha ushirikiano kati ya sekta za afya, elimu na kilimo ili kuongeza upatikanaji wa chakula bora na salama.



Amesema Kamati ya Lishe ya Mkoa itaendelea kusimamia kwa karibu utekelezaji wa viashiria vya lishe, huku akisisitiza kuwa taarifa za utekelezaji zinapaswa kuonesha matokeo halisi kwa wananchi badala ya kuishia kwenye takwimu pekee.



Wajumbe wa Kamati ya Lishe kwa upande wao wameeleza kuwa kuingizwa kwa afua za lishe katika bajeti ya mwaka 2026/2027 kutasaidia kupunguza mzigo wa magonjwa yanayotokana na utapiamlo, kuongeza tija ya nguvu kazi na kuharakisha maendeleo ya kiuchumi na kijamii katika Mkoa wa Singida.



Kikao hicho kilihitimishwa kwa azimio la kuhakikisha bajeti ya mwaka wa fedha 2026/2027 inakuwa bajeti ya matokeo katika sekta ya lishe, kwa lengo la kuharakisha mapambano dhidi ya utapiamlo, kuboresha afya ya mama na mtoto na kujenga jamii yenye afya, uzalishaji na maendeleo endelevu.






















Sunday, March 08, 2026

SINGIDA WAWEKA MIKAKATI KUBORESHA LISHE KWA VIJANA.

Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mhe.Halima Dendego, ameitaka jamii pamoja na viongozi wa ngazi mbalimbali kuongeza juhudi katika kuhamasisha lishe bora kwa vijana ili kuimarisha afya na ustawi wa kizazi cha sasa na kijacho mkoani humo.

Akizungumza katika kikao cha Kamati ya Ushauri ya Mkoa (RCC) kilichofanyika Machi 8, 2026 katika ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Singida, Dendego alisema ni muhimu kwa wadau wote kushirikiana kuhakikisha vijana wanapata chakula cha kutosha na chenye virutubisho muhimu kwa maendeleo yao ya kimwili na kiakili.

Kikao hicho kilihudhuriwa na viongozi wa serikali pamoja na wataalamu wa afya ambao waliwasilisha taarifa kuhusu hali ya lishe kwa vijana mkoani humo.

Akiwasilisha taarifa hiyo, Mganga Mkuu wa Mkoa wa Singida, Victorina Ludovick, alisema tathmini iliyofanyika inaonesha umuhimu wa kuendelea kuimarisha mikakati ya lishe bora kwa vijana wa umri wa miaka 15 hadi 19 ili kuwasaidia kufikia ukuaji wenye afya njema.

Alieleza kuwa juhudi zaidi zinahitajika kuhakikisha vijana wanapata chakula cha kutosha wakiwa shuleni na hata wanapokuwa nyumbani, hali itakayosaidia kuimarisha afya zao na uwezo wao wa kujifunza.

Akizungumzia suala hilo, Dendego alisisitiza umuhimu wa jamii kuendelea kuhamasishana kuhusu lishe bora ili kuhakikisha vijana wanapata chakula chenye virutubisho vinavyohitajika kwa maendeleo yao.

“Ni wajibu wetu sote kuendelea kuelimishana na kuhamasishana ili vijana wetu wapate lishe bora. Hii itasaidia kujenga kizazi chenye afya na nguvu ya kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya familia na taifa,” alisema Dendego.


Aliongeza kuwa lishe bora ina mchango mkubwa si tu katika ukuaji wa mwili bali pia katika afya ya muda mrefu na ustawi wa vijana wanapokuwa watu wazima.

Aidha, aliwataka wazazi na walezi kuwahamasisha vijana kula vyakula vyenye lishe bora na kupunguza utegemezi wa vyakula visivyo na virutubisho vya kutosha.

Kwa upande wake, Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida, Fatuma Mganga, aliwahimiza wazazi kuwafungashia watoto chakula wanapoenda shuleni ili kuwasaidia kupata lishe bora wakati wa masomo.

Alisema hatua hiyo itawasaidia wanafunzi kupata nishati na virutubisho vinavyohitajika ili kuendelea na masomo yao kwa ufanisi.

Naye Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Singida (Ilongero), Eliya Dighah, alisisitiza umuhimu wa viongozi katika maeneo yao kuendelea kutoa elimu ya lishe kwa vijana ili kuwasaidia kufanya maamuzi sahihi kuhusu vyakula wanavyotumia.

Katika kikao hicho pia ilisisitizwa kuendelea kuimarisha utekelezaji wa Mkataba wa Lishe katika ngazi ya halmashauri pamoja na kuhakikisha rasilimali zinazotengwa kwa ajili ya lishe zinatumika ipasavyo ili kuimarisha afya ya wananchi, hususan vijana.


Monday, March 02, 2026

WATUMISHI WA UMMA WATAKIWA KUANDAA BAJETI JUMUISHI.

 

Watumishi wa umma wametakiwa kuandaa bajeti zitakazogusa wanufaika wa jinsi zote kwa usawa, hususan makundi maalumu wakiwemo wazee, wanawake na watu wenye ulemavu, ili kuhakikisha maendeleo jumuishi katika jamii.

Wito huo umetolewa na Katibu Tawala wa Mkoa wa Morogoro , Dkt. Mussa Ali Mussa, wakati akiwa mgeni rasmi katika kikao kazi cha maandalizi ya bajeti yenye mrengo wa kijinsia kilichowakutanisha Maofisa Maendeleo ya Jamii, Katibu Tawala Msaidizi sehemu ya Afya, Mipango na Uratibu, Sehemu ya Biashara na Uwekezaji pamoja na Maafisa Habari wa Mikoa.

Kikao hicho kinafanyika mkoani Morogoro kwa siku mbili kuanzia tarehe 2 hadi 3, 2026, kikilenga kuwajengea washiriki uwezo wa kuandaa na kutekeleza bajeti zinazozingatia mahitaji ya makundi yote katika jamii.

Dkt Mussa amesema ni muhimu katika uandaaji wa bajeti hizo kushirikiana na makundi maalumu ambayo ni mahsusi kwa ajili ya bajeti hiyo ili kupata mawazo na vipaumbele kutoka kwao ikiwemo mahitaji yao kwa wakati husika sambamba na miradi wanayoipa kipaumbele na ambayo wanaweza kuifanyia kazi kwa muda mfupi na kuwapa mafanikio.

Kadhalika amewataka viongozi hao kuwa mstari wa mbele kwa kuhakikisha wanawaunga mkono wanufaika wote wa Mikopo ya asilimia kumi kwa kununua bidhaa zao ikiwemo mchanga,kokoto mawe katika matumizi ya ujenzi wa majengo ya serikali na mengineyo kwa lengo la kuwaongezea kipato,ari ya kufanya kazi kwa bidii sambamba na kuwawezesha kurejesha mikopo yao kwa wakati unaotakiwa na kuweza kukopa kwa awamu nyingine.

Bi.Lilian Liundi, mwezeshaji wa mafunzo ya bajeti yenye mrengo wa jinsia kutoka NIRAS, aliwasilisha mada mbalimbali kwa wajumbe wa kikao hicho ikiwemo mafunzo ya uelewa wa jinsi na jinsia,mahitaji ya msingi na ya kimkakati ya jinsia,kadhalika jinsi ya kutengeneza bajeti yenye mrengo wa kijinsia katika jamii yenye tamaduni imara zinazokinzana na sera za usawa wa kijinsia.

Kadhalika aliwasilisha mada ya nyenzo zinazopaswa kutumika katika uandaaji wa bajeti yenye mrengo wa kijinsia ikiwemo Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania , Dira ya Taifa 2050,Sheria ya fedha,Sheria ya Ununuzi,na nyinginezo.


Kwa ujumla, mafunzo hayo yanatarajiwa kuleta matokeo chanya kwa kuongeza usawa na ujumuishi katika utoaji wa huduma za umma, kuboresha upangaji wa vipaumbele kulingana na mahitaji halisi ya makundi maalumu, kuimarisha utekelezaji wa sera na sheria za kitaifa, kuongeza kipato kwa wanufaika wa mikopo ya asilimia kumi, kuimarisha uwajibikaji na ushirikiano wa wadau wa maendeleo, kubadili mitazamo hasi ya kijamii kuhusu masuala ya kijinsia, pamoja na kuongeza tija na mafanikio ya miradi ya maendeleo katika jamii.

Thursday, February 12, 2026

"WATOTO WANAOPATA LISHE WANAFANYA VIZURI DARASANI" MWL. BULENGA

Wazazi na walimu wameaswa kudumisha ushirikiano wa karibu ili kuhakikisha elimu bora inaendelea kutolewa shuleni na kuleta matokeo chanya kitaaluma. Rai hiyo imetolewa leo tarehe 12 Februari 2026 na Afisa Elimu Mkoa wa Singida, Bw. Makwasa Dulenga, wakati akishiriki mahafali ya kidato cha sita yaliyofanyika katika Shule ya Sekondari Ndago mkoani Singida.

Mwl. Makwasa Dulenga akitoa hotuba kwa wahitimu Shule ya Sekondari Dago wilayani Mkalama.

Akizungumza katika hafla hiyo, Bw. Makwasa amesema mafanikio ya kitaaluma shuleni yanategemea mshikamano wa wadau wote wa elimu, hususan wazazi na walimu wenyewe. Amefafanua kuwa ushirikiano huo hujidhihirisha kupitia hatua mbalimbali ikiwemo uhamasishaji wa utoaji wa chakula shuleni, ufuatiliaji wa maendeleo ya wanafunzi na michango ya hiari inayowawezesha walimu wanaojitolea kuendelea kutoa huduma bora ya ufundishaji.

Aidha, amewataka wazazi na walezi kuhakikisha watoto wao wanapata lishe bora wakiwa shuleni, kwa kuwahimiza kuchangia chakula shuleni akisisitiza kuwa kuna uhusiano wa moja kwa moja kati ya lishe bora na ufaulu mzuri darasani. Amesema mwanafunzi anayepata chakula chenye virutubisho muhimu shuleni huwa na uwezo mkubwa wa kuzingatia masomo na kufanya vizuri katika mitihani.

Vilevile, Afisa Elimu amewahimiza wanafunzi kuendelea kuthamini fursa ya elimu kwa kujituma zaidi katika masomo yao, akibainisha kuwa wazazi na walezi wao wanajitoa kwa hali na mali kuhakikisha wanawapatia mahitaji muhimu ya shule ikiwemo sare na vifaa vya kujifunzia ili kuwajengea msingi bora wa maisha ya baadaye.


Awali akiwasilisha taarifa fupi ya shule hiyo, Mkuu wa Shule ya Sekondari Ndago, Bi. Prisca T. Msemo, amesema wanafunzi wa kidato cha sita wanaohitimu wameonyesha kiwango kizuri cha maandalizi kitaaluma kupitia mitihani mbalimbali ya majaribio waliyoifanya, ikiwemo mtihani wa utimilifu (Mock) wa Mkoa wa Singida. Ameeleza kuwa katika matokeo ya mtihani huo, shule ilishika nafasi ya tano kati ya shule 27 za mkoa, ambapo wanafunzi 54 walipata daraja la kwanza, wanafunzi 13 daraja la pili na mwanafunzi mmoja daraja la tatu, matokeo ambayo yanaonesha juhudi za walimu na wanafunzi pamoja na mazingira mazuri ya ufundishaji na ujifunzaji yaliyopo shuleni hapo.



Kwa upande wa baadhi ya wazazi waliohudhuria mahafali hayo wameipongeza hotuba ya mgeni rasmi na kuahidi kuendeleza ushirikiano katika malezi na elimu ya watoto wao. Wamesema wataendelea kuhakikisha wanafunzi wanapata mazingira mazuri ya kusoma ili waweze kufikia ndoto zao za kuendelea na masomo ya ngazi za juu. "Mgeni rasmi umesema maneno mazuri sana, umewahusia vijana wetu na sisi wazazi umetuhusia, basi tutashirikiana na walimu wetu. Pia nawashukuru walimu kwa kuwalea watoto wetu na ninyi watoto wetu bado kuna hatua huko mbele hivyo jitahidini katika masomo yenu sisi tuko pamoja na walimu wenu." Amesema mmoja katika wazazi.


Nao wanafunzi wa kidato cha sita wa Shule hiyo wamewashukuru walimu wao kwa malezi bora ya kitaaluma na kimaadili waliyoyapata katika kipindi chote cha masomo yao shuleni hapo. Wamesema juhudi, moyo wa kujitolea na ufuatiliaji wa karibu kutoka kwa walimu wao umekuwa chachu ya maendeleo yao darasani na nje ya darasa. Aidha, wameahidi kuwa watajituma kwa bidii katika mitihani yao ya mwisho ili kufanya vizuri zaidi na kuendeleza rekodi ya ufaulu wa shule hiyo, huku wakisisitiza kuwa wataendelea kuitunza heshima ya shule yao kwa matokeo mazuri yatakayodhihirisha ubora wa elimu waliyoipata.