Thursday, December 18, 2025

RC DENDEGO: "ARDHI NI DHAHABU YA MAENDELEO YA WANANCHI"


Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mhe. Halima Dendego, amewataka wananchi kutumia ardhi kama rasilimali ya kimkakati kwa maendeleo ya kiuchumi na kijamii, akisisitiza umuhimu wa kuitunza na kuitumia kwa tija. Kauli hiyo ameitoa wakati wa hafla ya kukabidhi hati zaidi ya 800 za umiliki wa ardhi kwa wananchi wa Kijiji cha Makunda, Wilaya ya Iramba, ikiwa ni sehemu ya mpango wa Serikali wa kuimarisha usalama wa ardhi na kupunguza migogoro ya umiliki.

Akizungumza katika hafla hiyo iliyofanyika Makunda, Mhe. Dendego amesema Serikali imeendelea kuweka mifumo ya kumuwezesha mwananchi kumiliki ardhi kihalali ili aweze kuitumia kama mtaji wa maendeleo. Ameeleza kuwa umilikishaji wa ardhi unalenga kuwawezesha wananchi kupata mikopo, kuongeza uzalishaji wa kilimo na kuimarisha ustawi wa familia, huku akisisitiza nidhamu ya matumizi sahihi ya ardhi.

“Ninawaomba wananchi, hati hizi ni heshima, ni haki na ni uchumi. Ardhi kila mwaka inaongezeka thamani; ardhi ndio dhahabu tuliyonayo mkononi. Msipate haraka ya kuuza ardhi yenu, itumieni kujijenga kiuchumi na kuboresha maisha ya familia zenu,” amesema Mhe. Dendego, akionya dhidi ya matumizi yasiyo ya maendeleo yanayoweza kuleta migogoro ya kifamilia na kijamii.

Aidha, Mkuu wa Mkoa amesisitiza kuwa Serikali itaendelea kusimamia matumizi bora ya ardhi kwa kushirikiana na viongozi wa vijiji, huku akihimiza wananchi kutumia hati kama dhamana ya mikopo ya maendeleo, kuwekeza katika kilimo cha mazao ya kimkakati ikiwemo alizeti, na kuhakikisha watoto wanapata elimu kwa wakati kama msingi wa maendeleo ya muda mrefu.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Mkalama, Mhe. Moses Machali, aliyekuwa Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Iramba, amesema kukabidhiwa kwa hati hizo ni hatua muhimu katika kumuwezesha mwananchi kushiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi. Amewataka wananchi kuzihifadhi hati zao sehemu salama na kuzitumia kuongeza uzalishaji katika kilimo na biashara ndogondogo.

Naye Kamishna Msaidizi wa Ardhi Mkoa wa Singida, Bi. Shamim S. Hoza, amesema Kijiji cha Makunda ni miongoni mwa vijiji 241 vilivyopo kwenye mpango wa matumizi bora ya ardhi katika Mkoa wa Singida. Amesema wanakijiji 899 wamenufaika na zoezi hilo, akibainisha kuwa lengo ni kupunguza migogoro ya ardhi na kuongeza thamani ya ardhi kama rasilimali ya uzalishaji.

Mwenyekiti wa Kijiji cha Makunda, Bw. Yesaya Daudi Seti, amesema umilikishaji wa ardhi utasaidia kuimarisha amani na mshikamano kwa kupunguza migogoro ya mipaka na kumwezesha mwananchi kuwekeza kwa uhakika. Ameishukuru Serikali kwa kuleta mpango huo na kuahidi usimamizi mzuri wa kumbukumbu za ardhi ngazi ya kijiji.

Baadhi ya wananchi waliopokea hati hizo wamesema hatua hiyo imewapa uhakika wa kisheria wa kumiliki ardhi na kuwapa fursa ya kupata mikopo ya maendeleo. Wamesema kupitia umilikishaji huo, wanatarajia kuongeza uzalishaji wa kilimo na kuboresha maisha ya familia zao.

Kwa ujumla, zoezi la kukabidhi hati za ardhi Makunda ni sehemu ya mkakati wa Serikali wa kuhakikisha ardhi inatumika kama nyenzo ya maendeleo, kupunguza migogoro ya umiliki na kuchochea uchumi wa wananchi wa Wilaya ya Iramba na Mkoa wa Singida kwa ujumla.



Wednesday, December 17, 2025

"MTEJA NI MFALME” — DKT. FATUMA MGANGA

 

Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida, Dkt. Fatuma Mganga, amewataka wahudumu wa afya mkoani Singida kuzingatia maadili, utu na kuwajali wananchi wanapotoa huduma za afya, akisisitiza kuwa mteja ndiye mhimili mkuu wa mafanikio ya utekelezaji wa Bima ya Afya kwa Wote. Ameyasema hayo wakati wa ufunguzi wa kikao kazi cha kujadili utekelezaji wa Bima ya Afya kwa Wote kilichofanyika katika Ukumbi wa Chuo cha Uhasibu Tanzania (TIA) mkoani Singida.

Akizungumza katika kikao hicho kilichowakutanisha waganga wafawidhi wa vituo vya afya mkoa wa Singida, Dkt. Mganga amesema Serikali inaanza utekelezaji wa bima hiyo kwa majaribio kwa makundi maalum, hivyo ni muhimu wahudumu wa afya kuwahudumia wananchi kwa weledi ili kila mmoja anufaike na mpango huo. Amesema huduma duni au lugha isiyofaa inaweza kuwakatisha tamaa wananchi na kudhoofisha lengo la Serikali la kuhakikisha huduma za afya zinapatikana kwa wote.

Dkt. Mganga amewataka pia wasimamizi wa huduma za afya kufanya marekebisho na kuboresha utoaji wa huduma katika vituo vya afya ili wananchi wasijutie kujiunga na mfuko wa bima ya afya, hususan kwa makundi maalum ambayo Serikali itayalipia gharama. Amesisitiza kuwa mazingira ya vituo vya afya yanapaswa kuboreshwa ili mwananchi anapofika ajisikie kuthaminiwa na kupata huduma stahiki.

Aidha, amezitaka taasisi za afya kuhakikisha zinalipa madeni yanayodaiwa na Bohari ya Dawa (MSD) kwa wakati, ili kuwezesha upatikanaji wa dawa, vifaa tiba na huduma muhimu zinazokidhi mahitaji ya wananchi. Amesema upatikanaji wa dawa na vifaa ni msingi wa utoaji huduma bora na mafanikio ya bima ya afya kwa wote.

Kwa upande wake, Mganga Mkuu wa Mkoa wa Singida amewataka wahudumu wa afya kuvaa mavazi rasmi yanayotambulika ili kuongeza uaminifu kwa wagonjwa na kuimarisha taswira ya sekta ya afya. Ameongeza kuwa matumizi ya lugha nzuri na yenye staha kwa wagonjwa ni msingi muhimu wa kudumisha uhusiano mzuri kati ya wahudumu wa afya na wananchi.

Kwa niaba ya waganga wafawidhi wote wa mkoa wa Singida, viongozi wa vituo vya afya wameahidi kutekeleza maagizo yaliyotolewa na Katibu Tawala wa Mkoa kwa kuboresha huduma za afya, kuongeza uwajibikaji na kuhakikisha vituo vinaingiza mapato yatakayosaidia kuendeleza huduma. Wamesema dhamira yao ni kuufanya Mkoa wa Singida kuwa mfano wa utoaji huduma bora za afya nchini Tanzania.

Kikao kazi hicho pia kimewakutanisha wadau mbalimbali wa sekta ya afya, wakiwemo wawakilishi wa NHIF, TIRA, MSD na taasisi nyingine, ambao waliwasilisha mada na maelezo kuhusu mwelekeo wa utekelezaji wa Bima ya Afya kwa Wote, hatua inayotarajiwa kuboresha upatikanaji na ubora wa huduma za afya kwa wananchi wote.



Friday, December 05, 2025

MIFUMO YA KIDIGITALI KUWAFUNGULIA MILANGO WAJASIRIAMALI



Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mhe. Halima Dendego, amezindua mafunzo ya kujenga uwezo kwa wajasiriamali kuhusu matumizi ya GS1 Barcodes na QR Codes, akisisitiza kuwa mifumo hiyo ya kidijitali ndiyo njia ya kuwafungulia wajasiriamali milango ya masoko ya kitaifa na kimataifa. Mafunzo hayo yamefanyika chini ya kauli mbiu “GS1 Barcodes: Kiungo chako kwa wauzaji rasmi”, yakilenga kuwajengea wajasiriamali uelewa wa mifumo ya utambulisho wa bidhaa inayotambulika duniani kote.

Semina hiyo imewezeshwa na GS1 Tanzania kwa ushirikiano na taasisi mbalimbali za serikali ikiwemo TRA, BRELA na wadau wengine, ambao wameeleza kwa kina namna wajasiriamali wanaweza kupata barcode na QR code kisheria, hatua zinazowaepusha na ulaghai na kuwalinda dhidi ya matumizi mabaya ya bidhaa zao na makampuni mengine. Aidha, hatua hii ya kidijitali inatarajiwa kuongeza thamani ya bidhaa za Singida na kuziwezesha kupenya kwenye masoko makubwa duniani.

Akizungumza wakati wa ufunguzi, Mhe. Dendego amewataka wajasiriamali wa Singida kuchangamkia fursa hii ya kimkakati, akibainisha kuwa Mkoa wa Singida una bidhaa nyingi zenye ubora wa juu lakini bado hazijapata nafasi ya kutamba kimataifa kutokana na kukosa utambulisho wa kidijitali. “Kundi hili la wajasiriamali ni injini ya uchumi wa Singida. Sisi tuna bidhaa nzuri sana, lakini bila mifumo ya kimataifa kama barcode hatutaifika dunia. Soko la kimataifa linaendeshwa kidijitali, na kama hatuko huko, basi hatutapenya,” amesema.


Ameongeza kuwa Singida ni kitovu cha nchi na hivyo ni mahali sahihi kufunguliwa kwa ofisi ya pili ya GS1 Tanzania. “Ikiwa mtapanga kufungua ofisi mpya nchini, basi Singida ndiyo mahali pake. Tupo katikati ya Tanzania, wajasiriamali watapata huduma kwa urahisi, na hilo litakuwa chachu ya maendeleo makubwa,” amesema.

Mkuu wa Mkoa pia amesisitiza umuhimu wa kulinda amani ili biashara ziendelee kustawi. “Amani ikitoweka, biashara hazipo. Tunaishukuru serikali kwa kutengeneza mazingira bora ya biashara huru. Basi nasi tuitumie fursa hii kutangaza Singida duniani,” amesisitiza.

Kwa upande wake, Katibu Tawala Msaidizi Sehemu ya Rasilimali Watu, Bw. Pancras Stephen, amesema mafunzo hayo yamekuja wakati sahihi, hasa kutokana na ukweli kwamba hata watumishi wa umma wengi wanajihusisha na ujasiriamali. Amesema, “Ujasiriamali wa sasa uko kwenye mifumo ya kidijitali. Tunawaomba mjenge uthubutu na kutumia maarifa haya kupiga hatua katika familia, jamii na taifa.”

Aidha Katibu Tawala Msaidizi – Biashara na Uwekezaji, Bi. Donatila Vedasto, amewataka wajasiriamali kuwa mabalozi wa Singida kupitia bidhaa zao. “Baada ya mafunzo, kila mmoja achukue hatua. Singida inazalisha bidhaa bora sana, lakini bila barcode hatuwezi kufika soko la kimataifa,” amesema.

GS1 Tanzania, kupitia wakufunzi wake, wameahidi kuendelea kutoa mafunzo katika wilaya zote za Singida. Wamesema wajasiriamali wengi wamekuwa wakikosa nafasi ya kuuza kimataifa kwa sababu hawana elimu ya barcode. “Mafunzo haya yatafanya kila mjasiriamali awe na hamu ya kufika soko la kimataifa. Tutafika kila Halmashauri kuhakikisha hakuna anayebaki nyuma,”.

Nao Wajasiriamali walioshiriki semina hiyo wametoa shuhuda wakisema matumizi ya barcode yamewasaidia kuaminika katika supermarkets na malls, hatua iliyoimarisha mauzo na kuwapa nafasi ya kutambulika rasmi na serikali. Wameshukuru serikali kwa kuweka miundombinu ya kidijitali na kuwawezesha kufikia masoko makubwa nje ya nchi.

Hatua hii ya kidijitali imeelezwa kuwa mwanzo wa mageuzi makubwa ya biashara Singida, huku serikali na wadau wakiahidi kuendelea kuweka mazingira rafiki kwa ukuaji wa uchumi wa wajasiriamali.












Saturday, November 29, 2025

WAHITIMU WAHIMIZWA KUJITUNZA NA KUJILINDA WATAKAPOREJEA MAJUMBANI


Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mhe. Halima Dendego, amewaasa vijana wahitimu wa Chuo cha Ufundi na Marekebisho kwa Watu Wenye Ulemavu (Saba Saba) kujitunza na kufuata maadili watakaporejea mitaani baada ya kumaliza masomo yao, akisisitiza kuwa ujana ni rasilimali isiyorudi na ukiupoteza huathiri maisha ya baadaye.

Akizungumza wakati wa mahafali ya chuo hicho, Mhe. Dendego aliwataka vijana kuepuka matumizi ya dawa za kulevya na ngono zembe, akiwakumbusha msemo wa “Kula nanasi kwataka nafasi”, akimaanisha umuhimu wa kusubiri muda muafaka kabla ya kuingia katika mahusiano ili kuepuka mimba za utotoni na magonjwa ya zinaa.

Aidha, aliwaelekeza wakurugenzi, maafisa ustawi na maendeleo ya jamii kuhakikisha vijana wanaunganishwa katika vikundi na kupewa mitaji ili kuwawezesha kuanzisha shughuli za uzalishaji mali badala ya kubaki mitaani bila ajira. Alitoa wito kwa waajiri kuacha kuwaona vijana kama dhaifu, badala yake wawapatie ushirikiano na fursa za kazi.

Mhe. Dendego pia aliwasisitiza vijana kuepuka uharibifu wa rasilimali za taifa kama njia ya kutafuta suluhu ya changamoto zao, bali kuzitumia kwa manufaa yao. Aliwahimiza wahitimu kuwasilisha mawazo ya miradi yao ili kupata mikopo ya asilimia 10 inayotolewa na Halmashauri kwa makundi maalumu, hatua itakayowawezesha kuanzisha biashara na kukuza uchumi wao.


Kwa upande wake, Muuguzi Mkuu wa Mkoa wa Singida, Bi. Yasinta Alute, aliyemwakilisha Mganga Mkuu wa Mkoa, alisema kupungua kwa changamoto za afya ya akili miongoni mwa vijana kunatarajiwa kutokana na kuongezeka kwa uelewa na elimu pamoja na fursa za ajira zitokanazo na ujuzi wanaoupata vyuoni. Alisema kipato kitakachotokana na ujuzi huo kitawasaidia vijana kupata utulivu wa fikra na kupunguza msongo wa mawazo.

Akizungumza kwa niaba ya Afisa Elimu wa Mkoa, Bi. Sarah Mkumbo ambaye ni Afiaa elimu ya watu wazima,aliwahakikishia wanafunzi wenye mahitaji maalumu kuwa serikali inaendelea kuboresha mazingira rafiki ya kujifunzia, ikiwemo miundombinu wezeshi ili kuwarahisishia elimu. Aliwaomba kuwa mabalozi kwa vijana wengine wenye ulemavu ili wajitokeze kujiunga na mafunzo ya ufundi.

Naye Mkuu wa Chuo hicho, Bi. Fatuma Malenga, alisema chuo kimepata mafanikio makubwa kupitia programu ya wanagenzi ambayo imeongeza mwamko kwa vijana kujifunza fani za ufundi. Hata hivyo alitaja changamoto zinazokikabili chuo hicho kuwa ni pamoja na kuibiwa kwa uzio wa chuo, ukosefu wa ukumbi wa mihadhara na baadhi ya wanafunzi kushindwa kuhudumiwa ipasavyo kutokana na hali duni ya wazazi wao.






Friday, November 28, 2025

MUAROBAINI UFAULU SHULE YA MSINGI WAPATIKANA,RAS SINGIDA ATOA MIKAKATI.


 Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida Daktari Fatuma Mganga ametoa wito kwa walimu wa shule za msingi kuongeza ubunifu katika ufundishaji ili kuinua kiwango cha ufaulu wa wanafunzi wa darasa la saba.

Akiwa katika ziara ya kukagua miradi ya maendeleo katika Shule ya Msingi Sophia,leo Novemba 28,2025 amesema mbinu madhubuti za ufundishaji ndizo zitakazowezesha wanafunzi kuwa na uelewa mpana na maandalizi bora ya mitihani yao. Ameeleza kuwa walimu wanapaswa kuwahimiza wanafunzi kufanya mazoezi mengi ya masomo, jambo litakalowaongezea uwezo na kuondoa hofu ya mitihani.

Akiendelea kuzungumza, Katibu Tawala Dkt.Mganga amesisitiza umuhimu wa walimu kuhakikisha wanafunzi wanakuwa nadhifu na wenye usafi muda wote. Amesema suala la usafi ni sehemu ya malezi na maandalizi ya mwanafunzi kujiandaa na hatua inayofuata ya elimu. Kadhalika, amewataka wanafunzi kuheshimu muda wa kufika shuleni na kuwatii walimu wao, sambamba na kuhakikisha mazingira ya shule na madarasa yanabaki kuwa safi ili kuweka msingi wa nidhamu na utendaji bora.

Afisa Elimu wa Mkoa wa Singida akapata nafasi ya kuzungumza na wanafunzi hao na kuwataka kuongeza bidii katika masomo yao. Ameahidi kuanzisha mbinu shirikishi na rafiki kwa walimu ambazo zinalenga kuongeza ufaulu kwa wanafunzi wa darasa la saba kuanzia mwaka ujao. Aidha, amesema kuwa mitihani ya mazoezi ya kila mwezi itaanza kutolewa kuanzia Januari, na wanafunzi watakaofanya vizuri watazawadiwa ili kuongeza ari ya kujifunza na ushindani chanya miongoni mwao.


Kwa upande wa wanafunzi, Lucas Mwagoko ameonesha kujawa na hamasa na kuahidi kusoma kwa bidii ili kufaulu kwa kiwango cha juu katika mtihani wao wa taifa wa darasa la saba mwaka 2026. Amesema hotuba na maagizo yaliyotolewa yamewapa motisha ya kufanya kazi kwa bidii na kujiandaa mapema.

Ziara hiyo pia ilihusisha ukaguzi wa miradi ya maendeleo inayoendelezwa na Serikali Kuu katika Shule ya Msingi Sophia, ikiwemo ujenzi wa madarasa matatu, nyumba ya mwalimu na matundu 38 ya vyoo. Utekelezaji wa miradi hiyo unaelezwa kuwa sehemu ya mpango wa Serikali kuboresha miundombinu ya elimu na kuweka mazingira bora ya ufundishaji na ujifunzaji.

Katika matokeo ya darasa la saba kitaifa mwaka 2025 Mkoa wa Singida umepata wastani wa 81.

Kupitia maboresho hayo, Serikali inaendelea kuwaandaa wanafunzi wanaotarajiwa kujiunga na kidato cha kwanza kwa kuwajengea mazingira salama na rafiki ya kujifunzia. Hii inajumuisha ujenzi wa madarasa mapya, mabweni na maktaba, upatikanaji wa vitabu vya kutosha, vifaa vya maabara, TEHAMA, na kuongeza nguvu kazi ya walimu. Hatua hizo zinahakikisha kuwa wanafunzi wanapofika sekondari wanakutana na mazingira yaliyoboreshwa yanayowawezesha kusoma kwa ufanisi na kufikia malengo yao ya kitaaluma.