Tuesday, November 30, 2021

Hospitali ya Mandewa yakabidhiwa basi la kusafirishia wafanyakazi.

 

Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt. Binilith Mahenge Leo Novemba 30, 2021 amezindua Rasmi  na kukabidhi basi aina ya Coasta kwa ajili ya kusafirishia wafanyakazi wa Hospitali ya Mandewa iliyopo mkoani hapo kama kitendea kazi kitakachowasaidia kuongeza ufanisi katika utendaji kazi.

Akongea na wafanyakazi akiwa Hospitalini hapo baada ya kuwakabidhi basi Mkuu wa Mkoa amewapongeza watumishi kwa namna ambavyo wamekuwa wakifanya kazi katika mazingira magumu  na wengi wao wakitumia bodaboda kufika kazini lakini pia hawakukata tamaa.

RC Mahenge amemtaka Afisa usafirishaji wa Hospitali ya mkoa wa Singida kuhakikisha kwamba basi hilo linatunzwa na kuzingatia muda wa  kufanyia huduma (service) kila inapofika muda wake ili kulifanya lidumu kwa muda mrefu na kuendelea kuwasaidia watumishi.

Amewataka madaktari katika hospitahi hiyo ambayo ni Tawi la Hospitali ya Mkoa wa Singida  kuboresha huduma zao na kuzifanya ziwe za kibingwa  ili kuifanya Singida kuwa kimbilio la  mikoa ya jirani (center of excellence )

Aidha ameitaka bodi ya Hospitali hiyo kuanza kufikiria namna ya kujenga nyumba za watumishi kupitia vyanzo vyao vya ndani au kupitia  mashirika mbalimbali  kwa kuwa kukaa karibu na hospitali kunaongeza ufanisi katika kazi.

Akimalizia hotuba yake mkuu wa mkoa amewataka madaktari hao pamoja na bodi kuyafanya majengo ya zamani kuwa hospitali ya Wilaya halafu majengo ya Hospitali ya Mandewa yatumike kama hospitali ya mkoa.

Awali Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya mkoa  Dkt. Deogratius Banuba akisoma hotuba yake amesema gari hilo lina thamani ya zaidi ya Sh. Milioni 236 ambazo zilitokana na makusanyo ya ndani.

Hata hivyo amemhakikishi RC kwamba gari hilo litatumika kubeba watumishi kuwaleta kazini na kuwarudisha na pia kutumika katika shughuli za kijamii kwa watumishi hasa zile ambazo  zipo ki sharia kama  Msiba.

MATUKIO MBALIMBALI KATIKA PICHA WAKATI WA HAFLA FUPI YA UZINDUZI WA BASI 


Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt. Binilith Mahenge (kulia) akiwa ndani ya basi hilo muda mfupi baada ya uzinduzi. Kushoto ni Mkuu wa Wilaya ya Singida Mjini Mhandisi Paskas Muragili akimshukuru Mkuu wa mkoa kwa uzinduzi rasmi wa basi hilo.

Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt. Binilith Mahenge akisisitiza jambo wakati wa hafla fupi ya uzinduzi wa basi iliyofanyika katika viwanja vya Hospitali ya Rufaa mkoani Singida.


Sherehe ya Uzinduzi ukiendelea


Muonekano wa basi hilo la Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Singida

No comments:

Post a Comment