Sunday, July 06, 2025

AJALI YA MOTO SOKO KUU SINGIDA YATAFUTIWA UFUMBUZI


Posted on: July 6th, 2025

Serikali ya Mkoa wa Singida imeunda kamati ya kuchunguza na kufanya tathimini tukio la kuungua moto soko kuu la mjini Singida ili wafanyabishara waliopata janga hilo iangalie namna ya kuwasaidia.

Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mhe.Halima Dendego, akizungumza na wananchi na wafanyabishara leo baada ya kutembelea kukagua eneo la tukio, amesema kamati hiyo ifanya kazi hiyo kwa muda wa siku saba kuanzia leo.

Amesema kamati aliyoiunda itawajumuisha wafanyakazi wa serikali, Kamati ya Usalama ya Mkoa na mameneja wa benki zote zilizopo mkoani hapa na kwamba baada ya tathimini hiyo kazi ya kurejesha miundombinu ya soko hilo itaanza mara moja.

“Ndani ya kamati hizi kutakuwa na wataalam wa fedha,wataalamu wa biashara na wataalam wa afya pia kwani wenzetu wamepata mshtuko lazima tuwajue mmoja mmoja wapo wapi ili warejee katika hali salama na kazi hiyo inaanza leo na tumewapa siku saba wamalize kazi hiyo na sisi tutaanza kusafisha eneo hilo kwa ajili ya kujenga kwa haraka,” amesema.

“Naomba nitoe salamu za pole kutoka kwa Mhe.Rais Samia Suluhu Hassan,  tulimpa taarifa za awali na amenituma tukae mimi na kamati yangu kuweka kambi hapa ili tumjulishe uharibifu uliotokea hapa, lakini pia Waziri wa Tamisemi, Mhe.Mohamed Mchengerwa anawapa pole,” alisema Dendego.

Aidha,Dendego amekipongeza Kiwanda cha Pamba cha Biousastain na kiwanda cha Meru ambavyo vimeweza kusaidia kutoa vitendea kazi katika kufanikisha kazi ya kuzima moto.

Naye Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Singida, Martha Mlata, amewapa pole wafanyabiashara kwa janga hilo na kuwaahidi kwamba ana imani kubwa kuwa Serikali itarejesha miundombinu ya soko hilo ili shughuli za biashara ziendelee kama kawaida.

Kadhalika,Mlata amelipongeza Jeshi la Zimamoto na Ukoaji, Jeshi la Polisi na wananchi kwa jinsi walivyoweza kushirikia katika zoezi la uokoaji ambapo hakukuweza kutokea tukio la kupora mali za waathirika.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Singida, Godwin Gondwe, alisema ulinzi utaendelea kuimarishwa katika soko hilo ili uporaji woowote usiweze kufanyika.

Mwenyekiti wa Soko Kuu la Singida, Hassan Mboroo, alisema moto katika soko hilo ulianza kuwaka  saa 3:40 usiku wa kuamkia leo katika duka la kuuza vifaa vya ujenzi baadaye kuenea katika maduka mengine.

Amesema zoezi la kuuzima lilianza kufanyika muda huo na kufanikiwa kuuzima hapo baadae ambapo jumla ya maduka 15 yameteketea kwa moto zikiwamo bidhaa zilizokuwemo na kusababisha hasara kubwa kwa wafanyabiashara.

Mboroo alisema kufuatia tukio hilo kuna haja kwa serikali kuliboresha soko hilo kwa kuweka katika mpangilio mzuri ili kunapotokea majanga kama haya ya moto magari ya kuzimia moto yaweze kupita kwa urahisi kufanya kazi ya uokozi.

Monday, June 30, 2025

MAAFISA MAENDELEO KIKAANGONI,WAASWA KUJIPIMA KWA MATOKEO NA SIO IDADI YA VIKAO.


Posted on: June 30th, 2025

Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mhe. Halima Dendego, amesema kuwa Maafisa Maendeleo ya Jamii lazima wajipime kwa matokeo wanayoyaleta kwa wananchi na si kwa idadi yao au vikao wanavyohudhuria, akisisitiza kwamba kazi yao kuu ni kuifikia jamii na kuleta mabadiliko chanya.

Akizungumza katika kikao kazi cha Maafisa Maendeleo kutoka wilaya zote za Mkoa wa Singida kilichofanyika katika ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Mhe. Dendego amesema amefurahi kukutana nao kwa sababu ndiyo msingi mkubwa wa mafanikio ya wananchi katika ngazi ya jamii.

“Nimefurahi kukutana nanyi kwa sababu tuna mambo mengi ya kuyajadili ili kuhakikisha tunatekeleza mipango mbalimbali ya serikali na huduma zinawafikia wananchi. Tuhakikishe tunawafikia wananchi na tunawaelimisha, kwani haitakuwa na maana huduma hizi hazitawafikia,” amesema RC Dendego.

Ameeleza kuwa Maafisa Maendeleo wanapaswa kujitathmini kama kweli wanatekeleza wajibu wao ipasavyo na kuleta tija, badala ya kukaa maofisini wakisubiri wananchi wawafuate. “Ukiitwa Afisa Maendeleo, kila eneo linakuhusu. Tupimane kwa malengo yetu ili tulete tija kwa wananchi wetu,” amesisitiza.

Pia,Mkuu wa Mkoa amesema anaifahamu vyema taaluma hiyo kwa kuwa yeye mwenyewe ni mwana sayansi wa jamii, hivyo anajua namna ilivyo na jukumu kubwa katika kubadilisha tabia na ustawi wa wananchi. 

“Sisi tunahusika moja kwa moja na kurekebisha tabia za jamii, tunawajenga raia wema wa taifa hili,” amesema.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa Maafisa Maendeleo kuviunda vikundi, kuvisimamia, kuvilea na kuvifikisha kwenye taasisi za fedha, ili wanawake, vijana na watu wenye ulemavu waweze kupata mikopo na kujikwamua kiuchumi. “Tija sio uwingi wetu, tija ni namna tunavyoipeleka jamii mbele kwa vitendo,” amesema.

Ametumia kikao hicho kuwataka Maafisa Maendeleo waamke na waone kama wanatimiza malengo ya serikali.

 “Tupate ndoto ya kuwatoa wananchi wa Singida hapa walipo, tusibaki kusema hiki ni kikao kazi bila vitendo. Hiki ni kikao cha operation, kama kumponya mgonjwa, tupate suluhisho. Swali kubwa ni: namna gani mnaifikia jamii? Tuache kukaa tu ofisini, tufike field.”

Kadhalika Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida Daktari Fatuma Mganga amesema kuwa kikao hicho pia kina maazimio kadhaa cha kuhakikisha wanakwenda kujitathimini juu ya kwamba ni namna gani wameweza kuwafikia wananch na yapi ni matokeo ya wao kuwepo maeneo hayo ikiwa ni kuhakikisha wananchi wanaishi mazingira bora ikiwemo kuwa na vyoo bora,ukatili dhidi ya wanawake na watoto,mikopo ya wanawake na walemavu,fursa mbalimbali za wananchi kuwekeza,kadhalika dawati la huduma za msaada wa kisheria  ikiwa ni kwa namna gani wanatumia jukwaa hilo kuhakikisha wanashighulikia kero za wananchi na mengineyo mengi.

"Tunalo jukumu kubwa la kuhakikisha kuwa yale ambayo tumekasimiwa na Mhe.Rais,Wakurugenzi na viongozi wengine katika ngazi ya  Wilaya tunayafanyia kazi na yanaleta matokeo ili nasisi tuonekane kuwa tunafanya kazi yenye matokeo chanya katika jamii"amesema Daktari Mganga.

Kadhalika amesema kuwa moja ya azimio la kikao hicho ni kuhakikisha Maafisa hao wanakwenda kushuhulikia suala la marejesho ya fedha zote ambazo vikundi mbali mbali vilikopa ikiwemo mikopo ya asilimia kumi kwa lengo la kuhakikisha inawafikia wengine ambao hawajapata kadhalika kusimamia vema vikundi vilivyopo ili kupiga hatua kubwa zaidi za kiuchumi.

Kauli hizo zimekuja wakati Maafisa Maendeleo wakiwa kwenye mkutano wa pamoja kujadili changamoto zilizopo katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo, ikiwemo mikopo kwa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu, mikataba ya vikundi pamoja na namna ya kuhakikisha wanavifikia vikundi vyote vya jamii kwa usawa.

Ni katika majadiliano yao, Maafisa Maendeleo wamejadili changamoto zinazohusu utekelezaji wa kanuni mbalimbali ikiwemo mikopo kwa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu, pamoja na mikataba ya vikundi vya kukopeshwa ili kuhakikisha malengo ya serikali ya kuwainua kiuchumi makundi haya muhimu yanafanikiwa ipasavyo.

Kikao hicho kimetoa fursa kwa Maafisa Maendeleo kubadilishana uzoefu na kuja na mikakati ya pamoja itakayosaidia kuharakisha maendeleo katika jamii za Mkoa wa Singida.

Wednesday, June 25, 2025

WCF YAWASHIKA MKONO WENYE MAHITAJI MAALUM SINGIDA

 Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mhe. Halima Dendego, ametoa shukrani za dhati kwa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi - WCF (Worker's Compensation Fund) kwa kuonesha moyo wa huruma kwa watu wa Singida, hususan wenye mahitaji maalum. 

Ameyasema hayo leo Juni 25,2025 wakati wa hafla ya makabidhiano ya Vifaa saidizi kwa  wanafunzi wenye mahitaji maalumu katika Chuo cha Ufundi Stadi na Marekebisho kwa Watu Wenye Ulemavu Sabasaba mkoani Singida, 

Hafla hiyo imefanyika ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya miaka 10 ya WCF ambapo jumla ya viti mwendo 100 (viti maalum 10 na vya kawaida 90), fimbo nyeupe 154 na limu paper maalumu 200 vilikabidhiwa kwa uongozi wa chuo hicho.

Mhe.Dendego Ameongeza kuwa kitendo cha kuifanya Singida kuwa sehemu ya program hiyo ya WCF kwa watu wenye ulemavu kinaonesha upendo wa kweli, na kuongeza kuwa ofisi yake itaendelea kufuatilia na kushughulikia changamoto zote zilizotolewa na uongozi wa chuo hicho.

Katika salamu zake, Mhe. Dendego pia amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuendelea kumuamini kuiongoza Singida, akiahidi kuendeleza juhudi za kuhakikisha kila mwananchi ananufaika na fursa mbalimbali za maendeleo. Akikiri kuwa mchango wa taasisi kama WCF unathibitisha kuwa sekta ya hifadhi ya jamii ni mshirika halisi wa maendeleo ya mkoa.

Hata hivyo Mkurugenzi Mkuu wa WCF, Dkt. John Mduma, akitoa salaam zake ameeleza kuwa kuelekea kuadhimisha miaka 10 ya Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi - WCF (Worker's Compensation Fund) kwa kuwasaidia watu wenye ulemavu unatokana na mafanikio makubwa ya mfuko huo tangu kuanzishwa kwake huku akiahidi kuwa WCF itaendelea kuwekeza katika jamii kupitia sera yao ya kurudisha kwa jamii, ili kuhakikisha Watanzania wote, bila kujali hali zao, wananufaika na uwepo wa taasisi hiyo.

Kwa upande wake Mkuu wa Chuo hicho, Bi. Fatuma Malenga, ameeleza kuwa Taasisi hiyo ambayo inatoa mafunzo ya ushonaji, umeme na huduma za utengemano, kwa kupitia  msaada huo utasaidia wanafunzi kuwa na mazingira rafiki ya kujifunzia. Kadhalika ameahidi kuwa vifaa vilivyotolewa vitasimamiwa kwa weledi ili kutoa matokeo yanayotarajiwa kwa vijana hao.

Nao Wanafunzi wenye mahitaji maalum, wameonesha shukrani zao kwa WCF kwa msaada huo muhimu akiwemo Amina Mshana, mwanafunzi mwenye ulemavu wa miguu, amesema kiti mwendo alichopokea kitamrahisishia usafiri wa kila siku akiwa chuoni. Kadhalika Isack Edward, mwenye ulemavu wa macho, amepongeza upatikanaji wa fimbo nyeupe akisema sasa ataweza kusafiri kwa usalama zaidi. 

Zoezi hilo limeongozwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Mhe. Ridhiwani Kikwete  hafla ya makabidhiano ya vifaa saidizi ambaye ameeleza kuwa msaada huo utasaidia wanafunzi kujifunza kwa ufanisi na kujitegemea, huku akiwasihi walimu na watendaji wa chuo kuhakikisha vifaa hivyo vinatumika kwa malengo yaliyokusudiwa ili kutoa matokeo chanya kwa jamii.

Hafla hiyo imeonesha kwa vitendo namna taasisi za hifadhi ya jamii zinavyoweza kushiriki kikamilifu katika ujenzi wa jamii jumuishi na yenye usawa.

Tuesday, June 24, 2025

KAMATI YA MAADILI MKOANI SINGIDA IPO TAYARI KUWAHUDUMIA WANANCHI.


Posted on: June 24th, 2025

Jaji Mfawidhi Mhe.Dkt Juliana Masabo leo Juni 24,2025 ameapisha kamati ya maadili ya mahakimu ngazi ya Mkoa na Wilaya  tukio lililoshirikisha Wenyeviti,makatibu ,na wajumbe.

Tukio hilo limefanyika katika Ukumbi wa Mkuu wa Mkoa wa Singida huku Kamati zilizoapishwa ikiwa ni Wajumbe wa kamati ya Mkoa wa Singida,Wajumbe wa kamati ya Wilaya ya Singida,Iramba,Mkalama,Manyoni,Halmashauri ya Singida na Ikungi.

 Mhe.Dkt Masebo ametoa maagizo  kwa kamati hizo kuhakikisha wanakutana mara kwa mara ili kujengeana uwezo wa namna ya kushuhulikia kero za wananchi wanaoleta changamoto zao,kadhalika kuhakikisha vikao vinafanyika mara kwa mara kwa kuwaweka pamoja wajumbe wa Kamati ili kupeana miiko ya kamati yao na kuhakikisha wanakutana kila mwaka mara nne endapo kutakua hakuna malalamiko yeyote yanayowasilishwa.

Kadhalika ametoa wasilisho kwa wajumbe juu ya majukumu ya Kamati ya maadili ikiwemo namna kamati hizo zinafanya kazi katika namna ya uwasilishwaji na namna ya kushuhulikia malalamiko kwenye kamati ya Mkoa,upelelezi na utoaji wa  maoni.

Mhe.Moses Machali akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Singida,ameahidi kuwa Kamati hizo zitakwenda kufanya kazi kwa ushirikiano mkubwa ili kuweza kushughulikia vema malalamiko yote yanayowasilishwa na wananchi.

Kamati hizi zinaendeshwa kwa mujibu wa kanuni za mwaka 2023 zilizotengenezwa chini ya kifungu cha 66 cha Sheria ya Usimamizi wa Mahakama na zinahusika na uchunguzi wa tuhuma za ukiukwaji wa maadili dhidi ya Maafisa wa Mahakama.


Saturday, June 21, 2025

NDOTO YA SINGIDA KUWA KITUO CHA VIWANDA VYA KISASA TANZANIA KUTIM


Posted on: June 21st, 2025

Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe. Halima Dendego amesema kuwa Mkoa wa Singida umejipambanua kuwa kitovu cha viwanda vya kisasa nchini kupitia juhudi mbalimbali za kuboresha mazingira ya biashara, uwekezaji, na matumizi ya rasilimali zilizopo kikamilifu. 

Akizungumza katika Mkutano wa Baraza la Biashara la Mkoa wa Singida uliofanyika katika Ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Mhe. Dendego amesema kuwa Mkoa wa Singida umeendelea kuongeza idadi ya viwanda hadi kufikia 1,565 huku akibainisha kuwa viwanda vikubwa vimefikia 9, vya kati 11, vidogo 420 na vidogo sana 1,225 ambavyo kwa pamoja vinazalisha ajira kwa vijana na kuongeza mzunguko wa fedha kwa wananchi.

Amesema maendeleo haya ni matokeo ya mazingira bora yaliyowekwa na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambaye amekuwa mstari wa mbele kuhakikisha Tanzania inaingia katika uchumi wa viwanda kupitia uwekezaji wenye tija unaolenga kutumia rasilimali zinazopatikana katika kila mkoa. Ameongeza kuwa Mkoa wa Singida una rasilimali nyingi zikiwemo kilimo, madini, mifugo, na eneo zuri la kijiografia ambalo linaifanya Singida kuwa sehemu bora ya uwekezaji nchini.

Katika kuhakikisha kuwa viwanda hivyo vinaendelea kuzalisha kwa ufanisi, Mhe. Dendego amesema Serikali ya Mkoa imeweka mkazo mkubwa kwenye kilimo cha kisasa ambacho kinazalisha malighafi kwa ajili ya viwanda vya usindikaji. Aidha, amesema Mkoa unatarajia kuanza ujenzi wa soko la kimataifa la vitunguu kupitia mradi wa TACTIC kwa mwaka wa fedha 2025/2026, ambapo tayari mikataba imeshasainiwa.

 “Hii ni hatua kubwa ambayo itawainua wakulima wetu kwa kuwapatia soko la uhakika na kuongeza kipato chao kupitia thamani ya mazao wanayoyazalisha,” amesema Mhe.Dendego.

Kadhalika,ameongeza kuwa Serikali ya Mkoa inaendelea kuboresha mazingira ya uwekezaji kwa kushirikiana na taasisi kama TANESCO, TARURA, SUASA, na TANROADS katika kuhakikisha huduma za msingi kama umeme, maji, na barabara zinapatikana kwa urahisi katika maeneo yote ya Mkoa wa Singida. Amesema kuwa pamoja na fursa za kilimo, Mkoa pia una fursa kubwa katika sekta ya madini ikiwemo dhahabu, gypsum, shaba, aluminium na shaba nyeusi, na kwamba wawekezaji wanakaribishwa kuwekeza kwa wingi katika maeneo haya.

Kwa upande wake Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida, Dkt. Fatuma Mganga, akihitimisha mkutano huo, amewapongeza wajumbe wote kwa michango yao chanya iliyolenga kukuza uchumi wa mkoa. Amesema kikao hicho ni muhimu kwa kuwa uwekezaji na biashara ndiyo njia pekee ya kuzalisha fedha, siyo ajira pekee. Amewataka watumishi wa umma katika halmashauri kuwa na uelewa wa mazingira ya biashara ili kushirikiana kwa karibu na sekta binafsi katika kutengeneza mazingira rafiki ya uwekezaji.

 Dkt. Mganga amesema kuwa kikao hicho cha Baraza la Biashara kina umuhimu mkubwa kwa kuwa kinatoa majadiliano yatakayoleta maboresho ya mazingira ya biashara na uwekezaji akisema ni lazima taasisi za umma zichukue nafasi yake katika kuweka mazingira wezeshi kwa sekta binafsi ili kushirikiana katika uchumi. 

"Tukisikia tajiri mkubwa duniani hana ajira ya kawaida, wote ni wafanyabiashara. Biashara ndiyo njia pekee ya kuzalisha fedha. Wananchi wakizalisha fedha na sekta binafsi ikiongezeka, basi mzunguko wa fedha utaongezeka na ustawi wa jamii utaonekana," amesema.

Dkt. Mganga amesema mkoa umeweka kipaumbele katika kuhakikisha kuwa wakulima wanajiunga na vyama vya ushirika ili waweze kupata tija zaidi kwenye uzalishaji wao. Aidha, amepongeza juhudi za wakurugenzi wa halmashauri kwa kuboresha miundombinu na kuwafanya wawekezaji kuwa na mazingira rafiki ya kuwekeza huku akisisitiza kila halmashauri kutekeleza mpango wa kuwa na One Business Center ili wananchi wapate elimu ya biashara na uwekezaji kwa ukaribu zaidi.

Naye Katibu Tawala Msaidizi sehemu  ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara Bi. Donatila Vedasto ametoa taarifa ya hali ya biashara na uwekezaji katika Mkoa akisema kuwa Mkoa wa Singida una fursa nyingi sana ambazo zinahitaji kushirikiana kati ya sekta ya umma na sekta binafsi ili kuziwezesha kutumika ipasavyo.

 Amesema kuwa mpaka sasa kuna wafanyabiashara waliopo na wanaolipa kodi wapatao 10,400 waliopo kwenye makundi ya wakubwa, wa kati, na wadogo, huku machinga walioandikishwa ni 15,898. Amesema hatua hiyo inaonesha mwelekeo mzuri wa utayari wa wananchi kuingia kwenye sekta ya biashara.

Ameongeza kuwa sekta ya uwekezaji inahitaji msukumo zaidi kutoka kwa wawekezaji wa ndani hususan kwenye maeneo ya huduma kama Shopping Malls, Resting Places, na vitega uchumi vya halmashauri ili kuongeza mapato akibainisha kuwa Mkoa wa Singida umejipambanua kama mkoa tajiri wenye rasilimali nyingi za kuendeleza viwanda na biashara zenye tija kubwa kwa Taifa.

Wajumbe wa Baraza la Biashara wakiwemo kutoka sekta za madini, TRA, OSHA, COPRA na taasisi nyingine wameelezea namna Mkoa wa Singida unavyotoa fursa adhimu kupitia madini mbalimbali kama dhahabu, gypsum, aluminium, chumvi na shaba. Pia wamependekeza kuanzishwa kwa majukwaa ya pamoja baina ya wadau wa sekta binafsi na umma ili kusikiliza changamoto na kutoa mapendekezo ya pamoja yatakayowezesha maendeleo ya haraka ya sekta ya biashara.

Kikao cha Baraza la Biashara Mkoa wa Singida pia kimehimiza kuangalia upya namna bora ya kuwawezesha wakulima kupitia vyama vya ushirika ili kuondokana na dhuluma za bei na kupatikana kwa malighafi ya kutosha kwa viwanda. Aidha, kikao hicho kimeazimia kuwepo kwa ushirikiano zaidi kati ya taasisi za serikali na sekta binafsi ili kuhakikisha Mkoa wa Singida unafikia azma ya kuwa kitovu cha viwanda vya kisasa nchini.



Tuesday, June 17, 2025

RC DENDEGO: “MKURUGENZI BANANA NA WANAOZALISHA HOJA MPYA – TUNATAKA KUWAWAJIBISHA KWA MATOKEO”.

 

Posted on: June 17th, 2025

Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mhe. Halima Dendego, akiwa mgeni rasmi katika mikutano maalum ya Baraza la Madiwani kwa Halmashauri za Wilaya ya Ikungi na Mkalama, ametoa maagizo ya moja kwa moja kwa Wakurugenzi na Watendaji wote kuhakikisha hoja zote za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) zinafungwa ifikapo Julai 15, 2025, huku akipiga marufuku kuzalisha hoja mpya kwa kisingizio chochote akionya kuwa hoja mpya ni dalili ya uzembe wa moja kwa moja na ni hatari kwa ufanisi wa Serikali.

RC Dendego amesisitiza kuwa hayuko tayari kuona hoja mpya zikizaliwa kwa sababu hiyo ni sawa na kuruhusu maradhi katika mfumo wa utendaji kazi wa Serikali. 

"Kwa hiyo Mkurugenzi, banana na yeyote anayezalisha hoja mpya. Tukiona hoja mpya, tunajua kuna mtu anakula bila kunawa. Huo ni uzembe, na uzembe ni kipindupindu kwenye ofisi yako,” amesema kwa lugha ya picha akiwataka viongozi wa halmashauri kuhakikisha uwajibikaji wa hali ya juu.

Kadhalika,ameelekeza kuwa kabla ya Uchaguzi Mkuu, kila uamuzi wa Baraza la Madiwani uliofikiwa kabla ya kuvunjwa kwa mabaraza utekelezwe kikamilifu akisisitiza kuwa utekelezaji wa maamuzi ya mabaraza ni sehemu ya heshima kwa madiwani waliomaliza muda wao, na ni msingi wa kuendeleza imani kwa wananchi.

Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida, Dkt. Fatuma Mganga, amesema kuwa ufuatiliaji wa hoja za ukaguzi lazima ufanyike kwa maandishi na kwa nyaraka zenye ushahidi wa hatua zilizochukuliwa. 

Ameongeza kuwa Halmashauri hazipaswi kutegemea vyanzo vya kawaida pekee katika mapato, bali ziendelee kubuni miradi ya kimkakati kama vile uwekezaji wa hewa ya ukaa na uanzishaji wa viwanda vidogo ili kuongeza mapato endelevu.

Aidha, Dkt. Mganga aliwakumbusha wakurugenzi na wataalamu kuwa uandaaji wa taarifa, matumizi sahihi ya mifumo ya kielektroniki na utunzaji wa kumbukumbu ni msingi wa uwajibikaji akihimiza  Halmashauri kubuni vyanzo vipya vya mapato ikiwemo uwekezaji wa hewa ya ukaa, ujenzi wa viwanda vidogo na kuimarisha usimamizi wa rasilimali ardhi na mazao ya kilimo.

Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali Mkoa wa Singida, Bw. Othman Mwinjuma Jumbe, ameeleza kuwa kwa Halmashauri ya Mkalama, hoja nyingi zimepatiwa ufumbuzi lakini bado kuna hitaji kubwa la kuimarisha elimu kwa watendaji kuhusu namna ya kuandaa nyaraka, kufunga hoja na kuepuka hoja mpya. Kadhalika ameunga mkono hatua zinazochukuliwa na kuahidi ushirikiano wa karibu na kila halmashauri katika kusafisha na kuimarisha mifumo ya udhibiti wa fedha.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Ikungi, Mhe. Thomas Apson, amebainisha kuwa Halmashauri yake imekusanya mapato kwa zaidi ya asilimia 140 ya lengo na wameweka mikakati ya kubaini mianya ya upotevu wa mapato, hususani kwenye sekta ya kilimo na biashara huku akiahidi kuongeza msukumo katika utekelezaji wa maelekezo ya RC kwa kushirikiana na wataalamu waliopo katika kila kata.

Kadhalika Mkuu wa Wilaya ya Mkalama, Mhe. Moses Machali, amesema kuwa nidhamu ya fedha, matumizi sahihi ya sheria na usimamizi wa hoja kwa wakati ndio silaha pekee ya kulinda maendeleo ya wananchi akisisitiza kuwa Serikali haitavumilia ulegevu wowote kutoka kwa watendaji wa ngazi yoyote ile.

Mwenyekiti wa Halmashauri ya Ikungi, Mh. Ally Juma Mwanga, alisema kuwa kati ya hoja 26 za ukaguzi, saba zimefungwa na 19 bado ziko kwenye mchakato wa utekelezaji. Alimhakikishia Mkuu wa Mkoa kuwa wataendelea kusimamia utekelezaji wa maamuzi na hoja kwa karibu na kwa kasi inayotakiwa ili kufanikisha maelekezo ya Serikali.

Kadhalika,Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mkalama  Mhe. James Mkwega alitoa pongezi kwa uongozi wa Mkoa kwa usimamizi madhubuti wa miradi ya maendeleo na kupendekeza kuwa uwanja wa Bombadia ubatizwe jina la Dendego, akisema Mkuu huyo wa Mkoa amekuwa mfano wa kiongozi anayetenda kwa vitendo katika kuhamasisha utekelezaji wa miradi.

Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Ikungi, Bw. Kastory Msigala, amesema kuwa hoja zote zipo katika hatua nzuri za utekelezaji, na akatoa wito kwa Wakuu wa Idara kuhakikisha hawasubiri kukumbushwa bali wachukue hatua kwa wakati. Kadhalika ameahidi kuwa ofisi yake itafikia lengo la kufunga hoja zote ndani ya muda uliowekwa.

Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Mkalama, Bi. Asia Messos, alisema kuwa Halmashauri hiyo imeendelea kupokea hati safi kwa miaka minne mfululizo na sasa inahakikisha hoja zote zilizopo zimefungwa kupitia njia za maridhiano, ushauri wa kitaalamu na ufuatiliaji wa karibu.

Mikutano hiyo maalum ya baraza la madiwani imefanyika ikiwa ni sehemu ya hatua za mwisho kabla ya kuvunjwa kwa mabaraza yote nchini kwa ajili ya maandalizi ya uchaguzi mkuu wa serikali za mitaa. Mkoa wa Singida umeonesha dhamira ya kweli ya kuhakikisha kila hoja ya ukaguzi inashughulikiwa kwa matokeo, si kwa maneno pekee bali kwa ajili ya wananchi.

Kwa ujumla Mikutano hiyo maalum ya mabaraza maalum imefanyika kwa mafanikio makubwa kabla ya kuvunjwa kwa mabaraza ya madiwani nchini kote, ikiwa ni agizo kutoka Ofisi ya Rais – TAMISEMI. Mkoa wa Singida, chini ya uongozi wa Mkuu wa Mkoa Mhe. Halima Dendego, umeonesha msimamo thabiti wa kuhakikisha hoja za ukaguzi hazibaki kama historia, bali zinapatiwa majibu na hatua, huku fedha za umma zikisimamiwa kwa tija na ufanisi kwa maendeleo ya wananchi.