Thursday, August 29, 2024

*RC SINGIDA ATOA WITO KWA VIONGOZI KUSIMAMIA VYANZO VYA MAPATO NA KUFUATA TARATIBU ZOTE*

Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mhe. Halima Dendego, amewataka viongozi wa mkoa huo kusimamia kikamilifu vyanzo vyote vya mapato na kuhakikisha taratibu zote zinafuatwa kwa usahihi.

 Akizungumza (Agosti 29, 2024) ikiwa ni siku ya pili katika kikao kazi na watendaji wa Serikali pamoja na Sekta binafsi, Dendego amesisitiza umuhimu wa kuwa na nidhamu ya mapato na uwajibikaji katika ukusanyaji na matumizi ya rasilimali za umma.

 Amesema viongozi wanapaswa kuhakikisha vyanzo vya mapato vinatambuliwa, kusimamiwa, na kudhibitiwa ili kuzuia mianya ya upotevu wa fedha za umma. Ameongeza kuwa ukusanyaji wa mapato lazima uendane na sheria taratibu na kanuni zilizopo ili kuimarisha uwazi na uwajibikaji katika matumizi ya fedha.

 “Kila kiongozi anawajibika kuhakikisha mapato yanakusanywa ipasavyo na hakuna upotevu wa aina yoyote. Ni jukumu letu kuhakikisha tunasimamia rasilimali hizi kwa uadilifu na kufuata taratibu zote za kisheria,” alisema RC Dendego.

Aidha, ameonya dhidi ya vitendo vya rushwa na matumizi mabaya ya ofisi, akisema ni jukumu la viongozi wote kuwa mfano bora kwa kufuata sheria na taratibu katika utendaji kazi. Amesisitiza kuwa uwazi na uwajibikaji ni msingi wa mafanikio ya mkoa na kwamba hakuna kiongozi anayepaswa kukiuka taratibu za ukusanyaji na matumizi ya mapato.

 Dendego pia amewataka viongozi kuwa wabunifu na kutafuta vyanzo vipya vya mapato ili kuongeza mapato ya mkoa na taifa kwa ujumla, akisisitiza kuwa usimamizi mzuri wa vyanzo vya mapato utasaidia katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo inayolenga kuboresha maisha ya wananchi wa Singida.

 Amemalizia kwa kuwataka viongozi wote kuhakikisha wanatekeleza wajibu wao kwa uadilifu na kuhakikisha mapato yote yanakusanywa na kupelekwa benki kwa wakati huku akisisitiza umuhimu wa kufuata taratibu zote zilizopo bila kuzipindisha.

Viongozi wa serikali na sekta binafsi wakiendelea na mafunzo.

No comments:

Post a Comment