Sunday, March 16, 2025

"MNARA WA MAWASILIANO KUCHOCHEA MAENDELEO IRAMBA":DKT MGANGA


Kijiji cha Mbelekesye kilichopo Wilayani Iramba Mkoani Singida kimeendelea kunufaika na mawasiliano ya uhakika yenye tija katika nyanja za kiuchumi kutokana na uwepo wa mnara wa mawasiliano kijijini hapo

Hayo yameshuhudiwa leo baada ya Kamati ya Bunge kufika kukagua ujenzi na utendaji kazi wa mnara huo uliojengwa na mtandao wa Yas kwa ruzuku ya Tshs 124,235,000 kwa usimamizi wa Mfuko wa Mawasiliano kwa Umma UCSAF.

Akizungumza katika hafla hiyo,Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida Dkt.Fatuma Mganga amesema uwepo wa mnara huo utarahisisha mawasiliano baina ya watu,lakini pia huduma za kifedha zitakua rahisi sana kwani wananchi watakua huru kufanya miamala ya kifedha katika benki tofauti bila kutembea umbali mrefu kufika kwa mawakala au katika mashine za ATM.

Kadhalika,ameomba ushirikiano kutoka kwa wananchi kwa kuhakikisha mnara huo unatunzwa vizuri katika kuhakikisha unadumu ili kutoa huduma nzuri kwa jamii.

Naye Mbunge wa Busega,Simiyu ametoa pongezi kwa wananchi wa Mbelekyese kwa utayari wao wa kutoa eneo la kuujenga mnara huo ambao utakwenda kuwa nguzo kuu katika nyanja ya mawasiliano.Pia ameshauri uwepo wa mitandao mingine katika mnara huo mmoja kwa lengo la kukidhi mahitaji ya wananchi ambao wanatumia mtandao zaidi ya mmoja 

Hamady Nkungu,mkazi wa Kijiji cha Mbelekesye wilayani Iramba ameonyesha kufurahia kuzinduliwa kwa mnara huo ambao amesema unakwenda kuchochea maendeleo ya wananchi kiuchumi ambapo hapo awali yalikua ya taabu na kuzorotesha maendeleo yao ikiwemo kukosa masoko ya bidhaa zao mbalimbali za kilimo na ufugaji.

"Kwa sasa imekua rahisi kupata wateja wa mazao na mifugo yetu kwasababu mawasiliano ya uhakika yanatoweka karibu sana na wanunuzi tofauti na hapo nyuma ambapo tulitumia muda mwingi kutafuta wateja na kutumia muda kidogo katika shughuli za uzalishaji mali"amesema Nkungu.

Kuzinduliwa kwa mnara huu ni utekelezaji wa kujenga minara mingine 758 hapa nchini ambayo itawasaidia wananchi kuingia katika mfumo wa uchumi wa kidigitali.Lengo likiwa ni kupata taarifa muhimu za kukuza uchumi kama vile taarifa za pembejeo za kilimo na mifugo na mengineyo.








Saturday, March 15, 2025

SINGIDA NI SALAMA,WANAMICHEZO KARIBUNI MEI MOSI

Kikao hicho kimefanyika leo Machi 14,2025 katika ukumbi wa Mkuu wa Mkoa wa Singida kwa agenda kuu ya kujiandaa kimichezo katika sherehe za Mei Mosi ambapo michezo inatarajiwa kuanza wiki mbili kabla ya kilele cha maadhimisho.

Akizungumza kwa niaba ya Katibu Tawala wa Mkoa,Dkt Victorina Ludovick -Mganga Mkuu wa Mkoa,pia amewatahadharisha washiriki juu ya ugonjwa wa M-POX kwa kuwaasa kujilinda dhidi yake kwa kufuata taratibu zote za kujikinga,Pia amewahakikishia wageni na wakazi wa Singida kuwa Singida ni salama dhidi ya ugonjwa wa MPOX akiwakaribisha kushiriki na kusherehekea MEI MOSI kwa amani na utulivu Mkoani Singida.




















Video:



Sunday, December 01, 2024

"SINGIDA TUJILINDE NA MAAMBUKIZI MAPYA YA VVU NA UKIMWI":DC GONDWE

Hayo yamesemwa na Mkuu wa Wilaya ya Singida Leo hii katika maadhimisho ya siku ya UKIMWI duniani Disemba Mosi,2024 amemuwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe.Halima Dendego yakiyoadhimishwa katika Halmashauri ya Manispaa ya Singida katika chuo Cha uhasibu kampasi ya Singida.

Akizungumza katika maadhimisho hayo,ametoa wito Kwa vijana kupima afya zao ili kuweza kuziishi ndoto zao nyingi huku akiwasisitiza wanandoa kuwa waaminifu ili kuepuka ongezeko la maambukizi huku akisisitiza tohara Kwa wanaume kama njia mojawapo ya kuzuia magonjwa Kwa wanaume

"Wanandoa wawe waaminifu Kwa wenza wao,pia ni vema kuwapenda,kuwajali na kuwahudumia waathirika WA VVU.Pia ni vema vijana wakaacha tamaa za maisha mazuri ili kuepuka vishawishi ambavyo vinasababisha kujiingizia katika vitendo vinavyoweza kupelekea kupata VVU,kuepuka hilo ni vema kuishi katika uhalisia WA maisha Yao na kupambania ndoto zao za baadae".amesema Gondwe.

Dkt.Said Mgeleka ambaye ni Meneja wa Mradi kutoka USAID amesema kwasasa dawa za kufubaza virusi vya UKIMWI zinapatikana Kwa urahisi na Kwa wingi tofauti na miaka ya nyuma ambapo iliwalazimu watu wa makundi maalum pekee kama wamama wajawazito wakati WA kujifungia pekee na wagonjwa wale ambao CD4 zao zilianza kushuka na kusumbuliwa na magonjwa nyemelezi ndio waliokua wakipata dawa hizo kutokana na uchache wa dawa uliosababishwa na ufinyu WA bajeti 

"Kwasasa dawa za ARV zinapatikana katika ngazi zote sio tu katika hospitali za mikoa na Taifa Bali mpaka katika zahanati zote vijijini kwani tangu 2016 juhudi za Serikali na wadau zimewezesha utoaji wa dawa hizo Kwa yeyote yule atakayegundulika na maambukizi bila Kujali wingi wa CD4 au dalili yeyote ya magonjwa nyemelezi"amesema Dkt.Mgeleka

Amesema pia kwasasa huduma za kinga dhidi ya VVU zimeongezwa Kwa kuleta dawa kinga Kwa watu wote walio katika hatari ya kuambukiza au kupata VVU,Pia kwasasa ni rahisi kupima wakati wowote na mahali popote na Kwa usiri kwani vifaa vya kujipima maambukizi vinapatikana kwa wingi na sio katika vituo vya afya pekee kama wakati wa nyuma.

Amini Nyaungo ni mmoja wa vijana ambao wamejitokeza katika maadhimisho haya amesema kuwaa ameitumia siku hii vema Kwa kupima afya yake pia kupata elimu juu ya VVU NA UKIMWI ambayo ataiwasilisha pia Kwa vijana wengine ambao hawana uthubutu katika kupima na kupata elimu ya VVU na UKIMWI.

"Nitaitumia fursa hii Kwa kuwapa vijana wenzangu elimu juu ya VVU,pia ntawaekimiaha kuhusu matumizi ya dawa kinga Kwa lengo la wao kufahamu Nini wafanye pale ambapo wanaona kuwa wapo katika hatari ya kupata VVU na matumizi Sahihi ya ARV Kwa wale ambao wamegundulika kuathirika na ugonjwa huu ila wana hofu ya kuanza kutumia dawa za kufubaza virusi"alisema Nyaungo.

Maadhimisho hayo yametanguliwa na maandamano mapema asubuhi,ikifuatiwa na huduma ya kupima afya(VVU NA UKIMWI) na mjadala kuhusu UKIMWI na vijana jinsi gani watajilinda na maambukizi au jinsi gani ya kuepuka kuambukiza wengine VVU. 

Kaulimbiu ya maadhimisho haya mwaka huu ni "CHAGUA NJIA SAHIHI TOKOMEZA UKIMWI"




Thursday, October 03, 2024

RC DENDEGO AZIAGIZA HALMASHAURI KUFIKISHA FURSA MIKOPO YA 10% KWA WALENGWA MPAKA VIJIJINI.

Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe. Halima Dendego, ameagiza Halmashauri zote mkoani humo kuhakikisha mikopo ya asilimia 10 inawafikia walengwa hadi vijijini ikiwa ni pamoja na akina mama, vijana, watu wenye ulemavu, na wazee ili kuimarisha uchumi wa wananchi na kusaidia maendeleo hadi ngazi za vijiji. RC Dendego ametoa agizo hilo kwenye mkutano wa Programu ya Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi "IMARISHA UCHUMI NA MAMA SAMIA (IMASA)" iliyofanyika katika ukumbi wa mikutano RC Social uliyopo Singida Mjini Octoba 3, 2024.

Kwaupande wake, Katibu Tawala Mkoa wa Singida Dkt. Fatuma Mganga, amepongeza na kumshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuridhia mikopo ya asilimia 10 kupatiwa makundi ya akinamama, vijana, watu wenye ulemavu na wazee huku akiwataka kutumia fursa za mikopo hiyo kwenda kuanzisha viwanda vidogo vya uzalishaji nishati mbadala akisisitiza kuwa hatua hii itachangia katika kukuza uchumi wa mkoa na kuboresha maisha ya wananchi.

Ameeleza kuwa nishati mbadala ni muhimu katika kuimarisha maendeleo endelevu na kupunguza utegemezi wa nishati ya kawaida.

Sunday, September 29, 2024

RC SINGIDA, Apongeza Wawekezaji wa Ndani Kuimarisha Sekta ya Viwanda vya Mafuta, Pamba na Kuleta Ajira kwa Vijana.

Mkuu wa Mkoa wa Singida, Halima Dendego, amewapongeza wawekezaji wa ndani hasa katika sekta ya viwanda vya mafuta ya kupikia, Mount Meru Mellers LTD, Singida Fresh Oil Mill na kiwanda cha Pamba cha Biosustain vilivyopo mkoani Singida akisema uwepo wa uwekezaji huo unaipunguzia Serikali mzigo wa kuagiza mafuta ya kupikia kutoka nje na kuleta ajira kwa vijana.


RC Dendego, ametoa pongezi hizo Septemba 28, 2024 katika ziara yake ya kutembelea viwanda katika halmashauri ya Manispaa ya Singida ambapo amesema, uwekezaji katika viwanda vya mafuta utasaidia serikali katika kutimiza lengo lake la kuzalisha mafuta ndani ya nchi.

Akizungumzia kiwanda cha Singida Fresh Oil Mill, Dendego amekiri kupokea taarifa ya kuwa asilimia 95 ya ukamilishaji mradi huo tayari umefikiwa na zaidi ya watu 200 wanatarajiwa watapata ajira, hii ni kuunga mkono serikali katika juhudi za kuleta maendeleo katika mkoa wa Singida na taifa kwa ujumla.

Mkurugezi Mkuu wa Kiwanda cha kukamua mafuta cha Singida Fresh Oil Mills Khalid Omary (kulia) akimweleza jambo Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe. Halima Dendego (mwenye kilemba) wakati wa ziara ya kutembelea viwanda katika Manispaa ya Singida. kushoto ni Mkuu wa Wilaya ya Singida Godwin Gondwe.

"Sisi Serikali ya mkoa wa Singida tutahakikisha tunawezesha mazingira mazuri kwa wawekezaji na changamoto zenu tunazishughulikia. Pia nimefurahishwa jinsi wageni wanavyokuja na teknolojia mpya na kuwaachia ujuzi huo utawasaidia vijana kupata ajira". RC Dendego

Aidha, Mkuu huyo wa Mkoa amesema kuwa Mkoa wa Singida ni miongoni mwa wazalishaji wakubwa wa mazao ya kilimo, hususan mbegu za mafuta ya alizeti hivyo ametoa wito kwa wakulima mkoani humo kuzalisha kwa wingi ili kukidhi mahitaji.

Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe. Halima Dendego akizungumza na uongozi wa kiwanda cha Singida Fress Oil Mill (hawapo pichani) mara baada ya kutembelea kiwanda hicho.

Pia RC Dendego,, ameahidi kuwa serikali ya mkoa itahakikisha malighafi zinapatikana ili mafuta yazalishwe kwa wingi huku akiwataka wawekezaji wa viwanda vidogo kuhakikisha wanazalisha mafuta safi na salama kwa matumizi ya binadamu.

Hata hivyo, Dendego amewashukuru wawekezaji hao wa viwanda kwa ushirikiano kwa serikali na jamii kwa kuwa unaleta manufaa makubwa ikiwa ni pamoja na upatikanaji wa maji safi, ujenzi wa shule, na msaada katika kukabiliana na majanga.

Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe. Halima Dendego (wapili kutoka kushoto) akizungumza na Mkurugenzi wa Kiwanda cha kukamua mafuta ya Alizeti Mount Meru Millers kilichopo Singida mjini wakati wa kutembelea kiwanda hicho.

Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe. Halima Dendego akionyesha moja ya bidhaa ya sabuni inayozalishwa na kiwanda cha kukamua mafuta ya alizeti Mount Meru Millers wakati alipotembelea kiwanda hicho. 
kulia ni Mkuu wa Wilaya ya Singida Godwin Gondwe.




Ziara ikiendelea katika kiwanda cha kukamua mafuta ya alizeti SINGIDA FRESH OIL MILL kilichopo Singida Mjini.

Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe. Halima Dendego akipokea maelezo mafupi kutoka kwa viongozi wa kiwanda cha Pamba Biosustain kuhusu mchakato wa uzalishaji wakati alipotembelea katika kiwanda hicho kilichopo Singida Mjini, Septemba 28, 2024.


Muonekano wa magunia ya Pamba ambayo imezalishwa na kiwanda cha biosustain tayari kwa ajili ya kusafirisha.

Friday, September 27, 2024

RC Dendego Akutana na Watendaji wa Halmashauri ya Iramba: Atoa Maagizo kwa Wakuu wa Idara na Kusisitiza Uwajibikaji.


Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe. Halima Dendego, mapema leo (Septemba 27, 2024) amekutana na Watendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Iramba lengo kuu likiwa ni kuboresha utendaji kazi wa watumishi katika halmashauri hiyo ili waweze kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi.

Akizungumza kwenye kikao kazi kilichofanyia katika ukumbi wa mikutano wa Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Iramba, RC Dendego amewataka Wakuu wa Idara na Vitengo katika halmashauri hiyo kuhakikisha wanasimamia miradi yote ya maendeleo ili kukamilika kwa wakati, ubora na kwa thamani ya fedha pasipo kuzalisha madeni.

"Serikali inapoleta fedha za ujenzi wa mradi inakuwa imeshapiga mahesabu ya kukamilisha sasa ninashangaa iweje halmashauri nyingine mradi huohuo umekalimika kwa thamani ya fedha iliyoletwa nyie hamjakamilisha au umekamilika ila mmezalisha madeni, sitaki kusikia jambo hilo" RC Dendego

Mkuu huyo wa Mkoa amewasisitiza watendaji hao wa halmashauri kwa kila mkuu wa Idara kuweka mpango kazi wake kwa kufuata Ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) inavyoelekeza kwa kuhakikisha kuwa yale yanayotakiwa na ilani hiyo yanatekelezwa kikamilifu.

Aidha, katika kikao kazi hicho RC Dendego, amewaelekeza maafisa elimu wa halmashauri hiyo kuhakikisha wanapandisha hali ya taaluma kwa kiwango cha juu na kukomesha utoro wa wanafunzi kwa kuwa elimu ni msingi wa maendeleo ya taifa.

Katibu Tawala Mkoa wa Singida Dkt. Fatuma Mganga, akisisitiza jambo kwenye kikao kazi hicho.

Katika hatua nyingine Mkuu wa Mkoa huyo amewahimiza watendaji hao kushirikiana kikamilifu katika ukusanyaji na usimamizi wa mapato ya halmashauri akisema bila mpango wa kifedha unaoeleweka haiwezekani kufanikisha malengo ya halmashauri.

Akizungumza na Idara ya Utumishi amesema inawajibu wa kusimamia haki za watumishi na kuhakikisha kuwa masuala ya kiutumishi yanashughulikiwa ipasavyo ikiwa ni pamoja na matumizi bora ya teknolojia katika kurahisisha shughuli za kiutumishi.

Hata hivyo,  RC Dendego, ametumia kikao hicho kuwataka Wakurugenzi wa Halmashauri mkoani humo kutowahamisha watumishi bila idhini ya Katibu Tawala wa Mkoa (RAS) ili kudhibiti uhaba wa watumishi na kuweka uwiano bora katika utoaji wa huduma.

Pia RC Dendego, amewaagiza wakaguzi wa ndani katika halmashauri hiyo kuwa macho na kutoruhusu dosari zozote kutokea bila kuchukua hatua akisema kuwa hataki kusikia kwamba kuna jambo limegundulika lakini halijaripotiwa au kushughulikiwa.

Kwaupande wa Idara ya Afya RC Dendego, amewaagiza wahudumu wa afya kuongeza uangalizi wa hali ya juu pindi wanapokuwa kazini hasa wakati wa kutembelea wodi kujua changamoto za wagonjwa ili kutoa huduma bora.

Katika hatua nyingine Mkuu wa Mkoa huyo alihitimisha kwa kuwaonya viongozi kuwa hataki kuona halmashauri inarudi nyuma katika utekelezaji wa majukumu na maendeleo hususan katika usimamizi wa miradi, elimu, mapato huku akiwataka walimu na maafisa taaluma kuhakikisha kuwa wana mipango inayotekelezeka kwa manufaa ya elimu.


Tuesday, September 24, 2024

RAS Singida Aagiza Usimamizi Bora wa Miradi ya Ujenzi 2024/2025

Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida, Dkt. Fatuma Mganga, amewataka Wakurugenzi, Maafisa manunuzi, na Wahandisi wa mkoa huo kuhakikisha kuwa miradi yote inayotekelezwa inakamilika kwa wakati, kwa viwango vinavyotakiwa na kwa thamani sahihi ya fedha. 

Akizungumza kwenye kikao kazi na Watendaji wa Serikali kilichofanyi Septemba 24, 2024 katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa huo, Dkt. Mganga amesisitiza umuhimu wa kutoa huduma bora kwa wananchi kupitia usimamizi mzuri wa miradi ya serikali.

Dkt. Mganga amewasihi Wakurugenzi kuongeza umakini katika usimamizi wa rasilimali fedha za miradi inayotekelezwa katika halmashauri akisema Serikali inapoleta fedha inakuwa imeshafanya tathimini kwa kina kuhusu gharama za ukamilishaji wa miradi huku akiwasisitizia kuajili wakandarasi wenye uwezo na weledi ili kuepukana na makosa ya ujenzi na kuokoa muda wa ukamilishaji wa mradi.

Aidha, amewasisitiza Wahandisi wa halmashauri zote kusimamia kikamilifu mafundi wa ujenzi ili kuhakikisha miradi inajengwa kwa ubora na kukamilika kwa wakati. 

“Ni lazima kila mmoja afanye kazi yake kwa uzalendo na kujituma ili wananchi wapate huduma zinazostahili.” Dkt. Mganga

Pia, aliwataka maafisa manunuzi kufanya kazi kwa ufanisi na kufuatilia bei za soko kabla ya kuagiza vifaa vya ujenzi ili kuepuka gharama zisizo za lazima.

Hata hivyo amesisitiza kwamba maafisa manunuzi wanapaswa kupitisha malipo ya serikali kwa utaratibu sahihi, huku akionya kwamba hatua kali zitachukuliwa kwa wale watakaoshindwa kutekeleza wajibu wao kwa ufanisi. 

Akizungumzia makadirio ya vifaa, Dkt. Mganga amehimiza umuhimu wa kuhakiki wanafanya makadirio yanayotakiwa, badala ya kukadiria kwa wingi hadi vifaa kubaki hivyo amewataka kuwa na mipango sahihi ili kuhakikisha rasilimali za serikali zinatumika kwa ufanisi.

Akimalizia hotuba yake Katibu Tawala huyo wa mkoa amewataka Wakurugenzi kutowaachia walimu na wataalamu wa afya kusimamia miradi ya ujenzi ili kuepukana na uharibifu wa miradi ya ujenzi.