Tuesday, July 20, 2021

MWENGE WA UHURU 2021 WAPOKELEWA MKOANI SINGIDA, MIRADI 55 KUZINDULIWA

 

Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt. Binilith Mahenge akiwa ameushika Mwenge wa Uhuru 2021 

Miradi mbalimbali ya maendeleo yenye thamani ya shilingi bilioni 8.1 itakaguliwa na kuzinduliwa wakati wa Mbio za Mwenge wa Uhuru zilizoanza leo  Julai 20, 2021 Mkoani Singida.

Akiongea leo wakati wa mapokezi ya Mwenge wa Uhuru Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt. Binilith Mahenge amesema kiasi hicho cha fedha kimetumika katika miradi 55 ya maendeleo katika Mkoa mzima.

Jumla ya miradi 55 inayohusu TEHAMA, Elimu Afya, mazingira maji biashara, barabara programu za rushwa, VVVU/UKIMWI, malaria na mapambano dhidi ya dawa za kulevya itatembelewa” amesema Mhe. Mahenge.

Amesema katika mbio hizo za Mwenge wa Uhuru miradi mipya 9 itazinduliwa, miradi  miwili itafanyiwa ufunguzi, sita itawekwa jiwe la msingi na 36 itakaguliwa na miradi miwili itatembelewa.

Aidha Mhe. Mkuu wa mkoa amebainisha kwamba kiasi hicho cha fedha kwenye miradi hiyo inatokana na michango ya wananchi kiasi cha sh.Bilioni 1.9, mchango wa Halmashauri kiasi cha sh.milioni 69.6 na kiasi cha sh. milioni 4.6 kutoka Serikali kuu.

Hata hivyo Mhe. Dkt. Mahenge ametoa wito kwa wanasingida wote kutumia kaulimbiu ya Mwenge wa Uhuru 2021 “TEHAMA ni msingi wa Taifa endelevu” kwa kuwajibika ili kuleta maendeleo ya mtu na Taifa kwa ujumla.

Amesema kutokana na umuhimu wa TEHAMA katika maendeleo ya Taifa mkoa umeendelea kusimamia zaidi ya mifumo 30 inayotumika katika mamlaka za Serikali za mitaa, Sekretarieti ya mkoa pamoja na  taasisi mbalimbali zilizopo ndani ya mkoa.

Hata hivyo Mkuu wa Mkoa amewataka wananchi wa Singida kujiunga na bima ya afya ili kukabiliana na gharama za matibabu.

Amewasihi wananchi kutumia lishe bora kwa afya imara ambapo kiwango cha udumavu kimeendelea kupungua hadi kufikia asilimia 29 mwaka 2018.

Mkoa umeendelea kutafuta suluhisho la tatizo la    ukondefu na upungufu wa uzito kwa watoto kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa lishe ambapo jumla ya vituo 99 vya huduma ya afya  vinavyotoa matibabu kwa watoto vimeanzishwa. Alibainisha  mkuu wa mkoa 

Matukio mbalimbali katika picha



















Mwenge wa Uhuru 2021, katika Mkoa wa Singida utakimbizwa kwa muda wa siku Tano (5), katika Wilaya Tano kwa kuanzia na Wilaya ya Iramba leo tarehe 20/07/2021 na utahitimisha mbio zake mnamo tarehe 24/07/2021 na tarehe 25/07/2021 utakabidhiwa Mkoa wa Dodoma.

MWENGE WA UHURU 2021 WAPOKELEWA MKOANI SINGIDA, MIRADI 55 KUZINDULIWA


No comments:

Post a Comment