Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mhe. Halima Dendego, amewataka wananchi kutumia ardhi kama rasilimali ya kimkakati kwa maendeleo ya kiuchumi na kijamii, akisisitiza umuhimu wa kuitunza na kuitumia kwa tija. Kauli hiyo ameitoa wakati wa hafla ya kukabidhi hati zaidi ya 800 za umiliki wa ardhi kwa wananchi wa Kijiji cha Makunda, Wilaya ya Iramba, ikiwa ni sehemu ya mpango wa Serikali wa kuimarisha usalama wa ardhi na kupunguza migogoro ya umiliki.
Akizungumza katika hafla hiyo iliyofanyika Makunda, Mhe. Dendego amesema Serikali imeendelea kuweka mifumo ya kumuwezesha mwananchi kumiliki ardhi kihalali ili aweze kuitumia kama mtaji wa maendeleo. Ameeleza kuwa umilikishaji wa ardhi unalenga kuwawezesha wananchi kupata mikopo, kuongeza uzalishaji wa kilimo na kuimarisha ustawi wa familia, huku akisisitiza nidhamu ya matumizi sahihi ya ardhi.
“Ninawaomba wananchi, hati hizi ni heshima, ni haki na ni uchumi. Ardhi kila mwaka inaongezeka thamani; ardhi ndio dhahabu tuliyonayo mkononi. Msipate haraka ya kuuza ardhi yenu, itumieni kujijenga kiuchumi na kuboresha maisha ya familia zenu,” amesema Mhe. Dendego, akionya dhidi ya matumizi yasiyo ya maendeleo yanayoweza kuleta migogoro ya kifamilia na kijamii.
Aidha, Mkuu wa Mkoa amesisitiza kuwa Serikali itaendelea kusimamia matumizi bora ya ardhi kwa kushirikiana na viongozi wa vijiji, huku akihimiza wananchi kutumia hati kama dhamana ya mikopo ya maendeleo, kuwekeza katika kilimo cha mazao ya kimkakati ikiwemo alizeti, na kuhakikisha watoto wanapata elimu kwa wakati kama msingi wa maendeleo ya muda mrefu.
Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Mkalama, Mhe. Moses Machali, aliyekuwa Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Iramba, amesema kukabidhiwa kwa hati hizo ni hatua muhimu katika kumuwezesha mwananchi kushiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi. Amewataka wananchi kuzihifadhi hati zao sehemu salama na kuzitumia kuongeza uzalishaji katika kilimo na biashara ndogondogo.
Naye Kamishna Msaidizi wa Ardhi Mkoa wa Singida, Bi. Shamim S. Hoza, amesema Kijiji cha Makunda ni miongoni mwa vijiji 241 vilivyopo kwenye mpango wa matumizi bora ya ardhi katika Mkoa wa Singida. Amesema wanakijiji 899 wamenufaika na zoezi hilo, akibainisha kuwa lengo ni kupunguza migogoro ya ardhi na kuongeza thamani ya ardhi kama rasilimali ya uzalishaji.
Mwenyekiti wa Kijiji cha Makunda, Bw. Yesaya Daudi Seti, amesema umilikishaji wa ardhi utasaidia kuimarisha amani na mshikamano kwa kupunguza migogoro ya mipaka na kumwezesha mwananchi kuwekeza kwa uhakika. Ameishukuru Serikali kwa kuleta mpango huo na kuahidi usimamizi mzuri wa kumbukumbu za ardhi ngazi ya kijiji.
Baadhi ya wananchi waliopokea hati hizo wamesema hatua hiyo imewapa uhakika wa kisheria wa kumiliki ardhi na kuwapa fursa ya kupata mikopo ya maendeleo. Wamesema kupitia umilikishaji huo, wanatarajia kuongeza uzalishaji wa kilimo na kuboresha maisha ya familia zao.
Kwa ujumla, zoezi la kukabidhi hati za ardhi Makunda ni sehemu ya mkakati wa Serikali wa kuhakikisha ardhi inatumika kama nyenzo ya maendeleo, kupunguza migogoro ya umiliki na kuchochea uchumi wa wananchi wa Wilaya ya Iramba na Mkoa wa Singida kwa ujumla.

















































