Thursday, September 29, 2016

MKUU WA WILAYA YA MANYONI AWASIMAMISHA WATUMISHI WATANO KWA UZEMBE ,UTOVU WA NIDHAMU NA KUTOTIMIZA WAJIBU WAO.

Mkuu wa Wilaya ya Manyoni Geofrey Mwambe



TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Mkuu wa Wilaya ya Manyoni Mh. Geoffrey Idelphonce Mwambe amewasimamisha kazi watumishi watano wa Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni kwa kushindwa kutekeleza majukumu yao vizuri, uzembe na utovu wa nidhamu.
Mwambe amefanya uamuzi huo alipokuwa kwenye Mkutano na Wafanyakazi wa Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni leo Tarehe 29.09.2016, ambapo aliwataja Watumishi hao aliowasimamisha kazi kuwa ni Mkuu wa Idara ya Ugavi Bw. Genesius Rugemalira ambaye amesimamishwa kwa kushindwa kusimamia manunuzi ya Halmashauri na kuisababishia Serikali hasara ya Tshs. Mil 16, Daktari John Amita wa Hospitali ya Wilaya ya Manyoni aliyesimamishwa kazi kwa tuhuma za kupigana na daktari mwenzake hospitalini hapo, tuhuma za utoaji mimba, na uzembe uliopelekea kifo cha mama mjamzito.
Wengine waliosimamishwa ni Muuguzi wa Hospitali ya Wilaya ya Manyoni Bw. Mika Iloti kwa uzembe uliopelekea kifo cha Mama mjamzimzito, Msaidizi wa Ofisi Bw. Anthony Sanga kwa ufujaji wa mapato ya Halmashauri na Mtendaji wa Kijiji cha Makasuku Bw. Mussa Ndahani ambaye kwa kushirikiana na Mwenyekiti wa Kijiji chake wamekuwa wakitoa vibali vya uvunaji Misitu kwa Wafanyabiashara ya mbao bila kuzingatia sheria na taratibu kwa kofia ya zoezi la utengenezaji wa madawati linaloendelea.
Mh. Mwambe amemwagiza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni kuhakikisha Watumishi hao wanasimamishwa mara moja kupisha uchunguzi wa tuhuma zinazowakabili ili hatua Zaidi za kisheria zichukuliwe dhidi yao.
Wakati huo huo Mkuu huyo wa Wilaya ya Manyoni ametoa karipio kali na kumwagiza Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni Bw. Charles Edward Fussi kuwachukulia hatua Mganga Mkuu wa Wilaya ya Manyoni Dkt. Francis Mwanisi kwa kuficha taarifa na kufumbia macho matukio ya utovu wa nidhamu wa Madaktari na wauguzi wa Hospitali ya Wilaya ya Manyoni na Mhasibu Mkuu wa mapato Bw. Elias Mwachinyemba kwa kushirikiana na wazabuni wa ukusanyaji mapato ya Halmashauri waliomaliza muda wao kuhujumu mapato ya Halmashauri.
Mh.Mwambe pia ametengua uteuzi wa Kaimu Mkurugenzi wa Mji mdogo wa Manyoni, Bw. Yona Chalinze na Kaimu Mhandisi wa Maji Bw. Musoma Kanyere kwa utendaji kazi usioridhisha.
Akitoa maamuzi hayo Mh. Mwambe amewaeleza Watumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni kuwa ni lazima waelewe kuwa wao sio tu Watumishi wa Serikali bali ni Watumishi wa Umma hivyo wana wajibu kuutumikia umma kwa weledi, kujituma, uadilifu na kuacha kufanya kazi kwa mazoea lakini pia kuepuka vitendo vya Rushwa.

Imetolewa na:
Veronica D. Luhaga,
Afisa Habari,
HALAMASHAURI YA WILAYA
MANYONI.
0786-848497

No comments:

Post a Comment