Sunday, November 19, 2017

MAJARIBIO YA MBEGU CHOTARA YATOA MATUMAINI KWA WAKULIMA WA ALIZETI SINGIDA.





Meneja Msimamizi Maarifa na Mawasiliano kutoka shirika la AMDT Al-amani Mutarubukwa (aliyevaa miwani) akiwaonyesha wakulima na wasindikaji mbegu za alizeti za Chotara kabla ya kufanya majaribio ya usindikaji yaliyoonyesha kuwa mbegu za chotara zinatoa mafuta na mashudu mengi kuliko mbegu za zamani.
Mwakilishi wa Meneja wa Faida Mali Mary Daniel akiwaonyesha wakulima na wasindikaji tofauti kati ya mbegu za alizeti za Chotara na zile za zamani kabla ya kufanya majaribio ya usindikaji yaliyoonyesha kuwa mbegu za chotara zinatoa mafuta na mashudu mengi kuliko mbegu za zamani.

Wakulima na wasindikaji wakishiriki usindikaji wa mbegu za alizeti chotara na zile za zamani katika majaribio yaliyoonyesha kuwa mbegu za chotara zinatoa mafuta na mashudu mengi kuliko mbegu za zamani.
Afisa Kilimo Kutoka Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Singida Mashaka Mlangi akikagua mashudu wakati wa majaribio ya usindikaji wa mbegu za alizeti ambapo matokeo yameonyesha kuwa mbegu chotara zinatoa mafuta na mashudu mengi kuliko zile za zamani.

Mkulima aliyeshiriki majaribio ya kulima mbegu chotara za alizeti Kutoka Ihanja Wilayani Singida John Thomasi akitoa ushuhuda wa ubora wa mbegu hizo kwa wakulima wengine wa alizeti (hawapo pichani).

Wakulima na wasindikaji wa zao la Alizeti Mkoani Singida wameonekana kufurahia na kupata matumaini mapya mara baada ya kushuhudia matokea ya majaribio ya usindikaji wa mbegu chotara ya Alizeti mkoani Singida.

Wakulima na wasindikaji hao wameshuhudia majaribio ya usindikaji wa mbegu chotara ya alizeti yakifanyika katika kiwanda cha kukamua mafuta ya Alizeti cha Nuru mjini Singida, kwa kukamua mbegu chotara na zile za zamani kisha kulinganisha kiwango cha mafuta na mashudu yaliyopatikana.

Mbegu chotara zilizofanyiwa majaribio zimepandwa na wakulima mkoani hapa ikiwa ni sehemu ya majaribio hayo, ambapo matokeo yameonyesha kuwa mbegu chotara zinatoa mazao mengi, mafuta na mashudu mengi, zinatumia muda kidogo shambani mpaka kuvunwa, zinatumia maji kidogo na hazishambuliwi na magonjwa ikilinganishwa na mbegu za zamani.

Mmoja kati ya wakulima aliyeshiriki majaribio ya kulima mbegu hizo Kutoka Ihanja Wilayani Singida John Thomasi alihudhuria pia majaribio ya usindikaji wa mbegu hizo na kusema kuwa sasa wakulima wa alizeti wamepata mwanga kwa kuona namna ambavyo kilimo cha alizeti kwa kutumia mbegu chotara ya alizeti kitawakomboa.

“Mimi ni mmoja kati ya waliolima hizo mbegu chotara kama sehemu ya majaribio na tuliona kwa kuanzia shambani hazisumbui, zinatumia maji kidogo, na mavuno ni mengi, kilichobaki ilikuwa ni kujua ubora wake katika kutoa mafuta na mashudu jambo ambalo tumeshuhudia leo kuwa mbegu hizi zinatoa mafuta mengi kuliko zile za zamani”, amesema Thomasi

Meneja Msimamizi Maarifa na Mawasiliano kutoka shirika la AMDT Al-amani Mutarubukwa amesema shirika hilo linalojikita katika Kilimo cha alizeti nchini hasa katika kuboresha mfumo wa masoko, uzalishaji na usindikaji lilifanya utafiti ulioonyesha kuwa changamoto kubwa ya wakulima wa alizeti ni kutokuwa na mbegu bora.

Mutaburukwa amesema kwakuwa mbegu zilizokuepo zimekuwa hazitoi mazao ya kutosha Shirika hilo lilifadhili majaribio ya mbegu chotara Mkoani Singida kupitia mradi wa Faida Market link kwa kuwezesha wakulima kupanda mbegu hizo.

Ameongeza kuwa matokeo ya majaribio hayo yamekuwa mazuri ambapo kwa upande wa mavuno mbegu chotara zimethibitika kutoa mazao mengi ambapo kwa ekari moja mkulima mmoja ameweza kuvuna gunia 16 ambapo kwa mbegu za zamani angeweza kuvuna gunia 3 mpaka tano.

Mutaburukwa amesema “Mara baada ya kuvunwa kwa alizeti hiyo AMDT pia imefanya majaribio ya kusindika mbegu hizo ambapo kilogram ishirini za mbegu chotara zimetoa mafuta lita sita ambapo mbegu za zamani zimetoa lita tano kwa kilo hizo hizo, huku mashudu yakipatikana kilogram 14 kwa mbegu chotara tofauti na kilogram 13 za mbegu za zamani.

Ameongeza kuwa Sifa ya mbegu hizo chotara ni kutoa mazao mengi, kutumia maji kwa ufanisi, zinastawi katika udongo wa aina zote, na pia hazikai shambani mda mrefu kabla ya kuvunwa ambapo hutumia siku 84 mpaka kuvuna tofauti na siku 97 kwa mbegu za zamani.

Naye Mwakilishi wa Meneja wa Faida Mali Mary Daniel amesema majaribio ya mbegu chotara yalianza mwenzi wa nne na yalihusisha halmashauri nne ambazo ni Mkalama, iramba, ikungi na Singida, ambapo mbegu ziliyotumika katika kufanya majaribio ya usindikaji zililimwa Kijiji cha ihanja wilaya ya ikungi.

Mary amesema wakulima waliofika kushuhudia majaribio ni 25 na wasindikaji 12 kutoka katika wilaya ya singida na ikungi ambao kwa pamoja wameazimia kutumia mbegu ya chotara na kuwaelimisha wakulima wenzao faida ya mbegu hizo.

Ameongeza kuwa makampuni mawili ya SDC na BYTRADE wamejiandaa kusambaza mbegu chotara kwa wakulima wa mkoa wa Singida huku akiwahakikishia wakulima kuwa wasambazaji hao wataleta mbegu kwa wakati ili wapande ndani ya msimu wa kilimo.

No comments:

Post a Comment