Saturday, November 30, 2019

TAASISI YA UHASIBU NCHINI (TIA) KWA MARA YA KWANZA YATUNUKU SHAHADA KAMPASI ZA SINGIDA NA MWANZA

KWA mara ya kwanza tangu kuanzishwa kwa Kampasi za Singida na Mwanza chini ya Taasisi mahiri na kongwe ya uhasibu nchini (TIA) hapakuwepo na kozi ya Shahada ndani ya kampasi zake za Singida na Mwanza. Hivyo wahitimu wa kozi ya shahada kwa mwaka wa masomo 2018/2019 ndio wanaofanikiwa kuandika historia ya kuhitimu kozi hiyo kwa mara ya kwanza.


Katika mahafali ya 17 ya (TIA) kwa kampasi za Singida, Mwanza na Kigoma, na mahafali ya nane kwa kampasi ya Singida, jumla ya wahitimu 209 wamehitimu kozi ya Shahada, huku wengine 328 wakihitimu kozi ya Stashahada, Astashahada 504 na ngazi ya cheti 647 wote wakihitimu katika kozi za Uhasibu, Ununuzi na Ugavi, Uongozi wa Rasilimali Watu na Usimamizi wa Biashara.

Akizungumza kwenye mahafali hayo, kwa niaba ya Waziri wa Fedha, Dkt Philip Mpango mkoani hapa  jana, Mkuu wa Mkoa wa Singida, Dkt Rehema Nchimbi, mbali ya kupongeza juhudi lukuki zinazofanywa na taasisi hiyo katika kuboresha ubora wa taaluma na wanataaluma, aliwasihi wahitimu hususan wale wa shahada na uongozi mzima wa TIA kuanza kutumia sifa na ubora wa kitaaluma walionao katika kuongeza thamani kwa wananchi walio mitaani hususan vijana.

Dkt Nchimbi aliwatakafarisha na kuwataka wahitimu kujiuliza je sura ya kampasi hiyo huko nje ikoje? Kampasi hii inavyosifika kwa ubora je na akina mama lishe na waendesha bodaboda na bajaji  wanaoizunguka na kuihudumia kila kukicha nao wamepata fursa ya kuambukizwa ubora huo? Je kampasi hizi zinaonekanaje huko nje katika kubadili na kuongeza thamani hususan kwa vijana ili kuchagiza na kuleta chachu ya mabadiliko ya fikra kufikia maendeleo stahiki na ya kiushindani.

“Je haiwezekani TIA kuwa na mafunzo ya muda mfupi kwa vijana wetu, waendesha bodaboda, bajaji, mama lishe na wajasiriamali angalau na wao wakawa na mahafali yao ya kila wiki itapendeza, na itaongeza ubunifu tija na ufanisi ndani na nje ya kampasi zetu kwa maendeleo ya taifa letu,” alisema Dkt Nchimbi

Alisema watumishi wa Singida wamejiwekea kauli mbiu yao inayojulikana kama “ Mshahara wangu uko wapi”? huku akichekesha wahitimu kuwa kuna watumishi ambao wameshapokea mshahara wa mwezi Novemba mwaka huu, lakini ukimuuliza mpaka sasa hauoni Zaidi ya kulalamika mshahara hautoshi! Na kutoa rai kwa wanajumuiya ya TIA kuangalia namna ya kuanzisha somo mahususi la matumizi mazuri ya mshahara (fedha) akiamini ni taasisi hiyo pekee na wahitimu wake ndio jawabu la kutamka kwanini hautoshi, uko wapi na kutupa maarifa na stadi stahiki za siku zote kuiona mishahara yetu.

“Sisi wana Singida kwasasa tupo vizuri, ukimuuliza mtu mshaara wake upo wapi atakuonye mashamba ya korosho, nyumba nzuri, na n.k, hali inayopelekea kumpenda mwajiri wetu”. Dkt. Nchimbi

Aidha, akizungumzia kuhusu ubora wa elimu ndani ya taasisi Dkt Nchimbi alisema fani zinazotolewa na TIA ni muhimu sana katika kuendesha uchumi wa taifa, hususan katika kusimamia mapato na matumizi ya fedha za umma, hivyo aliwataka kuzidisha kasi ya umahiri huo katika kufanikisha azma ya sera iliyopo ya Tanzania ya Viwanda.
Alisema dunia ya sasa imetamalaki teknolojia na utandawazi hivyo jukumu lililopo ni kuendelea kuboresha mitaala ndani ya taasisi ili wakati wote ikidhi viwango vya kimataifa, na kuwasihi kuzidisha kuzalisha wataalamu wenye weledi, maarifa na umahiri wa kutatua changamoto na sio kuziongeza.

“Zingatieni kwa umakini suala la umahiri katika mitaala yenu ili tuweze kuwa na wataalamu wenye uwezo wa kulifikisha taifa kwenye uchumi wa kipato cha kati kabla ya ishirini ishirini na tano (2025),” alisema Dkt Nchimbi

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya Ushauri ya Wizara ya Fedha na Mipango, Wakili Said Musendo Chiguma, alisema jukumu la bodi ya ushauri, pamoja na mambo mengine ni kutoa ushauri kwa TIA kwa nia ya kutekeleza na kuendeleza jitihada za serikali kulingana na malengo makuu yaliyoianzisha.

Chiguma alisema lengo hasa la taasisi hiyo  ni kutayarisha wahitimu kwa uboreshaji endelevu wa mitaala, azma ikiwa ni kuandaa wafanyakazi wenye weledi na uwezo wa kujiajiri, sambamba na maboresho hayo kuzingatia juhudi za kujenga uzalendo, uaminifu na maadili, huku akisisistiza kwamba mhitimu asiye na sifa hizo siyo rasilimali kwa taifa.

Alisema kwa matokeo ya vigezo hivyo taasisi imeendelea kupendwa na kuwa kivutio kikubwa, hali iliyopelekea ongezeko kubwa la udahili wa wanafunzi kila mwaka licha ya kuwepo vyuo vingi vya ushindani idadi inayofikia jumla ya wanafunzi 18,585 katika kampasi zake zote sita ambazo zimesambaa kimkakati.

“TIA ni taasisi ya serikali, imeweza pia kuchangia bilioni mbili na milioni mia tano (2,500,000,000) kama ziada ya mapato yake serikalini,” alisema Wakili Chiguma

Awali, Afisa Mtendaji Mkuu wa TIA, Luciana Hembe, alisema Taasisi hiyo kwa sasa ina kampasi 6 zilizopo katika mikoa ya Dar es Salaam (Makao Makuu), Mbeya, Singida, Mtwara, Mwanza na Kigoma, zote zikiwa na jumla ya wanachuo 18, 587, huku jumla ya kozi zinazotolewa katika kampasi zote ni 20.

Hembe alibainisha kuwa, kwa mwaka 2019 katika kampasi zote kuna jumla ya wahitimu 8695 ikiwa ni ongezeko la asilimia 35.5 ikilinganishwa na wahitimu 6418 kwa mwaka 2018. Alisema mahafali hayo ni kwa wahitimu wa TIA ngazi tofauti Kampasi za Singida, Mwanza na Kigoma kwa mwaka wa masomo 2018/2019.

Alisema idadi ya wahitimu wote waliohudhuria na wasiohudhuria mahafali hayo katika kozi ya Cheti cha Awali, Astashahada na Shahada ni 1,688 wakiwemo wanawake 915 sawa na asilimia 54.21, na wanaume 773 sawa na asilimia 45.79.



No comments:

Post a Comment