Monday, November 28, 2016

WANANCHI CHANGIENI MAENDELEO-DC MANYONI.

Viongozi wa Vijiji kwa kushirikiana na Wananchi pamoja na wadau wa maendeleo, wametakiwa kujijengea tabia ya kuchangia shughuli za maendeleo katika maeneo yao.
 
Rai hiyo ilitolewa jana na Mkuu wa Wilaya ya Manyoni, Mh. Geoffrey Idelphonce Mwambe alipokuwa akizungumza katika Mkutano na WanaKijiji wa Kata ya Maweni ambapo alivitembelea Vijiji vya Ngaiti, Mvumi na Maweni akiwa katika ziara ya kujitambulisha kwa Wananchi na kuhamasisha Wananchi kuchangia shughuli za maendeleo katika Kata hiyo.

"Nawapongeza sana  Wananchi wa Kata hii kwa juhudi mnazofanya kuchangia shughuli za maendeleo hasa katika Sekta ya elimu, kwani mmejitahidi kuchangishana na  kufanikiwa kujenga jengo la madarasa mawili ya shule mpya ya msingi Ighose kwenye kijiji cha Ngaiti na nyumba ya walimu ambazo zimefikia katika hatua ya kupauliwa, na hii itasaidia kupunguza adha ya walimu kuishi mbali na maeneo ya shule na hivyo kuongeza morali wa kufundisha hivyo kuongeza ufaulu wa wanafunzi, hivyo basi, kwa kuonesha juhudi hizi, Ofisi ya Mkurugenzi ni muda Muafaka sasa kuwaunga mkono Wanakijiji hawa kuwasaidia kumalizia kupaua majengo haya, ili yaanze kutumika mapema mwakani shule zitakapofunguliwa" Alisema Mwambe.

Nae Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni, Bw. Charles 
E. Fussi akizungumza katika mkutano huo amewataka Watendaji wa Kata na Vijiji, wazazi,  Wenyeviti wa bodi za Shule na kamati za Shule kuwa mfano kwa kuwa mstari wa mbele kuchangia shughuli za maendeleo hasa elimu, katika kupambana na adui ujinga ili kizazi kijacho kiwe na maendeleo stahiki.

Diwani wa Kata hiyo ya Maweni Mh. Abdul Mwengwa amemshukuru Mkuu wa Wilaya kwa kufanya ziara katika Kata yake kwani imeamsha ari ya Wananchi kushiriki na kuchangia shughuli za maendeleo hasa ikizingatiwa sasa wako katika kuhamasisha Wananchi kuchangia ujenzi wa Zahanati yao ya Maweni na kutumia fursa hiyo kuwaomba wadau mbalimbali wa maendeleo kuwasaidia misaada ya hali na mali kukamilisha ujenzi wa Zahanati hiyo ili waondokane na adha wanayoipata sasa ya kukosa huduma za afya.

Katika hatua nyingine, Mkuu huyo wa Wilaya amewapongeza Wananchi wa Kata ya Chikuyu kwa kufanikisha ujenzi wa shule ya msingi Chilejeho, iliyopo kata ya Chikuyu ambayo inahitaji bati 25 na mifuko 50 ya saruji kukamilika, ili watoto waanze kuyatumia madarasa hayo ifikapo Januari mwakani. 

Mkuu wa wilaya alipita kijijini Chilejeho Kata ya Chikuyu, akiwa njiani kutoka kwenye ziara ya siku nzima aliyoifanya kwenye Kata ya Maweni, ambapo alitumia fursa hiyo kuwaasa wazazi kuacha kulichukulia suala la elimu kimzaha wakati Serikali ya Awamu ya tano imedhamiria kutoa elimu bure kuanzia chekechea hadi Sekondari.

No comments:

Post a Comment