Thursday, August 15, 2024

RC SINGIDA AAGIZA KUKAMILISHWA KWA MIRADI YOTE YA MAENDELEO HADI KUFIKIA MWISHONI MWA MWEZI HUU.

Mkuu wa Mkoa wa Singida Halima Dendego amewaagiza Watendaji katika Halmashauri Saba za mkoa huo kuhakikisha wanakamilisha utekelezaji wa miradi yote ya maendeleo hadi kufikia mwisho mwa mwezi huu.

Mkuu huyo wa mkoa wa Singida ametoa agizo hilo (14 Agosti, 2024) katika majumuisho ya ziara yake ya kukagua miradi mbalimbali ya Maendeleo katika Manispaa ya Singida.

Dendego amesisitiza kuwa miradi yote iliyoanza kutekelezwa katika kipindi cha miaka Mitatu nyuma lazima ikamilike ili wananchi waanze kupata huduma mbalimbali za kijamii kwa muda muafaka.

“Lengo la miradi hii sio kuona majengo bali ni kutoa huduma inayotakiwa lazima majengo yakamilike kwa wakati na kwenye matatizo Viongozi wakae na kutatua changamoto hiyo ili miradi isikwame, Ameeleza Dendego.

Ameeleza kuwa maeneo yote ya miradi ambayo yana migogoro lazima Viongozi wakae wahusika ili kuondoa changamoto hizo kwa wakati nia ikiwa ni kuona wananchi wanaanza kupata huduma bora na za msingi karibu na maeneo yao.

Dendego pia amepongeza hatua zinachukuliwa na Watendaji katika kusimamia na kutekeleza miradi hiyo ya maendeleo ili iweze kutekelezwa kwa viwango na ubora unaotakiwa.

Kwa upande wake, Katibu Tawala wa mkoa wa Singida Dkt. Fatuma Mganga amemhakikishia Mkuu wa mkoa wa Singida kuwa atahakikisha miradi yote inayotekelezwa mkoani humo inakamilika kwa wakati na kwa kuzingatia thamani ya fedha iliyotolewa.

Dkt. Mganga amewasisitiza Watendaji wote washiriki kikamilifu katika kusimamia miradi iliyopo kwenye maeneo yao ili wananchi waweze kufurahia huduma bora zinazotolewa na Serikali yao.

Naye, Mkuu wa Wilaya ya Singida Godwin Gondwe, ameeleza kuwa atafanya kazi kwa usiku na mchana kwa ushirikiano na Watendaji wengine ili kuhakikisha miradi yote ya Maendeleo inayotekelezwa kwenye Wilaya yake inakamilika hadi mwisho wa mwezi huu kama maelekezo ya Serikali yanayotaka.





No comments:

Post a Comment