Saturday, April 27, 2024
Friday, April 26, 2024
WANANCHI WA SINGIDA WAMPONGEZA RAIS SAMIA KWA KUWALETEA MAENDELEO MAKUBWA.
Mkuu wa mkoa wa Singida Mhe. Halima Dendego, akizungumza
kwenye maadhimisho ya miaka 60 ya Muungano wa Tanzania ambayo kimkoa
yamefanyika mjini Kiomboi wilayani Iramba amesema pamoja na Serikali Kuu kutoa
fedha nyingi kwa ajili ya miradi ya maendeleo lakini bado kuna umuhimu mkubwa
kwa wananchi kushirikiana na Serikali katika kujitolea nguvu kazi ili kuongeza
kasi katika ukamilishaji wa miradi hiyo.
Dendego, amesema maendeleo ya kweli hayawezi kuja kama watu
hawatashirikiana katika kufanya kazi hivyo ni muhimu kwa makundi yote
kushirikiana kwa kiwango cha juu ili kuharakisha maendeleo yao na ya Taifa kwa
ujumla.
Aidha, amewahakikishia wananchi wa mkoa huo kuwa yeye ni muumini
mzuri kwa watu wanaochapa kazi kwa bidii hivyo ni lazima wananchi wote kuchapa
kazi ili kujiletea maendeleo yao na ya Taifa kwa ujumla.
Katika maadhimisho hayo ya miaka 60 ya Muungano, Mkuu huyo wa mkoa ametoa zawadi mbalimbali kwa wanafunzi waliofanya vizuri katika uandishi wa isha pamoja na vikundi mbalimbali vya burudani zilizotumbuiza hususan kwa wimbo maalum wa Muungano.
RC DENDEGO AKONGA NYOYO ZA WANASINGIDA KWENYE MAADHIMISHO YA MIAKA 60 YA...
Wednesday, April 24, 2024
RC DENDEGO: SEKTA YA BIASHARA NA VIWANDA NI MUHIMU KWA UCHUMI WA MKOA WA SINGIDA
Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mheshimiwa Halima Dendego, amekutana na Uongozi wa Chama cha Wafanyabiashara, Wakulima na wenye Viwanda Tanzania (TCCIA) wa mkoani humo, leo Aprili 24, 2024 ofisini kwake, na kufanya nao mazungumzo yanayohusiana na sekta ya biashara ili kukuza na kuinua uchumi wa mkoa na Taifa kwa ujumla.
Kupitia kikao hicho, ujumbe wa TCCIA Mkoa wa Singida uliyoongozwa na Mwenyekiti wake Bw. Elly Kitila Mkumbo, ukiwa na lengo kwa Jumuiya hiyo ya Wafanyabiashara kujitambulisha mbele ya Mkuu huyo wa Mkoa aliyehamia Singida kutokea Mkoani Iringa hivi karibuni.
Aidha, katika kikao hicho walipata wasaa wa kujadili fursa mbalimbali kupitia Sekta ya biashara, uchumi, uzalishaji pamoja na uwekezaji zilizopo mkoani Singida hususani kwenye viwanda, kilimo, biashara, uvuvi, mifugo, madini, pamoja na miundombinu ya barabara na nishati ili ziweze kuinua na kuboresha maisha wananchi wa mkoa huo na Taifa kwa ujumla.
RC Dendego, ameuhakimishia uongozi wa Jumuiya ya Wafanyabishara hao kuwa ataimarisha ushirikiano zaidi baina ya pande zote mbili ili kukuzu uchumi wa wanasingida kupitia sekta binafsi kwakuwa Serikali ya Mkoa ipo imara katika Ulinzi na Usalama.
“Kwa kweli Jumuiya yenu ya Chamber of Commerce, ni muhimu na ni muhimili mkubwa katika uchumi, niwaombe sana tuendeleze ushirikiano huu kwa ajili ya maendeleo ya wananchi wetu ambao Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan amedhamiria kuboresha maisha ya mtu mmoja mmoja ndio maana miradi mbalimbali inatekelezwa.’ amesema Dendego.
Katika mazungumzo hayo, msafara wa Jumuiya ya Chamber of Commerce, kupitia Mwenyekiti Kitila, alimweleza Dendego umuhimu wa Serikali kuboresha soko la kimataifa la vitunguu lililopo Kata ya Misuna katika Manispaa ya Singida kutokana na umuhimu wake katika kuhudumia wakulima na wafanyabishara wa ndani na nje ya Tanzania.
Kitila amemhakikishia Mkuu huyo wa mkoa kuwa, Chamber of Commerce itaendeleza na kudumisha ushirikiano baina ya Jumuiya ya TCCIA na Serikali kwa nia thabiti ya kumkomboa na kuhakikishia mfanyabiashara shughuli zake zinatekelezeka kwa maslahi ya Taifa pamoja na kulitangaza soko la kimataifa la vitunguu lililopo mkoani Singida.
Kuhusu sekta ya Mawasiliano, mmoja wa wajumbe wa Chamber of Commerce, James Japheth (Buhanzo), ambaye pia ni Mkurugenzi Mtendaji wa Redio Standard iliyopo Singida Mjini ameahidi kuongeza wigo wa usikivu wa Redio hiyo aliyowekeza mkoani humo ili masafa yake yaweze kupatikana kwa urahisi ndani na nje ya mkoa wa Singida.
Buhanzo alilazimika kusema hayo, baada ya Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mhe. Halima Dendego, kumtaka atumie fursa ya uwekezaji wa kituo chake cha Redio kuongeza usikivu wa matangazo ili Wananchi wa mkoani humo waweze kupata habari mbalimbali za maendeleo zinazotekelezwa na Serikali pamoja na sekta binafsi.
Tuesday, April 23, 2024
KUELEKEA MAADHIMISHO YA MIAKA 60 YA MUUNGANO, RC SINGIDA AHIMIZA AMANI NA UTULIVU
Mkuu wa mkoa wa Singida Halima Dendego ameonya kuwa atawachukulia hatua kali watu au kikundi cha watu wanaotaka kuvuruga au kuvunja amani na utulivu kwa wananchi wa mkoa wa Singida.
Dendego, ametoa kauli hiyo (leo 23/Aprili/24 ) mjini Singida, katika uzinduzi wa wiki ya maadhimisho ya miaka 60 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar kwa kufanya usafi katika maeneo mbalimbali ya Soko Kuu la Singida.
Mkuu huyo wa mkoa wa Singida amewasisitiza wananchi wa mkoa wa Singida kuwakataa watu au mtu yeyote anayetaka kumdhalilisha Rais au Watanzania kwani wakiwaruhusu kufanya hivyo watakuwa wamedhalilisha Taifa na Watanzania wote hivyo ni lazima wananchi wote waungane kukataa watu hao wenye nia mbaya na Taifa la Tanzania.
Mkuu wa Mkoa wa Singida Mheshimiwa Halima Dendego, (wapili kushoto) akifanya usafi wa mazingira na wananchi katika soko kuu la Singida.
“Tuungane wote katika kupambana na yeyote anayetaka kuleta ujinga ujinga katika Taifa letu tuwabaini ili tuwawajibishe “ Amesisitiza Halima Dendego.
RC Dendego, amesema yeye ni rafiki wa wote Vijana, Wazee, Wanaume na Wanawake hivyo Ofisi yake ipo wazi muda wote kwa anayetaka kusaidiwa kwa shida yeyote aende ili asaidiwe nia ni kuona wananchi Singida wanaishi maisha mazuri na yenye staha bila kero.
Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Singida, Mhe. Godwin Gondwe amemhakikishia Mkuu wa mkoa huo kuwa atasimamia maelekezo yake yote aliyotoa hasa ya kuhakikisha Manispaa ya Singida inakuwa safi katika maeneo yote ya Masoko na maeneo yenye watu wengi kama hatua ya kudhibiti magonjwa ya maambukizi ikiwemo kipindupindu.
Gondwe amesema kuwa hivi karibuni watazindua kampeni kubwa ya usafi katika Manispaa ya Singida ambayo itasaidia kuboresha usafi katika maeneo yote ya mji wa Singida ikilinganishwa na hali ilivyo sasa.
Naye, Kaimu Mkurugenzi wa Manispaa ya Singida, Edward Mboya amebainisha kuwa kupitia mapato ya ndani wanaendelea na mchakato wa kununua gari nyingine mpya ya kubebea taka na vifaa vya kuhifadhi taka lengo likiwa ni kuifanya Manispaa ya Singida kuwa bora nchini hasa katika masuala ya Usafi.
Mkuu wa Wilaya ya Singida Godwin Gondwe, akifanya usafi wa mazingira na wananchi katika soko kuu la Singida.
Wananchi wa Singida Mjini wakifanya usafi wa mazingira ikiwa ni sehemu ya kuelekea maadhimisho ya miaka 60 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar.
Monday, April 22, 2024
MKOA WA SINGIDA WAANZA KUTOA CHANJO YA SARATANI YA MLANGO WA KIZAZI KWA WASICHANA 178,114.
Akizindua zoezi la utoaji wa Chanjo hiyo katika Kijiji cha Kisaki
Manispaa ya Singida, Mkuu wa mkoa wa Singida Mheshimiwa Halima Dendego (leo 22-Aprili-2024 ) amewaagiza
Maafisa Afya wahakikishe maeneo yote yaliyoandaliwa kutolewa huduma hiyo ya
chanjo yanafanya hivyo kwa viwango vya juu ili kuwalinda watoto wa kike na
saratani hiyo hatari.
Dendego amesisitiza kuwa chanjo hiyo pia ni lazima iwafikie
wanafunzi wanaosoma kwenye shule binafsi na watoto wa kike ambao wanaishi mitaani
nao wapate fursa ya kupata chanjo hiyo ili kuwakinga na saratari na mlango wa kizazi.
“Tunapoenda
kuwalinda watoto wa kike kwa kuwachanja chanjo hiyo maana yake tunawaepusha na
madhara ugonjwa wa saratani ili wasije wakaambukiza wavulana”Ameeleza RC. Halima
Dendego.
Amesisitiza kuwa chanjo hiyo ni muhimu kwa wasichana na inatolewa
bure kwa sababu Serikali kwa kushirikiana na Wadau wa maendeleo imegharamia
chanjo hiyo, hivyo ni muhimu kwa wazazi na walezi kuwapeleka watoto wao kupata
chanjo hiyo ili kuwaepusha na madhara yanayoweza kutokea.
Kwaupande wake, Mganga Mkuu mkoa wa Singida Dkt. Victorina
Ludovick amesema kwa Tanzania chanjo ya saratani ya mlango wa kizazi (HPV)
ilianza majaribio mwaka 2014 mkoani Kilimanjaro na kupata mafanikio makubwa kwa
kuwakinga wasichana wasipate ugonjwa huo.
Dkt. Victorina Ludovick ameeleza mtu yeyote anaweza kuambukizwa
saratani hiyo katika umri wowote ule hasa wakati wa tendo la ndoa na inaweza
kusababisha magonjwa mengine ikiwemo saratani ya koo na magonjwa mengine ya via
vya kizazi kwa wanamke na wanaume.
Naye, Katibu Tawala wa mkoa wa Singida Dkt. Fatuma Mganga
amewataka Maafisa Afya wanaotoa chanjo hiyo kuhakikisha wanafanikisha zoezi
hilo kwa viwango ili mkoa wa Singida uwe wa kwanza katika utoaji wa chanjo hiyo
kwa wasichana mwenye umri wa miaka Tisa hadi 14.
Amesema saratani hiyo inaua na ni ugonjwa hatari hivyo ni muhimu
kwa watoto wote wenye umri wa kupata chanjo wapewe kutokana na umuhimu wake
katika kulinda afya zao.
Nao, Mashuhuda waliopewa chanjo hiyo wakizungumza kwenye uzinduzi
wa utoaji wa chanjo ya satarani la mlango wa kizazi katika kijiji cha Kisaki
Manispaa ya Singida Lukuresia Andrea na Salisabila Athumani wote wakazi wa mkoa
wa Singida wamesema tangu wapatiwe chanjo hiyo hawajapata madhara yoyote hivyo
wameomba wazazi na walezi wasiwazuie watoto wao wa kike kwenda kupata chanjo
hiyo kwa sababu inafaida kubwa katika maisha yao.
Zoezi la kuimarisha chanjo ya HPV litakamilika tarehe 26 Aprili,
2024 hata hivyo hudumaa hiyo itaendelea kutolewa kwa utaratibu wa zamani yaani
shuleni, vituo vya kutolea huduma za afya na kwenye huduma za mkoba za Masuala
ya Afya ya Uzazi na Mtoto.
Chanjo ya HPV, kama ilivyo kwa chanjo nyingine zinazotolewa
kupitia Mpango wa Taifa wa Chanjo, haiuzwi kwa mteja yeyote, hivyo inatolewa
bure kwa walengwa katika vituo vyetu vya kutolea huduma.
Baadhi ya Wanawake waliopata chanjo ya saratani ya mlango wa kizazi mkoani Singida wakiwa na watoto wao.