Wednesday, September 08, 2021

Dkt. Mahenge Atembelea Miradi Ya Maji Ya SUWASA Awataka Kuongeza Ukusanyaji Wa Mapato

Mamlaka ya Maji Safi na Mazingira Mkoani Singida (SUWASA) wametakiwa kutumia mbinu mbadala kuongeza ukusanyaji wa mapato   ili waweze kuendeleza miundombinu na kupunguza upotevu wa maji.

Akiongea leo tarehe 07.09.2021 katika ukumbi wa mikutano SUWASA mara baada ya kutembelea miradi mbalimbali ya maji iliyojengwa na mamlaka hiyo  RC Singida Dkt. Binilith Mahenge amesema ukusanyaji wa mapato ukisimamiwa vizuri utasaidia kuongeza mapato na  kukarabati miundombinu na usambazaji wa  maji katika maeneo mengi Zaidi kwa kutumia fedha za ndani.

Aidha Dkt. Mahenge  amebainisha kwamba kiasi cha maji yanayopotea kwa Mkoa wa Singida ni asilimia 33.4  ambayo ni kiasi kikubwa  kikilinganishwa na asilimia 22 ya upotevu inayokubalika hivyo kuwataka SUWASA kuhakikisha upotevu unapungua.

Hata hivyo Dkt. Mahenge ameipongeza SUWASA  kwa kuanzisha miradi mingi ya maji  ambayo imejengwa kwa kutumia fedha za ndani  na kwa viwango vinavyokubalika.

RC ameishukuru Serikali kwa kutoa fedha zaidi ya shilingi bilioni  3.07 ili kutekeleza miradi ya maji iliyopo Manispaa ya Singida, Wilaya ya Iramba na Ikungi

Nawapongeza sana kwa kazi nzuri mliyofanya, Miradi mingi iliyojengwa ina viwango vinavyokubalika kwa fedha za ndani  hii inaonesha ubunifu mkubwa mliutumia  katika kutekeleza miradi hii, niwaombe muendelee kusimamia vizuri makusanyo ili muweze kuanzisha miradi mingine. Alisema Dkt. Mahenge

 Aidha ametoa wito kwa wananchi wote mkoani hapo wanaotumia huduma ya maji kuhakikisha wanalipia huduma hiyo  kwa wakati ili kusaidia Mamlaka kuendelea kusambaza huduma kwa watu wengine .

Naomba muandae  orodha ya Taasisi na watu wote wanao daiwa nizipate ofsini kwangu, lazima mtu aliyepatiwa huduma ya maji na akayatumia alipe, nitoe wito kwa yeyote anayejua kwamba ana deni la maji alipe kabla orodha hiyo haijanifikia. Alisisitiza RC Mahenge.

RC amewakumbusha watumishi wa  SUWASA kuhakikisha kwamba hakuna udanganyifu unaofanyika katika usomaji wa  mita na kuacha ukadiriaji kwa  mteja.

Akimalizia hotuba yake Dkt. Mahenge amewaagiza watumishi  kufanya ukaguzi wa kawaida utakaobaini ubora wa maji katika visima binafsi vinatoa huduma kwa wananchi na kuyapima ili kulinda afya za watu.

Awali Mkurungenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Maji safi na mazingira Mkoani Singida (SUWASA) Mhandisi Patrick Nzimba  amesema  mkoani hapo wametekeleza jumla ya miradi ya maji saba (7)  inayogharimu kiasi cha shilingi  bilioni  3.075 katika Kata za Unyambwe, Minga,  Mungumaji na Vijiji vya  Misigiri na  Ulemo

Aidha amebinisha kwamba Mamlaka ina mpango wa kuongeza uzalishaji wa maji  kwa kuchimba  visima 11  kupitia fedha za miradi 28 ya maji lengo likiwa ni kuhakikisha wananchi wengi wanapata maji.

Mhandisi Patrick amefafanua kwamba SUWASA kwa kushirikiana na RUWASA   watakarabati miradi nane (8)  pembezoni mwa mji  katika maeneo ya Unyamikumbi A, Mtamaa B, Manga, Ititi, Uhamaka,Unyianga Mtamaa A na Mwankoko A ambayo kwa sasa haitoi huduma ya maji.

 Ameendelea kusema kwamba wameweka mkakati wa kuhakikisha  wanaongeza mtandao wa maji kwa kusambaza mabomba  yenye urefu wa zaidi ya Kilometa 10 katika maeno ambayo hayana huduma hiyo.

Hata hivyo ameongeza kwamba  changamoto kubwa  katika utoaji wa huduma ya maji ni  uhaba wa mitandao ya majitaka  ambayo huathiri mazingira  na tayari mipango ya uanzishwaji wa mradi huo umekamilika.

Changamoto nyingine ni kupungua kwa uwezo wa visima kuzalisha maji  na vingine kuwa na maji  chumvi pamoja na uwepo wa mtandao wa mabomba ya zamani  wenye urefu  wa kilometa 40 ambayo husababisha upotevu wa maji. Alisema Mhandisi Patrick.

Aidha Mhandisi  Patrick amemueleza RC kwamba baadhi ya wateja wamekuwa kikwazo kwa kuwa hawalipi  madeni yao kulingana na huduma ya maji wanayoipata hivyo kusababisha deni la shilingi milioni 581.32 ambapo taasisi za Serikali pekee zinadaiwa kiasi cha shilingi milioni  305.

No comments:

Post a Comment