Monday, December 24, 2018

VIONGOZI WA KAMATI YA DINI MBALIMBALI MKOA WA SINGIDA WATOA SALAMU ZA KRISMASI NA MWAKA MPYA 2019

Viongozi wa Kamati ya Dini mbalimbali mkoa wa Singida wamewatakia Heri na Baraka wananchi wote wa mkoa wa Singida na Tanzania kwa ujumla katika kipindi hiki cha Krisimasi na kuelekea mwaka mpya 2019, na kuwataka wananchi kusherekea kwa amani na utulivu.

Salamu hizo zimetolewa leo na viongozi hao walipokutana katika ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt. Rehema Nchimbi na wameahidi kuendeleza maombi kwa nguvu zote kwa ajili ya kumuombea Mheshimiwa Rais Dkt. John Joseph Magufuli na Tanzania, ili iendelee kuwa kisiwa cha amani na utulivu.

Makamo mwenyekiti Askofu Kaale akisoma taarifa “Mwanadamu anapoishi hapa duniani hawezi akapata amani kutokana na vitu alivyonavyo kwa wingi kama fedha, dhahabu, magari, nyumba, mashamba na viwanja. Kwa sababu hiyo amani ya Mungu hupatikana kwa Mungu peke yake”

“Tunawahamasisha Watanzania na Singida yetu kwamba kila mtu ampe nafasi Mungu wa kweli amtawale ili kusababisha Amani ya kweli katika nchi yetu ya Tanzania”

Imedaiwa kuwa, amani na utulivu iliyopo nchini Tanzania, imechangia kwa kiasi kikubwa kwa Mheshimiwa Rais wa awamu ya TANO, Dkt. John Magufuli kuishangaza dunia kwa juhudi zake za kuanzisha miradi mikubwa ya maendeleo ndani ya miaka mitatu.

Katika kuijengea nguvu hoja yao hiyo, Askofu Kaale, alinukuu Maandiko Matakatifu kutoka katika Biblia kitabu cha Isaya 32:17  inayosema “Na kazi ya haki itakuwa amani; na mazao ya haki yatakuwa utulivu na matumaini daima”.

“Sisi Kamati ya Dini mbalimbali hapa Mkoa wa Singida, tunaziona na kuzipongeza jitihada za Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Joseph Magufuli”

“Ipo miradi mingi iliyotekelezwa na Serikali ndani ya miaka mitatu ya Rais Magufuli. Amesimamia misingi ya Uchumi, pamoja na changamoto kadhaa zinazoikumba uchumi wa dunia na hata ukanda wa Afrika, Kusini mwa Jangwa la Sahara”

“Katika mwaka 2017/2018 uchumi wa Tanzania umekuwa kwa asilimia 7.1 na kuifanya kuwa ya kwanza kwa Afrika Mashariki, lakini katika takwimu zilizotolewa na Benki ya Dunia (WB) ni ya Tisa kati ya nchi 10 duniani ambazo uchumi wake unakuwa kwa kasi zaidi”  Askofu Kaale akisoma taarifa.

Aidha, Viongozi hao kutoka Madhehebu mbalimbali ya mkoa wa Singida wamesema kwa umoja wao, wanaiunga mkoa Serikali ya Awamu ya Tano na kuwaasa watanzania kuendeleza utamaduni wa kulipa kodi ili fedha hizo zitumike kukamilisha miradi ya maendeleo katika taifa letu la Tanzania.

Naye kiongozi wa dhehebu la Kiislamu mjini hapa, Mbiaji Hassan, ametumia fursa hiyo kuyaomba madhehebu mengine yasiwe kikwazo kwa sikukuu hii ya Krismasi na kuelekea mwaka mpya 2019 na ameyasihi kuhakikisha sikukuu hizi zinasherekewa kwa amani na utulivu.

Hafla hiyo imehudhuliwa na mkuu wa mkoa wa Singida, Dkt. Rehema Nchimbi pamoja na Kamanda wa Jeshi la Polisi mkoani hapa, ACP Sweetbert Njewike.

Kwaupande wake, Kamanda wa Jeshi la Polisi mkoani hapa, ACP, Njwewike, amewatoa hofu waumini wa madhehebu ya dini ya Kikristo na mengine na kwamba wamejipanga vema kuhakikisha sikukuu ya Krismasi na mwaka mpya zinapita vizuri bila kikwazo au usumbufu wa aina yoyote mkoani Singida.

Naye, Mkuu wa mkoa wa Singida, Dkt. Rehema Nchimbi, amesema ni ukweli usiopingika kwamba bei ya amani ni ndogo mno, lakini ikitoweka gharama yake ya kuirejesha ni kubwa mno.

 “Kutokana na ukweli huo, natarajia kila mkazi wa mkoa huu uliopo jirani na makao makuu ya  nchi anashiriki kuitunza na kuilinda amani na utulivu kama ilivyo kwa utamaduni wa mkoa wa Singida. Krismasi haipo kwa ajili ya kumuudhi mtu, ipo kwa ajili ya sherehe zinazotawaliwa na amani”, amesema Dkt. Nchimbi.

Hata hivyo, ametoa wito kwa familia kutumia sikukuu hizi kwa kukaa na familia zao ili kusherekea kwa amani na umoja na amesisitiza kwa wazazi kuwa waangalifu kwa watoto wao.

“Kipindi hiki cha mwisho wa Mwaka ndicho ambacho familia zinatakiwa zikae na kutafakari mwaka mzima yote ambayo yamefanyika na ambayo tumekutana nayo, wapi tumekwenda vizuri, wapi hatukufanikiwa sana. Familia zikae pamoja zitafakari kwa pamoja na katika umoja wetu ni lazima tutashinda”

“Na unapokuta viongozi wa dini mbalimbali wanakaa pamoja na wanakuwa na nia moja na wanawafikia wananchi wao ambao ni waamini wao kwa pamoja, kwa vyovyote mahali hapo Mungu yupo”, Dkt. Nchimbi akielezea zaidi.

“Singida yetu ni Singida ya umoja, ni Singida ya upendo, ni Singida ya mshikamano, ni Singida ya amani, ni Singida ya utulivu na ni Singida ya maendeleo”

“Wakati huu wa Sikukuu ya Noel na  mwaka mpya 2019, nawatakia Watanzania wote moyo wa Upendo, Furaha, Ukarimu na Amani kwa kila mtu, 
KARIBUNI SINGIDA”. Dkt. Rehema Nchimbi.

Salamu kuu: “Dini Mbalimbali - Upendo na Amani"...

MATUKIO KATIKA PICHA


  Mwenyekiti wa Kamati ya dini mbalimba mkoa wa Singida Alhaj. Hamis Kisuke akizungumza.

 Mkuu wa mkoa wa Singida, Dkt. Rehema Nchimbi (kushoto) pamoja na Kamanda wa Jeshi la Polisi mkoa wa Singida, ACP Sweetbert Njewike wakisikiliza kwa makini na kupokea salamu za sikukuu za Krismasi na mwaka mpya 2019 kwa niaba ya wananchi wa mkoa wa Singida kutoka kwa Kamati ya Dini mbalimbali mkoa wa Singida.


 Kiongozi wa dhehebu la Kiislamu mjini Singida, Mbiaji Hassan akizungumza.


 Kamanda wa Jeshi la Polisi mkoa wa Singida, ACP Sweetbert Njewike akizungumza.

 Viongozi wa Kamati ya Dini mbalimbali mkoa wa Singida wakikabidhi kwa maandishi Salamu za Krismasi na Mwaka mpya 2019 kwa Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt. Rehema Nchimbi.

IMETOLEWA NA'
KITENGO CHA HABARI NA MAWASILIANO
OFISI YA MKUU WA MKOA
SINGIDA.
24/12/2018

No comments:

Post a Comment