Mkuu wa Mkoa wa
Singida Dkt Rehema Nchimbi akizungumza na madiwani na watendaji katika baraza
maalumu la madiwani wa halmashauri ya Wilaya ya Manyoni la kujadili hoja za
Mkaguzi na Mdhibiti wa Hesabu za Serikali.
Watendaji wa
halmashauri ya Wilaya ya Manyoni wakifuatilia kwa umakini hoja zikijadiliwa
katika baraza maalumu la madiwani la kujadili hoja za Mkaguzi na Mdhibiti wa
Hesabu za Serikali.
Mkuu wa Mkoa wa
Singida Dkt Rehema Nchimbi ameagiza na kutoa mwezi mmoja mali za watendaji 21
wa vijiji katika halmashauri ya Wilaya ya Manyoni zitaifishwe na kuuzwa ili
kufidia fedha walizotumia za chakula cha njaa katika kipindi cha mwaka 2012.
Dkt Nchimbi ametoa
agizo hilo katika baraza maalumu la madiwani la kujadili hoja za mkaguzi na
mdhibiti wa hesabu za serikali ambapo kulikuwa na hoja ya watendaji wa vijiji
30 waliokusanya kwa wananchi shilingi milioni 15,268,700 kwa ajili ya chakula
cha njaa na hawakuziwasilisha katika halmashauri hiyo.
Amesema kitendo hicho
ni wizi na hakistahili kuvumiliwa licha ya watendaji tisa kurejesha kiasi cha shilingi
milioni 3,277,000 na hivyo kusalia watendaji 21 wanaodaiwa shilingi milioni 11,991,700
walizokusanya.
“Huu ni wizi na
hatutauvumilia, hao watendaji wa vijiji hakikisheni wanarudisha fedha za
serikali, Mkuu wa Wilaya na Mkurugenzi, anzisheni utaratibu wa mahakama tembezi
muwafuate huko waliko, kamateni mbuzi, kuku, uzeni tupate hiyo fedha na zoezi
hilo lifanyike ndani ya mwezi wa nane” ameagiza Dkt Nchimbi.
Ameongeza kwa kusema
kuwa, “watendaji hawa nasikia wengine wameshaandikiwa barua za onyo zaidi ya
mara tatu, kwanini wanaendelea kuwa watumishi wa umma?, kwanini wasikae pembeni
tupate watanzania wengine wazalendo wazibe nafasi hizo?. Hawa hawafai kuwa
watumishi wa umma, ila hakikisheni kwanza fedha inarudi ndipo hatu nyingine
zichukuliwe”.
Dkt. Nchimbi amesema
hoja nyingi katika halmashauri hiyo zimetokana na uzembe wa watumishi pamoja na
kutegemea taarifa za makaratasi badala ya kutembelea maeneo husika kujionea
hali halisi ya utekelezaji wa shughuli mbalimbali za serikali mpaka ngazi ya
vijiji na mitaa.
Aidha amemtaka
mwanasheria wa halmashauri na mkaguzi wa ndani kuisaidia halmashauri kuepuka
kuwa na hoja nyingi zinazoepukika kwa kutoa ushauri sahihi na kwa wakati, huku
akiwasisitiza watumishi wote kubadilika, kuacha uzemba na kufanya kazi kwa
mazoea bali waendane na kasi ya serikali ya awamu ya tano.
Kwa upande wake Mkaguzi
wa Nje wa Hesabu za Serikali Anna Kakunguru amewataka viongozi kuhakikisha
wanasimamia ili hoja zifungwe kabla ya watendaji waliosababisha hoja hizo
kustaafu, kuhama au kuachishwa kazi ili kuepuka hasara.
Kakunguru amesema
imekuwa ikichukua muda mrefu kwa halmashauri kufuta hoja jambo linalosababisha
waliotengeneza hoja hizo kutopatikana na kuzijibu ili halmashauri isibaki na
hoja nyingi.
Ameongeza kuwa uwepo
wa hoja za serikali ni kiashiria kuwa kuna sehemu katika utendaji wa halmshauri
kuna mapungufu au umelegalega na hivyo halmashauri inapaswa kushirikiana na
Mkaguzi wa nje na ndani ili kurekebisha na kuzuia kabisa udhaifu huo.
Naye Kaimu Mkuu wa
Wilaya ya Manyoni Miraji Mtaturu amesema atahakikishika kufikia tarehe 30
Agosti watendaji 21 watakuwa wamerejesha fedha walizochukua za wananchi huku
akiagiza apatiwe orodha ya watendaji hao ili aweze kuwashughulikia vizuri.
Mtaturu ameongeza
kuwa atasimamia kikamilifu ili mahakama tembezi itakayoanzishwa iweze
kutekeleza agizo hilo na kurejesha fedha hizo na endapo watatokea watendaji
watakaokaidi kutoa ushirikiano atawachukulia hatua zaidi za kisheria.
Ameongeza kwa kumtaka
Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manyoni kuweka utaratibu wa kukutana na watendaji
wake mara mbili kwa mwezi ili wajadili namna ya kufuta hoja zilizojitokeza
pamoja na kupeana maelekezo ya namna ya kuepuka kutengeneza hoja nyingine.
Wakati huo huo Mkuu
wa Mkoa wa Singda Dkt Rehema Nchimbi amewashauri madiwani wa halmashauri hiyo
kutenga ekari tano kwa ajili ya kilimo cha korosho katika kata zao ili kuongeza
kipato kwa wananchi wao, kutunza mazingira na kufikia lengo la kuwa wazalishaji
wakubwa wa korosho nchini.
Dkt Nchimbi pia
ameshauri madiwani hao na watendaji kutofanya mzaha na waliovamia misitu ya
hifadhi kwakuwa wanahatarisha usalama wa raia kutokana na wanyama kutoka katika
hifadhi na kuvamia makazi ya watu.
Amesema “Tusifanye
mzaha kwa hili, na hakuna siasa hapa, sio kwamba tunawajali wanyama kuliko
wananchi hapana, watu wameingia katika maeneo ya hifadhi wamesababisha wanyama
watoke huko na kuja kuvamia watu, mpaka sasa wananchi saba wameshafariki, tuwe
wakali kweli kwa wavamizi hawa”.
Madiwani wa
halmashauri ya Wilaya ya Manyoni wakifuatilia kwa umakini hoja zikijadiliwa
katika baraza maalumu la madiwani la kujadili hoja za Mkaguzi na Mdhibiti wa
Hesabu za Serikali.
Kaimu Mkuu wa Wilaya
ya Manyoni Miraji Mtaturu akizungumza katika baraza maalumu la madiwani la
kujadili hoja za Mkaguzi na Mdhibiti wa Hesabu za Serikali.
Mkaguzi wa ndani na Mweka hazina wa Halmashauri
ya Wilaya ya Manyoni wakipitia hoja zilizowasilishwa katika baraza maalumu la
madiwani la kujadili hoja za Mkaguzi na Mdhibiti wa Hesabu za Serikali.
No comments:
Post a Comment