Thursday, May 04, 2017

ACHENI KUWAITA WANANCHI MASIKINI, WA CHINI; DKT. NCHIMBI AELEKEZA.



Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt. Rehema Nchimbi akimkabidhi Diwani Viti maalum kata ya Ibaga Habiba Issa cheti cha mafunzo ya usimamizi wa miradi na jitihada za jamii za mbinu za kutambua fursa na vikwazo.


Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt. Rehema Nchimbi akizungumza na madiwani kabla hajawapatia vyeti vya mafunzo ya usimamizi wa miradi na jitihada za jamii za mbinu za kutambua fursa na vikwazo.


Wanasiasa wameshauriwa kuacha kuwakatisha tamaa wananchi kwa kuwaita masikini hali inayosababisha washindwe kuchangia na kushiriki kikamilifu katika miradi na shughuli za maendeleo hususani miradi ambayo ina ufadhili kidogo wa serikali na wahisani.

Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt. Rehema Nchimbi ametoa katazo hilo kabla ya kugawa vyeti kwa waheshimiwa madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama waliofuzu mafunzo kuhusu jitihada za jamii kupitia mbinu shirikishi ya fursa na vikwazo kwa maendeleo iliyoboreshwa na usimamizi wa miradi ya maendeleo.

Dkt. Nchimbi amesema wanasiasa akitoa mfano wa madiwani wamekuwa wakisema wananchi ni masikini na wa chini kauli zilizokuwa zikiwakatisha tama ya kuchangia maendeleo kwa kiwango kikubwa na kujiona hawana uwezo huo.

“Mnawaita wananchi wa chini nani amewaweka ninyi juu? Inapofika wakati wa michango ya maendeleo mnasema wananchi ni masikini hawawezi kuchangia, nawaambia mkitoka hapa kwenye mafunzo mkatubu na muifute kauli ya kuwaita masikini, wananchi hawa ni msingi wa maendeleo na wana mchango mkubwa kwa maendeleo ya halmashauri” amesisitiza.

Ameongeza kuwa kumekuwa na kutokuaminiana kati ya madiwani na watendaji hali inayowafanya kutupiana lawama pale jambo linapoharibika badala ya kutafuta suluhu kwa pamoja ili wananchi wapate huduma na maendeleo kwa haraka.

Dkt. Nchimbi amesema mafunzo hayo waliyopewa yaonyeshe tofauti kati ya zamani na sasa huku akisisitiza kutumia fursa zilizopo vizuri na halmashauri kusimamia na kuhakikisha wananchi wananufaika na fursa zilizopo katika halmashauri yao.

Madiwani na watendaji kwa kauli moja wamekubali kuwa kabla ya mafunzo kumekuwa na kutokuaminiana na kusababisha shughuli kutofanikiwa kwa kukosa ushirikiano wa wananchi, wanasiasa na watendaji wenyewe ila baada ya mafunzo wanasiasa na watendaji watafanya kazi kwa kushirikiana na kuwahusisha wananchi ili wao ndio waibue miradi na kuimiliki.

Diwani Viti Maalumu kutoka kata ya Kinyangiri Eunice Kalaila amesema mafunzo hayo yatawafanya waweze kusimamia fedha zinazotolewa na serikali ili ziweze kukamilisha miradi kwa gharama na ubora sahihi.

Kalaila ameongeza kuwa kutokana na mafunzo hayo utoaji wa taarifa utakuwa yakinifu huku miradi yote iliyosimama kwa kukosa ushirikiano wa wananchi itaendelea na kukamilika huku wananchi wataelimishwa kutambua fursa zilizopo na kuibua miradi yao watakayoikamilisha wenyewe na si kuitegea serikali.

Kwa upande wake Diwani Viti Maalumu kutoka Kata ya Ibaga Habiba Issa amemkabidhi mkuu wa mkoa matunda ya asili aina ya furu huku akisisitiza kuwa sasa vijana wataelekezwa kutambua fursa zilizopo kuliko kusubiria ajira za serikali huku akitoa mfano wa fursa ya kutengeneza juice kutokana na matunda hayo ya asili.

Naye Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mkalama Godfrey Sanga amesema atahakikisha anasimamia maelekezo yote ili wananchi wake wapate huduma nzuri na maendeleo kwa haraka huku akiamini lawama na malalamiko yatapungua.

Sanga amesema sasa hakuta kuwa na uhasama kati ya watendaji na wanasiasa na hivyo ushirikiano huo utasaidia katika kuibua na kusimamia miradi pamoja na kutambua na kuzitumia fursa za maendeleo zilizopo Mkalama.
Madiwani na watendaji kutoka halmashauri ya Mkalama wakimsikiliza Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt. Rehema Nchimbi alipokuwa akizungumza nao kabla hajawapatia madiwani vyeti vya mafunzo ya usimamizi wa miradi na jitihada za jamii za mbinu za kutambua fursa na vikwazo.


Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt. Rehema Nchimbi akipokea na kufurahia zawadi ya matunda asilia aina ya furu kutoka kwa  Diwani Viti maalum kata ya Ibaga Habiba Issa mara baada ya mafunzo ya usimamizi wa miradi na jitihada za jamii za mbinu za kutambua fursa na vikwazo, matunda aina ya furu yanaweza kutengenezwa juice na kuwa fursa ya ajira kwa vijana.

Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt. Rehema Nchimbi akimuonyesha Mkuu wa Wilaya ya Mkalama Mhandisi Jackson Masaka zawadi ya matunda asilia aina ya furu aliyopewa na  Diwani Viti maalum kata ya Ibaga Habiba Issa, matunda hayo yanaweza kutengenezwa juice na kuwa fursa ya ajira kwa vijana.

No comments:

Post a Comment