Wednesday, March 26, 2025

TUENDELEE KUTENDA MEMA HATA BAADA RAMADHANI

 

               Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe.Halima Dendego amewaasa waumini wa dini ya kiislamu kuhakikisha matendo mema yanakuwa sehemu ya maisha yao na wala sio kutenda mema katika kipindi cha mfungo wa Ramadhani pekee.

                   Ameyasema hayo wakati wa kupata ifutari pamoja na waumini wa dini ya kiislamu iliyoandaliwa Katika kuunga mkono mfungo wa mwezi mtukufu wa ramadhani katika Kiwanda cha kuchambua pamba cha Bioustain mkoani Singida, wakifuturisha waumini wa Kiislamu na wananchi wengine waliojumuika pamoja.

          Akizungumza katika iftari hiyo, Mkuu wa Mkoa wa Singida Mheshimiwa Halima Dendego amepongeza uongozi wa kiwanda hicho kwa kuweza kufuturisha, huku akisema kitendo hicho kinampendeza mwenyezi Mungu kwa kuonyesha ishara ya mshikamano na upendo kwa Waislamu na jamii kwa ujumla.

             "Sadaka kama hizi ni jambo la heri, mwenyezi Mungu anawapenda wanaojitolea kwa ajili ya wenzao wengi, na bila shaka, huu ni mfano wa kuigwa," alisema Mheshimiwa Dendego.

Katika hatua nyingine, Mhe.Dendego, amewakumbusha Wananchi kutumia vizuri sherehe za mei mosi, zitakazofanyika kitaifa mwaka huu mkoani Singida akisema sherehe hizo ni fursa adhimu kwa wananchi wa mkoa wa Singida, kwani kwa muda wa wiki mbili mkoa utapokea zaidi ya wageni 6,000, ambao watahitaji huduma mbalimbali, ikiwemo chakula na malazi.

                "Hii ni nafasi nzuri kwa wafanyabiashara na watoa huduma mbalimbali kuweza kujiandaa ipasavyo, ili wanufaike kiuchumi...tuitumie vyema fursa hii kwa kuongeza kipato chetu, na kuboresha maisha ya familia zetu," alisisitiza Dendego.

Naye Sheikh wa Mkoa wa Singida, Issah Nassoro, ametumia fursa hiyo kutoa wito kwa waumini wa Kiislamu na jamii kwa ujumla, kuendelea na mwenendo mzuri hata baada ya Ramadhani.

                "Tusirejee kwenye dhuluma na maovu, naomba wafanyabiashara wazingatie njia halali za kutafuta riziki, huku nao watumishi wa umma watosheke na mishahara yao, badala ya kujihusisha na vitendo vya rushwa, amesema.

.                                       Aidha, Sheikh Nassoro ametangaza kuwa Swala ya Idd El-Fitr kwa mkoa wa Singida mwaka huu itafanyika kwenye viwanja vya Bombadia, huku akiwataka waumini wa Kiislamu kujitokeza kwa wingi kusali pamoja akisema ni vyema waumini waendelee kudumisha mshikamano na kujihusisha na ibada, hata baada ya Ramadhani, huku akitoa mfano wa namna mwezi mtukufu unavyoleta mabadiliko chanya katika jamii.

            Matendo mema, uadilifu na mshikamano ni nguzo muhimu si kwa mwezi wa Ramadhani pekee, bali kwa maisha ya kila siku, na ni jukumu la kila mmoja kuhakikisha thamani ya mfungo wa mwezi mtukufu, inakuwa sehemu ya maisha ya kudumu.



VIDEO:







MAAFISA ELIMU KATA WAPATIWA MAFUNZO YA USIMAMIZI WA SHULE NA UJAZAJI TAKWIMU .

 


Maafisa elimu Kata 136 mkoani Singida wamepatiwa mafunzo maalumu kuhusu Usimamizi Saidizi katika maeneo yao ya uongozi wa shule na ujazaji wa takwimu katika Mfumo wa "School Information System" (SIS). Mafunzo hayo yamefanyika Machi 24,2025 katika ukumbi wa Halmashauri ya Wilaya ya Iramba, yakihudhuriwa na viongozi wa elimu ngazi ya Mkoa, Wathibiti Ubora wa shule Mkoa na Wilaya, Wakuu wa Divisheni Elimu ya Awali na Msingi, yakiongozwa na wawezeshaji kutoka ADEM na TAMISEMI.

Akifungua mafunzo kwa niaba ya Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida Dkt. Elipidius Baganda amepongeza juhudi za maafisa elimu Kata katika kutekeleza majukumu yao, akibainisha kuimarika kwa ufaulu wa wanafunzi katika mitihani ya taifa. Aidha, ameutambua mchango wa Mradi wa Shule Bora katika kuboresha ufundishaji wa walimu na ujifunzaji kwa wanafunzi wote wakiwemo wenye mahitaji maalumu kutokana na weledi wa walimu kupitia mafunzo mbalimbali yanayofanyika katika halmashauri zote za mkoa wa Singida. Na amewasihi wadau wa elimu kuendelea kushirikiana na Serikali katika kuboresha elimu kwa ngazi zote, ikiwemo elimu ya watu wazima na elimu nje ya mfumo rasmi.

       "Mafunzo haya yanalenga kuwaongezea ujuzi maafisaelimu Kata ili waweze kusimamia ipasavyo shughuli za elimu katika maeneo yao, hususani katika kuhakikisha ujazaji sahihi wa taarifa za shule kwenye Mfumo wa SIS." alisema Dkt. Baganda

Pia, Amesisitiza umuhimu wa kuongeza ufaulu wa wanafunzi, kukamilisha miundombinu kwa ubora, kutoa taarifa za maendeleo kila wiki, huku akiwakumbusha watumishi wa umma kutojihusisha na siasa.

"Hakikisheni ufaulu wa wanafunzi unaongezeka, miundombinu ya shule inakamilika kwa wakati na kwa ubora unaotakiwa, taarifa za maendeleo zinatolewa kila mwisho wa wiki. Pia, ni muhimu mtumishi wa umma kuepuka kujihusisha na masuala ya kisiasa, ili kuepusha mgongano wa maslahi." alisema Dkt. Baganda

Shule Bora ni mradi wa Serikali unoatekelezwa kupitia Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia na TAMISEMI, ukisimamiwa na Cambridge Education kama mshauri na kufadhiliwa na Serikali ya Uingereza kupitia FCDO.














Thursday, March 20, 2025

WATUMISHI WAAGIZWA KUWA NA MAADILI BORA KATIKA KAZI

 


Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe.Halima Dendego amesisitiza maadili katika maeneo ya kazi kwa kutoa maagizo ya utendaji Bora wa kazi kwa watumishi pamoja na usimamizi bora wa viongozi wa idara na vitengo mbalimbali.

Ameyasema hayo leo hii wakati akifungua kikao cha kujadili mapitio ya bajeti kwa mwaka 2025/26 kilichofanyika katika Ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Singida.

           Amesisitiza Viongozi wa idara,vitengo na sekta mbalimbali kuhakikisha wanawajibika kwa kuwaongoza vema waliopo chini yao kwa kutoa maamuzi sahihi na kuhakikisha wanafanya kazi katika mazingira yenye furaha na mazingira bora ya utendaji kazi ambayo yatawafanya kufanya kazi kwa kujiamini na kwa weledi ambayo yataleta matokeo changa katika utendaji wa kazi.

"Tutimize wajibu kwa kuzingatia haki,wajibu na sheria, changamoto katika Shemu za kazi zipo,tuwe watulivu na wasikivu kwani sisi ni vioo katika jamii hivyo maisha yetu yawaguse wale tunaowaongoza".amesema Mhe.Dendego

              Pia amesisitiza nidhamu ya watumishi katika kazi kwa kuwa kioo kwa jamii na wale tunaowaongoza kwa kuhakikisha wanavaa mavazi yanayostahili kazini,aina za misuko,viatu na mengine mengi.

Akizungumzia kuhusu suala la nidhamu kwa watumishi kazini,Katibu Tawala wa Mkoa Daktari Fatuma Mganga amesisitiza uwajibikaji kwa watumishi kwa kuhakikisha wanakuwa mstari wa mbele katika utekelezaji wa majukumu mbalimbali huku akikumbusha watumishi kubwa na haiba ya kuwahi kazini ili kutekeleza majukumu yao kwa wakati muafaka.

               Katibu Tawala msaidizi sehemu ya Rasilimali watu Bw.Pancras Stephen amezungumzia suala la ukiukwaji wa maadili kwa watumishi kama sifa mbaya kwa watumishi huku akisema mikakati imekwishawekwa kwa ajili ya kuhakikisha tabia zisizofaa kimaadili kwa watumishi zinazooneshwa ili kurejea katika mstari ulio sahihi.

     Kikao hicho kimehudhuriwa na viongozi mbali mbali kutoka katika vyama vya wafanyakazi ngazi za halmashauri,wilaya na ngazi ya Mkoa.















VIDEO:



        """""KARIBU SINGIDA:MEI MOSI 2025"""""

Wednesday, March 19, 2025

MADAKTARI BINGWA WATOA MAFUNZO ELIMU YA MAMA KWA MTOTO.


 Madaktari bingwa wa mpango wa Mama Samia kutoka mikoa mbalimbali wametoa mafunzo ya kuboresha utoaji huduma kwa mama na watoto wachanga kwa watumishi wa afya wa Hospitali ya Wilaya ya Singida na vituo vya afya jirani.

Lengo la mafunzo haya ni kuwajengea uwezo watoa huduma, hasa katika sekta ya afya ya mama na mtoto, ili kupunguza vifo vya wajawazito na watoto wachanga. Mafunzo hayo ya siku tatu yalifanyika kuanzia tarehe 17 hadi 19 Machi, 2025, katika ukumbi wa Hospitali ya Wilaya ya Singida.

          Watumishi wa afya walioshiriki wameeleza shukrani zao kwa madaktari hao kwa ujuzi waliopata na wameahidi kutumia maarifa hayo kuboresha utoaji huduma na kuongeza weledi katika kazi zao za kila siku.

            Mpango huu ni moja ya juhudi za serikali za kuimarisha huduma za afya nchini na kuhakikisha mama na mtoto wanapata huduma bora na salama



Sunday, March 16, 2025

"MNARA WA MAWASILIANO KUCHOCHEA MAENDELEO IRAMBA":DKT MGANGA



Kijiji cha Mbelekesye kilichopo Wilayani Iramba Mkoani Singida kimeendelea kunufaika na mawasiliano ya uhakika yenye tija katika nyanja za kiuchumi kutokana na uwepo wa mnara wa mawasiliano kijijini hapo

Hayo yameshuhudiwa leo baada ya Kamati ya Bunge kufika kukagua ujenzi na utendaji kazi wa mnara huo uliojengwa na mtandao wa Yas kwa ruzuku ya Tshs 124,235,000 kwa usimamizi wa Mfuko wa Mawasiliano kwa Umma UCSAF.

Akizungumza katika hafla hiyo,Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida Dkt.Fatuma Mganga amesema uwepo wa mnara huo utarahisisha mawasiliano baina ya watu,lakini pia huduma za kifedha zitakua rahisi sana kwani wananchi watakua huru kufanya miamala ya kifedha katika benki tofauti bila kutembea umbali mrefu kufika kwa mawakala au katika mashine za ATM.

Kadhalika,ameomba ushirikiano kutoka kwa wananchi kwa kuhakikisha mnara huo unatunzwa vizuri katika kuhakikisha unadumu ili kutoa huduma nzuri kwa jamii.

Naye Mbunge wa Busega,Simiyu ametoa pongezi kwa wananchi wa Mbelekyese kwa utayari wao wa kutoa eneo la kuujenga mnara huo ambao utakwenda kuwa nguzo kuu katika nyanja ya mawasiliano.Pia ameshauri uwepo wa mitandao mingine katika mnara huo mmoja kwa lengo la kukidhi mahitaji ya wananchi ambao wanatumia mtandao zaidi ya mmoja 

Hamady Nkungu,mkazi wa Kijiji cha Mbelekesye wilayani Iramba ameonyesha kufurahia kuzinduliwa kwa mnara huo ambao amesema unakwenda kuchochea maendeleo ya wananchi kiuchumi ambapo hapo awali yalikua ya taabu na kuzorotesha maendeleo yao ikiwemo kukosa masoko ya bidhaa zao mbalimbali za kilimo na ufugaji.

"Kwa sasa imekua rahisi kupata wateja wa mazao na mifugo yetu kwasababu mawasiliano ya uhakika yanatoweka karibu sana na wanunuzi tofauti na hapo nyuma ambapo tulitumia muda mwingi kutafuta wateja na kutumia muda kidogo katika shughuli za uzalishaji mali"amesema Nkungu.

Kuzinduliwa kwa mnara huu ni utekelezaji wa kujenga minara mingine 758 hapa nchini ambayo itawasaidia wananchi kuingia katika mfumo wa uchumi wa kidigitali.Lengo likiwa ni kupata taarifa muhimu za kukuza uchumi kama vile taarifa za pembejeo za kilimo na mifugo na mengineyo.




VIDEO: