Tuesday, January 24, 2023

Waliokula fedha za CHAMWAI dawa yao inachemka - Serukamba

 

Hali ya Chama cha Walimu cha akiba na mikopo cha Wilaya ya Iramba (CHAMWAI) imeendelea kuwa  tete baada shauri lao na Mkuu wa Mkoa wa Singida kuahirishwa ili kutafutwe nyaraka husika.

Shauri hilo limesogezwa mbele mpaka tarehe 31 Januari 2023  ili kutoa fursa kwa wahusika kuandaa nyaraka ambapo ameelekeza kuletewa  jalada la chama hicho lililopo CRDB likiwa na nyaraka zote muhimu, Wakurugenzi wa Halmashauri ya Iramba na Mkalama kuleta nyaraka zote zenye uhusiano na chama hicho.

Kauli hiyo imetolewa leo na RC Serukamba alipokutana na Walimu wastaafu katika ukumbi wa mikutano wa Ofisi hiyo ambapo walieleza kwamba madai yao ni zaidi ya Milioni 300.

RC Serukamba alieleza kwamba analazimika kuahirisha kikao hicho ili kutoa nafasi ya kuzipata nyaraka zote tokea chama hicho kilipoanzishwa lengo likiwa sio kupata madeni ya walimu hao bali kuangalia fedha nyingine za chama hicho ambazo zimeibwa.

Amesema ni kweli yapo madeni yanayotakiwa kulipwa na Halmashauri ya Iramba zaidi ya Milioni 20 na Mkalama zaidi ya milioni 14 lakini inawezekana zipo fedha nyingine ambazo CRDB wanatakiwa kutoa maelezo jinsi walivyozitoa pasipo kufuata utaratibu.

"Mikopo yote ina utaratibu wake hivyo nataka kuona muhutasari unaoruhusu kuchukuliwa mkopo huo na masharti kama yamefuatwa" alisema Serukamba

"Tukisema tuwaambie Wakurugenzi waliotumia fedha za chama hicho watafanya hivyo lakini inawezekana walimu wanapata hela zao lakini chama kinaendelea kupoteza haki zao" Aliendelea kueleza Serukamba

Hata hivyo RC amemuagiza DC wa Iramba Seleimani Mwenda kuhakikisha siku ya kujadili tena swala hilo wawepo waliokuwa viongozi wa CHAMWAI wa awali ili kujibu hoja zitakazojitokeza.

Kwa upande wa msemaji wa wastaafu hao Mlogwa Temaeli amesema wameridhishwa na utaratibu uliowekwa na RC Serukamba wa namna ya kutatua swala lao huku akieleza kwamba wamepata matumaini mapya.

MATUKIO MBALIMBALI KATIKA PICHA




Mkutano ukiendelea

No comments:

Post a Comment