Friday, September 20, 2019

MAONESHO YA PILI YA SIDO KITAIFA 2019 KUFANYIKA MKOANI SINGIDA

Akizungumzia maonesho haya Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt. Rehema Nchimbi, amesema hii ni fulsa kwa wote ambao wanahusika na masuala ya uzalishaji mali na kuongeza thamani kwa bidhaa zetu hapa Tanzania. 

Dkt. Nchimbi amesema fulsa nyingine katika maonesho haya ni wajasiriamali kukutana kwa pamoja na kunufaika na fulsa kubwa ambazo zinatengenezwa na maonesho haya ikiwemo fulsa ya masoko. 


“Hapa tutaone teknolojia mbalimbali ambazo zinauwezo mdogo, wa kati na zenye uwezo mkubwa. Tutakutana pia na milango ambayo tulifikiri haipo kumbe ipo kwa ajili ya bidhaa mbalimbali tunazozizalisha kwa kutumia malighafi zetu katika viwanda vyetu” Dkt. Nchimbi 

Kwaupande wake Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la kuhudumia Viwanda Vidogo (SIDO) Bw. Silvester Mpanduji amesema maonesho haya yanatarajiwa kuhudhuriwa na wageni mbalimbali kutoka ndani ya Tanzania na nchi zaidi ya 6 ili kuonesha teknolojia mbalimbali zinazotumika katika kutengeneza bidhaa mbalimbali kupitia viwanda vidogo, vya kati na vikubwa. 

Akifafanua zaidi amesema kutakuwa na wajasiriamali kutoka nchi za Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), Afrika Kusini, Namibia, Kenya, India na China ambapo teknolojia mbalimbali mahususi zitaoneshwa ambazo watu wakiziona watashawishika kwenda kuzitumia na kuanzisha viwanda. 

Aidha, ametoa wito kwa watanzania kwenda kutembelea ili kuona na kununua bidhaa zinazozalishwa na viwanda vyetu na kusisitiza kuwa sasa ni wakati muafaka kwa Watanzania kutumia bidhaa zinazozalishwa hapa nchini kwani ni bora na zenye viwango vya juu. 

Naye Kaimu Mkurugenzi wa masoko na uwekezeji mkoa wa Singida Bi. Shoma Kibende amesema huduma zote za SIDO zitakuwepo wakati wa maonesho ikiwemo ushauri wa kiteknolojia na jinsi ya uanzishaji viwanda na uboreshaji, mafunzo ya kibiashara na ufungashaji ulio bora na utumiaji wa vifungashio. 

Pia kutakuwa na siku ya kuenzi au kuhamasisha utumiaji wa bidhaa zinazozalishwa na viwanda vya ndani ya Tanzania pamoja na uhamasishaji wa mazao mbalimbali yakiwemo alizeti, korosho na mazao mengine. 

Amesisitiza kuwa katika maonesho haya taasisi mbalimbali zitakuwepo ili kutoa huduma ikiwepo Taasisi ya usajili (BRELA) na Taasisi ya Uongezaji Ubora (TBS).


“NDUGU ZANGU NINAWAKARIBISHA NA NINAAMINI HAKUNA MTU ATAKAYEKOSA MAONESHO HAYA MAKUBWA” 
DKT. NCHIMBI


Imetolewa na; 
Kitengo cha Habari na Mawasiliano
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
SINGIDA

No comments:

Post a Comment