Thursday, June 27, 2024

WAKUU WA IDARA, VITENGO WATAKAOZALISHA HOJA ZA CAG KUWAJIBISHWA - RC DENDEGO

Mkuu wa Mkoa wa Singida Halima Dendego, ameagiza kuchukuliwa hatua kwa Wakuu wa Idara ambao watazalisha hoja mpya za Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kama hatua ya kuimarisha utendaji kazi kwenye Halmashauri hizo.

Mkuu huyo wa Mkoa wa Singida ametoa kauli hiyo (26/Juni/2024) katika Kikao Maalum cha kujadili hoja za CAG cha Baraza la Madiwani wa Halmashauri ya Manispaa ya Singida.

Dendego ametoa agizo hilo kufutia Halmashauri ya Manispaa ya Singida kuwa na hoja 64 kutoka mwaka wa fedha 2011 hadi Juni 2024 ambazo hazijafungwa jambo ambalo amesema sio zuri na linatia dosari katika kutekeleza sheria, kanuni na taratibu za Serikali hasa katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

Ameonya kuwa hataki kusikia uzalishaji wa hoja mpya zinazalishwa tena na kama zikitokea basi aliyesababisha hoja hiyo aitwe na kuhojiwa kwa nini hoja hiyo imetokea ikiwezekana achukuliwe hatua kwa kusababisha hoja hiyo.

Amesema hoja hizo zinapotokea zinasababishwa na kuwepo kwa kasoro hasa katika usimamizi hafifu wa miradi ya maendeleo.

Katibu Tawala wa mkoa wa Singida Dkt. Fatuma Mganga, akizungumza kwenye mkutano huo maalum wa baraza la Madiwani kuadili hoja za ukaguzi katika Halmashauri ya Manispaa ya Singida.

Naye, Katibu Tawala wa mkoa wa Singida Dkt. Fatuma Mganga ameonyesha kukerwa na uwajibikaji hafifu wa Watendaji wa Manispaa ya Singida katika kujibu hoja za CAG licha ya ushauri uliowapatia katika kikao cha Kamati ya Fedha.

Dkt. Mganga amesema mambo mengi walioshauri ambayo yangesaidia kwa kiasi kikubwa kumaliza hoja za CAG hayajafanyiwa kazi jambo ambalo ameonya lazima likome na Watendaji lazima wawajibike ipasavyo katika kuondoa kasoro hizo.

Amewataka Wakuu wa Idara katika Halmashauri za mkoa huo kuacha uzembe na kuhakikisha hawazalishi hoja mpya za CAG na kujibu kwa uhakika hoja zilizopo ili ziweze kufungwa na CAG.

Mstahiki Meya wa Manispaa ya Singida Yagi Kiaratu, akizungumza kwenye mkutano huo maalum wa baraza la Madiwani kuadili hoja za ukaguzi katika Halmashauri ya Manispaa ya Singida.

Kwa upande wake, Mstahiki Meya wa Manispaa ya Singida Yagi Kiaratu, amemhakikishia Mkuu wa mkoa wa Singida kuwa watafanyia kazi maelekezo yao ili kuhakikisha hoja 64 za CAG zinafanyiwa kazi ili kuhakikisha Manispaa ya Singida inakuwa bora katika utendaji wake wa kazi.

Mkuu wa Wilaya ya Singida Godwin Gondwe, akizungumza kwenye mkutano huo maalum wa baraza la Madiwani kuadili hoja za ukaguzi katika Halmashauri ya Manispaa ya Singida.

 Mkaguzi Mkuu Ofisi ya Mdhibiti wa Hesabu za Serikali Mkoa wa Singida Othman Jumbe, akishauri jambo kwenye mkutano huo maalum wa baraza la Madiwani kujadili hoja za ukaguzi katika Halmashauri ya Manispaa ya Singida.

Mkutano ukiendelea

Wakuu wa Idara na Vitengo wa Manispaa ya Singida wakiwa kwenye Kikao cha Baraza la Madiwani cha kujadili hoja za CAG.

Sehemu ya Madiwani wa Halmashauri ya Manispaa ya Singida wakishiriki mkutano huo maalum wa baraza la Madiwani kujadili hoja za ukaguzi Singida mjini.

No comments:

Post a Comment