Saturday, May 06, 2017

RC SINGIDA; MKURUGENZI SINGIDA DC HAMIA KATIKA HALMASHAURI YAKO.



Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt. Rehema Nchimbi akisisitiza jambo katika baraza la madiwani la Halmashauri ya Wilaya ya Singida.

Mkurugenzi wa halmashauri ya Wilaya ya Singida Rashid Mandoa ameagizwa kuhakikisha ofisi za halmashauri hiyo zinahamia ndani ya eneo la halmashauri hiyo na kutoka walipo sasa katika manispaa ya Singida.

Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt. Rehema Nchimbi ametoa agizo hilo jana wakati akikabithi vyeti kwa madiwani wa halmashauri ya Singida walipohitimu mafunzo kuhusu jitihada za jamii kupitia mbinu shirikishi ya fursa na vikwazo kwa maendeleo iliyoboreshwa na usimamizi wa miradi ya maendeleo.

Dkt. Nchimbi amesema endapo mkurugenzi atahamishia ofisi na watendaji katika halmashauri yake watapata ubunifu wa kutatua shida na kero za wananchi na hivyo kuiendeleza halmashauri.

“Ukikaa kwenye nyumba inayovuja ndipo utapata akili na ubunifu wa kutatua changamoto hiyo, ukiangaia wanufaika wa Tasaf wameweza kufanya mambo mazuri kwa pesa kidog waliyonayo, mkurugenzi uige mfano huo, mhamie katika halmasahuri yenu, wananchi hawafurahii kuwaona ninyi na watendaji wengine mkiishi manispaa” amesisitiza Dkt. Nchimbi.

Ameongeza kuwa kusitasita kwao kutohamia katika halmashauri yao kutasababisha halmasahuri hiyo ikavunjwa na hivyo kukosa ajira kwa watumishi huku akiwaeleza madiwani kuwa wataponzwa wa kukosa kura katika uchaguzi ujao kwani wananchi wangependa kupata huduma kwa ukaribu.

Dkt. Nchimbi amesema kuhusu makao makuu ya halmashauri hiyo baraza la madiwani litachagua makao makuu yao huku akishauri wazingatie eneo ambalo litafaa kwakuwa Halmashauri hiyo inapitiwa na miradi mbali mbali ya kitafa ikiwemo mradi wa bomba la mafuta kutoka Uganda hadi Tanga na ujenzi wa kituo cha jeshi.

Akizungumzia mafunzo waliyopea amesema ana imani kuwa sasa mafunzo hayo yataleta matokeo mazuri ikiwa ni pamoja na kuwa na lugha nzuri ya kuwasiliana na wananchi na kujisogea pamoja na wananchi, huku akiwaasa wasitumie kauli za kuwakatisha tama wananchi.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Singida Elias Tarimo amesema mafunzo yatawasaidia madiwani kusimamia miradi ikamilike na iwe na ubora unao takiwa huku akitarajia kuona wananchi wakiibua na kukamilisha miradi ya maendeleo.

Tarimo ameongeza kuwa madiwani wanapaswa kuhakikisha simu huu wa mavuno wananchi wanavuna na kuhifadhi mazao yao vizuri pamoja na kuwaelimisha wayatumie vizuri ili wapate fedha za kujiendeleza.

Kwa upande wao madiwani hao wamesema mafunzo hayo yamekuwa msaada kwao kwa kuwaelimisha majukumu yao na mipaka yao ili waweze kitekeleza kwa ufanisi uwakilishi wao wa wananchi.

Wamesema wengi walikuwa hawafahamu mipaka yao na hivyo kushindwa kutekeleza baadhi ya majukumu huku wakieleza kuwa mafunzo yameimarisha ushirikiano baina yao na watendaji tofauti na hapo awali.
Madiwani wa halmashauri ya Wilaya ya Singida wakifuatilia kikao cha baraza hilo.
 

Mkurugenzi wa halmashauri ya Wilaya ya Singida Rashid Mandoa (katikati) akimsikiliza kwa makini Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt. Rehema Nchimbi (kulia kwake) na kushoto kwake ni Mwenyekiti wa Halmashauri ya Singida Eliya Digha.


Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt. Rehema Nchimbi akitunuku cheti kwa mmoja wa madiwani waliohitimu mafunzo ya jitihada za jamii kupitia mbinu shirikishi ya fursa na vikwazo kwa maendeleo iliyoboreshwa na usimamizi wa miradi ya maendeleo.

No comments:

Post a Comment