Tuesday, April 01, 2014

SINGIDA SASA NI DIJITALI



Mji wa Singida sasa unapokea matangazo ya televisheni katika mfumo mpya wa dijitali unaotoa fursa ya kupata chaneli nyingi na matangazo yenye ubora zaidi.

Meneja Mawasiliano wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) Innocent Mungy amesema Mikoa ya Singida na Tabora ni sehemu ya awamu ya pili ya uzimaji wa mitambo ya analojia nchini.

Meneja Mawasiliano Mamlaka ya Mawasiliano Nchini (TCRA) Innocent Mungy akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani) kuhusu kuhamia dijitali Mji wa Singida. Kushoto kwake ni Mhandisi wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania Injinia Andrew Kisaka.

Mungy amesema wananchi na wadau wa sekta ya utangazaji Mkoa wa Singida wamepewa elimu kupitia njia mbalimbali kuhusu kuhamia katika  teknolojia ya mfumo wa utangazaji wa dijitali.

Amewatahadharisha wananchi wa Singida wasitupe televisheni za zamani bali wanapaswa kununua ving'amuzi kwa wasambazaji wanaotambulika ili waweze kupata fundi wa kuwafungia ving'amuzi kwa usahihi.

Mungy amesema mamlaka imehakikisha uwepo wa wasambazaji na mafundi wa kutosha kwa mji wa Singida ambapo tayari mawakala sita wametambuliwa.

Amefafanua kuwa uzimaji wa mitambo ya analojia hautawaathiri wananchi wanaopokea matangazo ya Televisheni kwa kutumia 'cable' na 'satellite'.

 Mfano wa 'dish' ambalo mtumiaji hataathirika na uzimaji wa mitambo ya analojia.

Mitambo ya analojia kwa  miji ya Singida na Tabora imezimwa saa sita kamili usiku Machi 31, 2014.

No comments:

Post a Comment