Tuesday, November 16, 2021

Mabadiliko Makubwa Yaja Mkoa wa Singida – Katibu Tawala

 
Wakazi wa Mkoa wa Singida wametakiwa kuendelea kufanya kazi kwa bidii na kutokuwa wanyonge kwakuwa wamebarikiwa kuwa na  Mkoa wenye mafanikio makubwa  katika uzalishaji na uinuaji vipato.

Serikali ya Mkoa ina mkakati wa kufanya mabadiliko makubwa ya kiuchumi na kimazingira kwa kupitia uzalishaji katika kilimo ili kuendelea kuwanufaisha wananchi wa Singida.

Akiongea wakati wa kutoa shukurani baada ya kukamilika kwa kikao kazi kilichofanyika leo katika ukumbi wa mikutano wa Social holl Mjini Singida, Katibu Tawala wa Mkoa huo Dorothy Mwaluko, amesema wamejipanga kuondoa uhaba wa mafuta nchini kwa kutekeleza mkakati wa kuongeza uzalishaji wa alizeti na matumizi ya pembejeo bora za kilimo kwa wakulima.

Dorothy amewakumbusha wananchi wa Mkoa huo kuongeza bidii katika kufanya kazi hasa katika kipindi hiki cha msimu wa kilimo ambapo mazao kama alizeti korosho mkonge na degu vimeendelea kuwa na soko ndani na nje ya mkoa wa Singida.


Akiongea kwa niaba ya Makatibu Tawala wa Mikoa ya Dodoma, Simiyu na Manyara, Dorothy amemuahidi Waziri wa Kilimo Prof. Adolf Mkenda kwamba mikoa hiyo imejipanga kutekeleza  kikamilifu mkakati wa kuondoa tatizo la uhaba wa mafuta nchini kwa  kipindi kifupi kijacho.


Aidha Katibu Tawala huyo ameishukuru  Wizara ya Kilimo kwa maamuzi yake ya kuzindulia ugawaji wa mbegu mkoania Singida kupitia mradi unaofadhiliwa na Mfuko wa Maendeleo ya Kilimo IFAD  katika mkoa wa Singida ambapo utakuwa umeongeza chachu kwa wakulima wa alizeti.


Dorothy amebainisha kwamba mkoa  umepokea tani  252 za  mbegu za alizeti kutoka Taasisi ya uzalishaji wa mbegu za kilimo (ASA) kupitia Wizara ya Kilimo.


Aidha Katibu Tawala huyo akakamilisha salamu zake kwa kuwataka wawekezaji kuwekeza katika mkoa wa Singida ambao unastawisha vizuri mazao kama mkonge korosho alizeti dengu karanga na mtama.


No comments:

Post a Comment