Wednesday, February 22, 2017

TIMU YA MAJI NA USAFI WA MAZINGIRA MANYONI YATAKIWA KUTEKELEZA MAJUKUMU YAKE IPASAVYO.

Timu ya maji ya Mkoa wakiwa katika moja ya chanzo cha maji cha kijiji cha Mbwasa kilichopo Halmashauri ya wilaya ya Manyoni, mradi huo una visima viatau vyenye uwezo wa kutoa jumla ya lita 90,000 kwa saa.

Katibu wa Timu ya maji na usafi wa Mazingira ya Mkoa Mhandisi Lydia Joseph ambaye pia ni Mhandisi wa maji Mkoa akipata maelezo ya moja ya chanzo cha maji cha kijiji cha Mbwasa kilichopo Halmashauri ya wilaya ya Manyoni, mradi huo una visima viatau vyenye uwezo wa kutoa jumla ya lita 90,000 kwa saa.
 
Timu ya Maji na usafi wa mazingira ya Wilaya ya Manyoni imetakiwa kutekeleza majukumu yao ipasavyo ikiwa ni pamoja na kusimamia uundwaji na ufuatiliaji wa jumuiya za watumia maji ili ziweze kutunza na kuendeleza miradi yote ya maji wilayani humo.
 
Rai hiyo imetolewa na Katibu wa Timu ya Maji na usafi wa mazingira ya Mkoa Mhandisi Lydia Joseph wakati akizungumza na timu hiyo ya wilaya katika kikao cha ufuatiliaji wa masuala ya maji na usafi wa mazingira huku timu hiyo ikionekana kutotekeleza majukumu yao ipasavyo.

Mhandisi Lydia amesema timu hiyo inapaswa kushiriki kikamilifu katika kutekeleza mpango wa kitaifa wa usafi wa mazingira, kufuatiliaji ujenzi wa vyoo shuleni na kuhakikisha kampeni za usafi zinatekelezwa.

Ameongeza kuwa shule zote za Msingi 69 za Manyoni zinatakiwa kuanzisha klabu za usafi wa mazingira shuleni huku timu ya maji na usafi wa mazingira ya wilaya inapaswa kufuatilia uhai wake kwakuwa imebainika kuwa shule zenye klabu hizo ambazo ziko hai zimepunguza magonjwa yanayoambukiza kama kipindupindu pamoja na kuwa na mazingira mazuri.

Aidha timu hiyo imeshauri shule zote ambazo hazina maji kama mateni au mabomba zihakikishe vibuyu chirizi vinafanya kazi na wanafunzi waweze kunawa vizuri mara baada ya kutumia choo iliwajikinge na magonjwa kama minyoo na kipindupindu.

Kwa upande wa wajumbe wa timu ya maji na usafi wa mazingira wameahidi kutekeleza majukumu yao ipasavyo huku mwenyekiti wa timu ya maji na usafi wa mazingiza ambaye ni Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manyoni Charles Fussi amesema atasimamia vema masuala yote ya maji na usafi wa mazingira katika halmasahuri yake.
Katibu wa Timu ya maji na usafi wa mazingira wa Wilaya ya Manyoni akitoa maelezo ya chanzo cha maji cha Kijiji Mbwasa Wilayani humo.

Chanzo cha maji cha Kijiji Mbwasa Wilayani Manyoni chenye uwezo wa kutoa lita 15,000 kwa saaa.

No comments:

Post a Comment