Sunday, September 18, 2016

MWENGE WA UHURU WAPOKELEWA MKOANI SINGIDA NA MAMIA YA WANANCHI.




Katibu Tawala Mkoa wa Singida Dokta Angelina M. Lutambi akiupokea mwenge wa uhuru kutoka Katibu Tawala Mkoa Dodoma Rehema S. Madenge.

Mkoa wa Singida umepokea mwenge wa uhuru mapema asubuhi kutoka mkoani Dodoma ili uweze kukimbizwa katika halmashauri zote saba, uzindue, utembelee na utaweka mawe ya msingi katika miradi mbalimbali ya maendeleo.

Akiupokea mwenge huo kutoka kwa Katibu Tawala Mkoa wa Dodoma Bi. Rehema S. Madenge katika Kijiji cha Lusilile Kata ya Kintinku Wilaya ya Manyoni, Katibu Tawala Mkoa wa Singida Dkt. Angelina M. Lutambi amesema jumla ya miradi 61 yenye thamani ya shilingi bilioni 14 itazinduliwa, itatembelewa na kuwekewa mawe ya msingi.

Dkt. Lutambi ameongeza kuwa miradi hiyo imejikita katika sekta za ufugaji, mazingira, maji, afya, elimu, barabara, utawala bora, kilimo, kshirika, biashara, ardhi pamoja na programu za mapambano dhidi ya dawa za kulevya, malaria, rushwa na ukimwi.

Amesema wananchi na viongozi kwa pamoja wako tayari kuukimbiza mwenge wa uhuru mkoani Singida, kuulinda kuuenzi na kudumisha upendo amani na mshikamano wa Taifa letu ulioasisiwa na baba wa Taifa Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere kwa mara ya awali juu ya kilele cha Mlima Kilimanjaro Disemba 9, 1961.

Mara baada ya kuupokea mwenge huo, Katibu Tawala Mkoa wa Singida Dokta Lutambia alimkabidhi Mkuu wa Wilaya ya Manyoni Geofrey Mwambe ili aanze kuumbiza katika halmashauri yake, utembelee, uzindue na kuweka mawe ya msingi katika miradi mbalimbali ya maendeleo.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Manyoni Geofrey Mwambe amesema Mwenge huo unatarajiwa kuzindua  miradi saba yenye thamani ya shilingi milioni 831,719,569.

Mwambe ameongeza kuwa miradi itakayozinduliwa ni pamoja na uzinduzi wa programu ya ufuatiliaji na kuteketeza mbu, kufungua mradi wa ujenzi wa vyumba viwili vya madarasa na matundu nane ya vyoo na ukarabati wa vyumba viwili vya madarasa.

Miradi mingine ni ufunguzi wa daraja la Makutupora, kuzindua klabu ya wapinga rushwa, kuzindua mradi wa ujenzi wa kituo cha maarifa ya kupambana na UKIMWI, kuzindua mradi wa vijana wa kufyatua matofali, na kuzindua klabu ya kupambana na dawa za kulevya.

Mbio za Mwenge wa uhuru kwa Mwaka 2016 zimebeba kauli mbiu ya "Vijana ni nguvu kazi ya Taifa, Washirikishwe na kuwezeshwa" ambapo hata hivyo kila Halamashauri nchini zimeelekezwa kutenga asilimia 5% ya mapato yake ya ndani kwa ajili ya vijana na asilimia 5% nyingine kwa ajili ya kina mama.

Katika kumaliza mizizi wa rushwa, dawa za kulevya, ukimwi na malaria Mwenge wa uhuru umejikita zaidi katika kauli mbiu ya "Timiza wajibu wako kata Mnyororo wa Rushwa" kwenye mapambano dhidi ya Rushwa, Kauli mbiu ni "Tujenge jamii, Maisha na Utu wetu bila dawa za kulevya".

Kwenye Mapambano dhidi ya dawa za kulevya, kauli mbiu ya "Tanzania bila maambukizi mapya, Unyanyapaa na Vifo vitokanavyo na UKIMWI inawezekana"  wakati kwenye Mapambano dhidi ya Malaria kauli mbiu ni " Wekeza katika maisha ya baadae, Tokomeza Malaria".

Kwa mujibu wa ratiba za mbio za Mwenge wa Uhuru za mwaka huu, unakimbizwa katika Halmashauri na Manispaa zipatazo 183 na kilele cha mbio hizo ni Octoba 14, katika Mkoa wa Simiyu.

















Katibu Tawala Mkoa wa Singida Dokta Angelina M. Lutambi akimkabidhi Mkuu wa Wilaya ya Manyoni Mwenge wa uhuru ili uweze kukimbizwa katika halmashauri hiyo.

















Katibu Tawala Mkoa wa Singida Dokta Angelina M. Lutambi akiupokea mwenge wa uhuru kutoka mkimbiza mwenge kitaifa.
















Kiongozi wa mbio za mwenge wa uhuru mwaka 2016 George Jackson Mbijima akisalimiana na Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Miraji Mtaturu mara baada ya kuwasili Mkoani Singida.
Wakazi wa Mkoa wa Singida wakiupokea na kuushangilia mwenge uhuru mara baada ya kuwasili katika kijiji cha Lusilile Kata ya Kitinku, Wilayani Manyioni.

No comments:

Post a Comment