Wednesday, March 27, 2024

RC DENDEGO : NATOA SIKU 30 KILA MKURUGENZI ANIPE TAARIFA YA VIFAA TIBA

MKUU wa Mkoa wa Singida, Halima Dendego, ametoa muda wa mwezi moja kwa Wakurugenzi wa Halmashauri zote za Mkoa huo kumpatia taarifa za vifaa tiba vilivyoletwa na Serikali kwenye Hospitali za Wilaya, Zahanati na Vituo vya Afya ili kuweka mkakati wa kutunza vifaa hivyo ipasavyo.

Dendego ametoa kauli hiyo leo Machi 27, 2024 Wilayani Ikungi katika mwendelezo wa ziara yake ya kikazi ya kukagua miradi ya maendeleo pamoja na kuzungumza na Viongozi, Watumishi wa Umma, na Wakuu wa Taasisi za Umma mkoani humo.

Amesema vifaa vinavyotolewa na Serikali katika Hospitali, Vituo vya Afya na Zahanati nchini ni ghali mno hivyo ni muhimu kwa kila watumishi kuhakikisha wanavitumia kwa ufasaha katika kutoa huduma bora kwa wananchi na kuvitunza ili viweze kudumu kwa muda mrefu.

“Haya majengo ni yetu sote wala hayajamlenga mtu yeyote ni sisi tuliokuwepo hapa na wengine ni muhimu yakalindwa na kutunzwa kwa sababu huwezi kujua siku wala saa utakapoumwa”

Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mhe. Halima Dendego akizungumza na Watumishi wa Umma katika Halmashauri ya Wilaya ya Ikungi Mkoani Singida

Kuhusu huduma za Wazee, Mkuu wa Mkoa huyo ameagiza kila Halmashauri katika Mkoa huo kutenga bajeti kwa ajili ya kununulia dawa za Wazee kama hatua ya kuondoa malalamiko kuhusu uduni wa utoaji wa huduma za afya katika kundi hilo.

Amesisitiza kuwa itakuwa ni jambo zuri kama hata maeneo yanayotoa huduma za matibabu kwa wazee yawekewe maji na chai kwa sababu Wazee hao wametumikia Taifa hivyo ni muhimu wakatunzwa na kuhudumia vizuri.

“Tengeni fedha zinazotokana na mapato ya ndani kwa ajili ya kununua dawa za wazee kwa sababu magonjwa yao yanajulikana” Dendego amesisitiza.

Nao Viongozi wa Wilaya ya Ikungi wamemshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa upatikanaji wa fedha za kutusho hususan ndani ya uongozi wake wa miaka mitatu kuwezesha ukamilishaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo na kumuahidi Mkuu huyo wa Mkoa kutekeleza maagizo aliyoyatoa ili wananchi waweze kupata huduma bora na za uhakika karibu na maeneo yao.

Akiwa Wilayani Ikungi, Dendego ametembelea na kukagua miradi ya maendeleo ikiwemo mradi wa maji wa kijiji cha Matare, Hospitali ya Wilaya ya Ikungi, Ujenzi wa barabara ya Matongo kwa kiwango cha lami na Shule ya kisasa ya Mtaturu.

MATUKIO KATIKA PICHA

Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mhe. Halima Dendego akizungumza na Wanafunzi wa shule ya Msingi Mtaturu iliyopo Wilayani Ikungi wakati wa ziara yake.


Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe. Halima Dendego, akisisitiza jambo wakati alipotembelea Ujenzi wa barabara ya Matongo kwa kiwango cha lami uliyopo katika halmashauri ya Wilaya ya Ikungi. 








Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe. Halima Dendego, akishuhudia upatikanaji wa maji safi na salama katika mradi wa maji wa kijiji cha Matare wilayani Ikungi unaohudumia wananchi zaidi ya 5036. 

Mkuu wa Mkoa wa Singida akikagua miundombinu ya mradi wa maji katika kijiji cha Matare wilayani Ikungi wakati wa ziara.

Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Thomas Apson, akitoa taarifa ya hali ya usalama katika Wilaya ya Ikungi kwa Mkuu wa Mkoa wa Singida wakati wa ziara yake ya kujitambulisha na kukagua miradi.

Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Ikungi Justice Kijazi, akisoma taarifa kwa Mkuu wa Mkoa wa Singida (hayupo pichani) wakati wa kikao kazi cha kuzungumza na Watumishi wa Umma katika halmashauri hiyo.

Baadhi ya Watumishi wa Umma katika Halmashauri ya Wilaya ya Ikungi wakimsikiliza Mkuu wa Mkoa wa Singida akizungumza nao katika ukumbi wa mikutano wa halmashauri hiyo.

No comments:

Post a Comment