Wednesday, October 21, 2020

UN YAMUUNGA MKONO MAGUFULI KUTOKOMEZA UKATILI WA MWANAMKE IKUNGI

 Ikungi - Singida

Mkuu wa  Mkoa wa Singida Mhe, Dk. Rehema Nchimbi  amezindua  miongoni mwa miradi mikubwa iliyowahi kutekelezwa nchini, mradi wa  pamoja  baina ya Mashirika ya Kimataifa ya UN Women na UNFPA kupitia ufadhiri  wa  Shirika la KOICA wa “Tuufikie usawa  wa jinsia kupitia kuwawezesha wanawake na wasichana” utakaogharimu takribani bilioni 11.5 za kitanzania  ambao utatekelezwa  katika Wilaya ya Ikungi mkoani Singida na Msalala mkoani  Shinyanga katika kipindi cha  miaka mitatu kuanzia sasa.

 Dk. Nchimbi amesema lengo kuu la mradi huo ni kuchangia  katika kuwawezesha  wanawake na wasichana  kuwakwamua kiuchumi na kijamii katika mikoa ya Singida na Shinyanga  ili kufikia usawa wa kijinsia ambapo amewataka watendaji wote wa Serikali ambao watatekeleza mradi huo kuwa makini katika utekelezaji wa mradi ili  malengo ya mradi huo yaweze kufikiwa.

Amesisitiza kuwa Serikali haitasita kuwachukulia hatua kali watendaji ambao  kwa namna moja au nyingine hawataendana na kasi ya utekelezaji wa miradi chini ya Serikali ya awamu ya Tano  inayoongozwa na Rais John Pombe Magufuli ambapo amesema  mrai huo  ni sehemu ya utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi  ili kuwaletea wananchi  maendeleo ya  kweli.

Kwa mujibu wa  Mkurugenzi wa  KOICA  Tanzania, Bi Jieun Mo,  walengwa wasio wa moja kwa moja takribani  wakazi 40,000 kutoka kwenye wilaya  ya Ikungi na Msalala na walengwa  wa moja  kwa moja 2350 wanawake na wasichana  kutoka katika wilaya hizo watanufaika na mradi huu ambapo pia  wanaume na wanawake 6000 wa Wilaya  ya Ikungi watanufaika kwenye eneo la muingiliano wa  hati za ardhi.

Mo ameainisha kuwa  shughuli za mradi katika kuwaweza wanawake  kwenye eneo la uchumi zitajikiza zaidi kwenye kuimarisha uwezo wa wanawake  na vijana   wakulima ili waweze kutumia  njia nzuri za kilimo na hali ya hewa katika uzalishaji wa alizeti na kilimo cha bustani, kukuza uuzaji wa pamoja, ujuzi wa ujasiriamali na wakala wa uchumi  wa wanawake  na kuimarisha  usalama wa ardhi na umiliki.

Amesisiza kuwa  shughuli hizo zitatekelezeka  kupitia kuunda  vikundi vya uzalishaji wa kilimo cha bustani kwa wanawake, kuunganisha  wanunuzi wa vikundi  vya wakulima vya wanawake,kusaidia ujenzi wa  ghala kubwa  moja la alizeti na kituo cha ukusanyaji kilomo cha bustani ili  kuboresha uuzaji wa pamoja na utunzaji baada ya kuvuna, kutoa mafunzo ya ujasiriamali, kutoa mafunzo ya ujasiriamali na ufikiaji wa habari za kifedha na kufuatilia ushauri wa usimamizi wa biashara na  fedha na kukuza  umiliki wa ardhi pekee na wa pamoja  wa wanawake kupitia utoaji wa  Hati za Haki za kimila za Makaazi(CCROs).

Mwakilishi wa UN Women  Bi, Hodan Addou ameishukuru Serikali  ya  Tanzania  kuwa ushirikiano wake katika kuhakikisha  kuwa mradi huu  hatimaye umeanza kutekelezwa ambapo amesema Shirika lake  linaunga mkono juhudi za Serikali za kumkomboa mwanamke ili kuondokana na  unyanyasaji wa kijinsia.

Bi Addou amesisitiza kuwa mradi utasaidia uwezeshaji kijamii kwa kuwawezesha  wanawake kusimamia haki zao, kujenga ujuzi wa ujasiiamali wa wanawake na wasichana kukabiliana  na unyanyasaji wa kijinsia na kuimarisha mifumo ya kuzuia na kukabiliana na unyanyasaji wa kijinsia kupitia kuanzisha na kuandaa vifaa katika madawati matatu ya  Polisi ya Jinsia na Watoto, kuanzisha  vituo vitatu vya  huduma  ya dharura katika  vituo vya wilaya, kuunda nafasi salama ya umma, kujenga uwezo  wa nambari ya msaada ya watoto kitaifa, kuunda na kuimarisha Klabu za Wasichana na kuunda Kamati za ulinzi na ukatili dhidi ya wanawake na watoto.

Kwa upande wake Mwakilishi Mkazi wa Umoja wa Mataifa Nchini Tanzania  Zlatan Milisic   ameipongeza Serikali kwa kuwa  na mradi huo na kuongeza kuwa mradi huo unaendana na malengo ya endelevu ya 2030 hususani lengo namba 5 kuhusiana kuwaendeleza wanawake  katika nyanja mbalimbali na kuongeza kuwa mwaka 2020 ni mwaka muhimu sana kwa kuwa tunaelekea  katika kutimiza miaka 25 ya azimio la wanawake la Beijing.

Ameeleza kuwa  malengo endelevu ya 2030 yameeleza kuwa ili kufikia maendeleo ya nchi kumtambua mwanamke ni jitihada muhimu sana  katika kuharakisha na kutimiza malengo yote ya maendeleo ambapo ameihakikishia Serikali ya Tanzania kuendelea kufanya kazi kwa karibu sana  ili kuhakikisha wanawake wanakuwa chachu ya maendeleo katika  nchi ya Tanzania.

Mwakilishi wa UNFPA, Dk. Winfred amesema kuwa uzinduzi wa mradi umelenga kutokomeza aina zote za unyanyasaji wa kijinsia  na kuimarisha usawa katika jamii ikiwa ni pamoja na  kuimarisha maisha ya wanawake ambapo amesisitiza kitovu cha matatizo ya kijinsia  ni wanaume na mila na desturi potofu zinazomtazama mwanamke kwa kumdharirisha hivyo juhudi za makusudi  zinatakiwa  kufanywa za kuwaweka wanaume mbele ili kutokomeza unyanyasaji wa kijinsia kwa wanawake.

Naye  Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Edward Mpogolo  amesisitiza kuwa kazi nzuri zinazofanywa na  Rais John Pombe Magufuli katika Nyanja mbalimbali ndiyo zinazoyafanya  jumuiya za kimataifa  kuunga mkono kwa kutoa  misaada  kupitia miradi mbalimbali hapa nchini.

No comments:

Post a Comment