Thursday, April 18, 2019

SIKU KUU YA PASAKA


WAUMINI wa madhehebu ya Dini mbalimbali na wasio waumini mkoani Singida wamehimizwa kuitumia siku kuu ya Pasaka kumaliza tofauti zilizopo kwenye ndoa, familia zao ili amani na utulivu iendelee kudumu kuanzia ngazi ya familia, mkoa na taifa kwa ujumla.

Wito huo umetolewa na mwenyekiti wa  umoja wa madhehebu ya dini manispaa ya Singida, Sheikh Hamisi Kisuke, wakati akizungumza kwenye hafla ya kuwatakia kheri waumini wa dhehebu ya dini ya  Kikristo, waumini wengine na wale wasiokuwa na dini.

Akifafanua amesema, amani na utulivu ndio mambo pekee ambayo yanatoa fursa kwa  binadamu kujiletea maendeleo endelevu, kwa uhuru mkubwa.

Aidha, amewataka waumini hao kutumia siku kuu ya Pasaka kuimarisha upendo bila kujali itikadi ya dini yoyote kwa madai  Mungu kwenye amri zake, ameagiza binadamu kupendana.

“Kwa kifupi katika umoja wetu wa madhehebu ya dini, tunapenda kuona mume na mke wa dini yoyote kama kuna sitofahamu yoyote waitatue kipindi hiki cha Pasaka. Pasaka ikimalizika waanze maisha mapya na mema” amesema Sheikh Kisuke ambaye pia ni diwani kata ya Misuna.

Pia Sheikh Kisuke, ametumia nafasi hiyo kumpongeza na kumshukru mkuu wa mkoa wa Singida, Dkt. Rehema Nchimbi, kwa juhudi zake za kusimamia vema maendeleo ya mkoa wa Singida kwa ufanisi.

“Mkuu wetu wa mkoa Dkt. Rehema Nchimbi ni muasisi wa umoja wetu wa madhehebu ya dini mbalimbali katika mkoa huu. Umoja huu umesaidia kwa kiasi kikubwa waumini wa madhehebu ya dini kuheshimiana, kuaminiana  na kushikamana kama ndugu. Nampongeza sana Dkt. Nchimbi kwa hili” amesema mwenyekiti huyo.

Kwa upande wake Askofu msataafu Kanisa la Pentekoste (FPCT) la mjini kati, Dkt. Paulo Samwel, amesema, Umoja huo sio wa kisiasa. Umoja huo ni wa kweli na unatekeleza yote yale yanayompendeza Mungu na raia wote wema.

“Ndugu zangu, mvua msimu huu haijakidhi mahitaji, nawaomba waumini wa madhehebu ya dini mbalimbali na wasio na dini waondoe hofu ya aina yoyote. Mungu wetu hatatutupa kamwe, ataleta neema zake kwa namna nyingine” amesema Dkt. Paulo.

Wakati huo huo, Jaji mstaafu, Fatuma Masengi, amesema, wakazi wa mkoa wa Singida wawe na amani kipindi hiki cha Pasaka kwa kuwa Mungu ataendelea kuwalinda wao na viongozi wao.

No comments:

Post a Comment