Wednesday, August 31, 2016

MKUU WA MKOA AKABIDHI MADAWATI 630 YA WADAU KWA WAKURUGENZI.

Mkuu wa Mkoa wa Singida Mathew J. Mtigumwe akimkabidhi Mkurugenzi wa Halmashauri ya Ikungi Rustika Turuka madawati yaliyochangwa na wadau mbalimbali wa maendeleo Mkoani Singida.

Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhandisi Mathew J. Mtigumwe amekabidhi madawati 630 kwa wakurugenzi wa halmashauri saba za Mkoa wa Singida yakiwa ni mchango wa wadau na taasisi mbalimbali zilizojitolea kuunga mkono uchangiaji wa madawati mkoani hapa.

Katika makabidhiano hayo yaliyofanyika  katika Ukumbi wa Ofisi za Mkoa Mtigumwe amesema kuwa hali ya Madawati ilikuwa chini ya asilimia 40 lakini chini ya uongozi wake kwa kushirikiana na wadau 67 wa Maendeleo wameweza kuchangia jumla ya shilingi milioni 42,626,500 na kufanikisha lengo la utengenezaji wa madawati kwa asilimia 98.

Ameongeza kuwa upungufu Mkubwa ulikuwa zaidi katika Halmashauri za Singida na Manyoni huku akiwataka Wakurugenzi hao kuyachukua madawati hayo haraka na kuyapeleka Katika shule zenye upungufu mkubwa ili kuboresha mazingira ya kujisomea.

Mtigumwe ameeleza kuwa mwanzoni mwa mwezi June mwaka huu aliteua kamati ndogo ya uratibu wa madawati kwa kushirikisha wadau mbalimbali katika Mkoa baada ya kuona juhudi za serikali kupitia mamlaka za Halmashauri ya Manispaa na Wilaya na kamati hiyo ilifanikiwa kukusanya milioni 42,626, 500.

Amesema wadau waliojitokeza na kuunga mkono juhudi za halmashauri ni wadau 60 waliochanga pesa taslimu 29,046,500, wadau watano waliotoa madawati 60 yenye thamani ya shilingi 3,580,000 na kampuni ya Bonite Bottlers iliyotoa madawati 100 yenye thamani ya shilingi 10,000,000.

Naye Mwenyekiti wa kamati ya kuratibu  harambee ya madawati Elias Donaty Seng’ongo amefafanua kuwa kamati ilishirikisha wadau mbalimbali na walioweza kushiriki ni pamoja na taasisi za serikali (TBA, Gispa, Tanroads, Sido, Veta, Temesa, Sekretarieti ya Mkoa, Takukuru na TRA), Mashirika ya huduma (NHC, Tanesco, Suwasa na Posta), taasisi za fedha (NMB na CRDB), Mifuko ya hifadhi ya jamii (NHIF, NSSF, na PSPF) na Mashirika yasiyo ya serikali (NGO’s, SEMA, HAPA, TUNAJALI, na HELVETAS).

Seng’ongo amewataja wadau wengine waliochangia kuwa ni Vyuo na idara za serikali (NAO, Madini, Hazina Ndogo, Chuo cha Uhasibu, TIA, Utumishi wa Umma, Chuo cha walimu Singida, Abet English Medium School, Maasai English medium  School, Lake School), Viwanda vya usagishaji mafuta (Mount Meru na Umoja wa wakamuaji mafuta Mkoa wa Singida), Wafanyabiashara mbalimbali, wauzaji wa vinywaji baridi (Bonite Bottles Ltd), Wauzaji wa vipuri vya magari, Makandarasi, Wakala wa huduma za misitu TFSA, maduka ya vifaa vya ujenzi, Hoteli, Baba na Mama Lishe wa mkoani humo.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Ikungi Rustika Turuka akipokea madawati 90 kama sehemu ya mgao wa madawati hayo amewashukuru wadau na Mkuu wa Mkoa kwa juhudi zao za kuwaunga mkono ili kufanikisha lengo la serikali la kuhakikisha kuwa hakuna mwanafunzi wa shule ya msingi na sekondari anayekaa chini.

Turuka amesema kwa niaba ya wakurugenzi wote waliopokea madawati hayo watahakikisha wanayaelekeza katika maeneo yenye upungufu na kusimamia yanatunzwa huku akiongeza kuwa madawati hayo yataboresha  mwandiko na ufahamu wa wanafunzi hivyo kuinua kiwango cha ufaulu Mkoani Singida.

Akiwakilisha wadau waliochangia madawati, Mkulima na Mfugaji Hassan Tati amesema kuwa Mkuu wa mkoa wa Singida Mhandisi Mathew J. Mtigumwe amebuni njia nzuri ya kuwapa motisha kwa kutoa Hati kwa wadau wote waliochangia jambo ambalo litaamsha ari zaidi katika kuchangia shughuli za Maendeleo ya Mkoa na taifa kwa ujumla.

Tati amesema kuwa inasikitisha sana pale anaposikia kuwa mkoa wa Singida unashika nafasi ya Tano kwa umasikini katika Mikoa yote nchini ilihali ni mkoa wenye rutuba ya kutosha na eneo pana katika uwekezaji hivyo amewasihi wananchi na wadau kwa pamoja kushirikiana kwa pamoja katika kukomesha umasikini huo.

Mfanyabiashara Salum Nagji akipongezwa na kupewa hati ya shukrani kutoka kwa Mkuu wa Mkoa wa Singida Mathew Mtigumwe kama mdau mmojawapo aliyechangia madawati, anayesoma taarifa ni Mwenyekiti wa Kuratibu harambee ya madawati Elias Seng'ongo na katikati ni Katibu Tawala Mkoa wa Singida Dokta Angelina Lutambi.

Sehemu ya madawati yaliyochangwa na wadau mbalimbali wa maendeleo Mkoani Singida.

Mkuu wa Mkoa wa Singida Mathew Mtigumwe na kulia kwake ni Katibu Tawala Mkoa wa Singida Dokta Angelina Lutambi wakiwa wameketi katika madawati na Wakuu wa Wilaya za Mkoani Singida, waliosimama ni wakurugenzi wa halmashauri za Wilaya ya Singida mara baada ya makabidhiano ya madawati.
 
Mkuu wa Mkoa wa Singida Mathew Mtigumwe na kulia kwake ni Katibu Tawala Mkoa wa Singida Dokta Angelina Lutambi wakiwa wameketi katika madawati na Wakuu wa Wilaya za Mkoani Singida, waliosimama ni baadhi ya wadau waliochangia madawati.

No comments:

Post a Comment