Saturday, June 11, 2016

MKUU WA WILAYA AAGIZA MTUMISHI ALIYESTAAFU AJIBU TUHUMA ZA UBADHIRIFU.


Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Iramba ambaye ni Mkuu wa Wilaya ya Mkalama Christopher Ngubiagai akiagizwa kusimamishwa kazi watumishi wanne na kurudisha mmoja aliyestaafu ili ajibu tuhuma za ubadhirifu. 

Baadhi ya wajumbe wa kamati ya ulinzi na usalama ya wilaya ya Iramba wakimsikiliza kaimu Mkuu wa Wilaya ya Iramba Christopher Ngubiagai.


Na Omary Mtamike- Mkalama

Kwa mara ya kwanza tangu kuanzishwa kwa utaratibu wa kusimamishwa kazi watumishi wenye tuhuma mbalimbali za matumizi mabaya ya fedha au mali ya umma nchini, Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Iramba Mhe: Christopher Ngubiagai leo ameagiza kurejeshwa kwa mtumishi aliyestaafu ili aje ajibu tuhuma zinazomkabili.
Mhe: Ngubiagai ametangaza uamuzi huo mbele ya Waandishi wa habari ofisini kwake Wilayani Iramba kufuatia Udanganyifu na matumizi mabaya ya madaraka katika fedha za halmashauri ya Wilaya hiyo kati ya mwaka 2013 na 2015 ambapo jumla ya shilingi 398,593,675 zimetumika bila idhini ya kamati ya Fedha, Uongozi na Mipango na Baraza la Madiwani kama inavyoelekezwa chini ya kanuni ya 42(3) ya kanuni za kudumu zinazoongoza Halmashauri ya Wilaya ambapo fedha hizo ni za mwaka wa bajeti 2013/2014 na 2014/2015.
Kufuatia ubadhirifu huo, Mhe: Ngubiagai ameagiza mamlaka husika kuwasimamisha kazi na kuwakabidhi kwenye vyombo husika watumishi watano ambapo watatu kati yao walihamishiwa vituo vingine vya kazi, mmoja amestaafu na mwingine bado ni mfanyakazi  wa halmashauri ya Wilaya hiyo.
Watumishi hao ni pamoja na aliyekuwa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya hiyo Bi. Halima Mpita ambaye kwa sasa ni Mkurugenzi wa halmashauri ya Mji Tunduma, aliyekuwa Afisa Utumishi wa Wilaya hiyo Tabia Nzowa ambaye kwa sasa ni Afisa Utumishi wa Wilaya ya Kyela, aliyekuwa Afisa Mipango wa Wilaya Hiyo Stephen Pundile ambaye kwa sasa ni Afisa Mipango wa Wilaya ya Ulanga, Injinia Mstaafu wa Wilaya hiyo L.S.K Rweyemamu na Afisa Maendeleo ya Jamii wa Wilaya hiyo mpaka sasa, Focus Marwa.
“Wale ambao walishahamishiwa vituo vingine vya kazi, taratibu zinafanywa ili waweze kusimamishwa kazi huko na kurejeshwa kuja kujibu tuhuma zao huku wakipisha uchunguzi wa kina utakaofanywa na vyombo husika dhidi yao” Alisema Ngubiagai.
Mhe: Ngubiagai ambaye pia ni Mwenyekiti wa kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya hiyo alimalizia taarifa yake kwa kuwataka Wakuu wa Idara, Viongozi na Watumishi wa halmashauri ya Wilaya hiyo Kutenda na Kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia kanuni na misingi ya maadili ya Viongozi wa umma na kwamba atakayefanya kinyume na hivyo atakuwa amejitafutia matatizo.

No comments:

Post a Comment