Tuesday, September 02, 2025

UWEKEZAJI KATIKA ELIMU KUTOA FURSA KWA WOTE

 

Posted on: September 1st, 2025

Mkuu wa Wilaya ya Iramba, Mhe. Suleiman Yusuph Mwenda, amefunga kongamano la maadhimisho ya Juma la Elimu ya Watu Wazima na Elimu Nje ya Mfumo Rasmi yaliyofanyika katika Halmashauri ya Wilaya ya Iramba, akimwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mhe. Halima Dendego, na kusisitiza kuwa elimu ndiyo msingi wa kuondoa ujinga na kuimarisha maendeleo ya Taifa. 

          Akihutubia wadau wa elimu, Wanafunzi na wananchi waliohudhuria maadhimisho hayo, Mhe. Mwenda amesema wiki ya elimu ya watu wazima inalenga kuhamasisha kila mwanadamu atambue haki yake ya kupata elimu. 

“Elimu ya watu wazima ni muhimu sana kwa kupata ujuzi unaomwezesha mtu kujiajiri. Pia inamuondoa mtu kwenye ujinga na kumwezesha kuendana na zama za sasa za kidigitali kupitia sayansi na teknolojia,” amesema.

Aidha ameongeza kuwa Mkoa wa Singida umeendelea kupiga hatua kubwa kielimu kuanzia shule za awali hadi vyuo vikuu, na matokeo yake ni ufaulu mkubwa wa vijana. “Vijana wetu wanafaulu kwa asilimia 98, jambo linaloonesha mabadiliko makubwa ukilinganisha na miaka iliyopita. Hii inatupa matumaini makubwa ya mustakabali wa elimu,” ameongeza.

Mhe. Mwenda amesisitiza kuwa serikali inaendelea kuwekeza kwenye miundombinu na vifaa vya kufundishia ili kuhakikisha fursa za elimu zinapatikana kwa wote.

 “Shule mpya zimejengwa na zinaendelea kujengwa ili vijana wetu wasome hadi kidato cha tano na sita na hatimaye vyuo vikuu,” amesema.

Akisoma ripoti ya Hali ya elimu ya Watu wazima katika Mkoa wa Singida, Afisa Elimu ya Watu Wazima Mkoa wa Singida, Bi. Sarah Mkumbo, ameeleza kuwa mkoa wa Singida una jumla ya shule za msingi 691 na sekondari 194, zote zikitumika pia kama vituo vya elimu ya watu wazima na elimu nje ya mfumo rasmi. Amesema pia Singida inayo vyuo mbalimbali vikiwemo vya walimu, afya, maendeleo ya jamii, VETA na Chuo Kikuu Huria.

Bi. Mkumbo ameongeza kuwa mkoa unatekeleza programu kadhaa ikiwemo MUKEJA yenye zaidi ya wanafunzi 111,000 wanaojifunza masomo yenye manufaa, pamoja na wengine zaidi ya 136,000 wanaoshiriki kwenye elimu ya uzalishaji mali. “Programu hizi zimekuwa kichocheo cha kupunguza ujinga na kuongeza maarifa ya vitendo miongoni mwa wananchi,” amesema.

           Naye Mkuu wa Wilaya ya Mkalama, Mhe. Moses Machali, amesema elimu ni kila kitu katika msingi wa maendeleo ya jamii. “Shule nyingi zinahitaji kuja kujifunza Singida kwa sababu elimu yetu inajikita kwenye vitendo. Hii imekuwa msaada mkubwa katika kuibadilisha jamii nzima,” amesema.

Mhe. Machali ameongeza kuwa kila jamii iliyofanikiwa duniani imepiga hatua kupitia elimu. “Vijana hawa wanapaswa kuwezeshwa ili waweze kuibadilisha jamii. Mambo yote duniani—iwe ni afya, biashara au teknolojia—yanahitaji elimu ili kufanikishwa kwa ufanisi,” amesema.

Maadhimisho hayo yamehitimishwa kwa msisitizo kwamba elimu ya watu wazima na elimu nje ya mfumo rasmi si chaguo bali ni hitaji la lazima katika zama za kidigitali, ili kujenga taifa linalojitegemea, lenye mshikamano na maendeleo endelevu.Tukio hilo limebeba kaulimbiu isemayo “Kukuza kisomo katika zama za kidigitali kwa maendeleo endelevu ya taifa letu.”


Kutazama yaliyojiri katika maadhimisho hayo fungua kiungo kilichopo hapo chini:





Friday, August 22, 2025

SINGIDA YAAZIMIA KUBORESHA HALI YA LISHE KWA WATOTO NA WATU WAZIMA.

Posted on: August 22nd, 2025

Mkoa wa Singida umeazimia kuboresha hali ya utoaji na matumizi ya lishe bora katika mkoa huo kwa makundi yote ya watoto na watu wazima ili kuhakikisha wanakua na afya njema itakayowaweka mbali na magonjwa yatokanayo na lishe duni ikiwemo ukondefu, udumavu, upungufu wa damu na uzito pungufu.

Hayo yamejiri katika kikao cha utekelezaji wa hali ya lishe katika ngazi ya Mkoa leo Agosti 22, 2025, kilichowakutanisha Kamati ya Lishe ya Mkoa, Wakurugenzi wa Halmashauri, Waganga Wakuu wa Halmashauri, Maafisa Elimu, Waweka Hazina, Timu ya RHMT ya Mkoa pamoja na wadau mbalimbali wa lishe.

Mganga Mkuu wa Mkoa wa Singida, Dkt. Victorina Ludovick, alisema kuwa kikao hicho ni sehemu ya jitihada endelevu za kuboresha afya na lishe ya wananchi kwa kuhakikisha changamoto zilizopo zinapatiwa suluhu za haraka na zenye ufanisi.

“Kwa sasa bado tuna udumavu , ukondefu kwa watoto chini ya miaka mitano kwa asilimia 2.3, upungufu wa damu, na uzito pungufu kwa asilimia 11.1. Lakini kikao hiki kinatupa nafasi ya kuweka mikakati mipya ya kupunguza changamoto hizi. Tunapopambana vizuri katika ngazi ya mkoa, mchango wetu kitaifa unakuwa mkubwa zaidi,” alisema Dkt. Ludovick.

Aidha alisisitiza kuwa wataalamu wa afya na lishe, kwa kushirikiana na sekta mtambuka, wanapaswa kuja na mbinu bora zaidi za kupunguza matatizo hayo, ili kuhakikisha Singida inakuwa na wananchi wenye afya bora na taifa lenye nguvu kazi imara.

Kwa upande wake, Afisa Lishe wa Mkoa, Bi. Tedda Sinde, amewasilisha taarifa ya utekelezaji wa masuala ya lishe akibainisha kuwa hatua mbalimbali zimechukuliwa ikiwemo usimamizi shirikishi katika sekta za afya, ustawi wa jamii na lishe, uhakiki wa ubora wa takwimu, utoaji wa elimu ya lishe katika vituo vya afya, jamii, redioni na mashuleni.

“Tumeendelea pia kufanya tathmini ya mara kwa mara ya hali ya lishe na elimu ya magonjwa yasiyoambukiza sambamba na kuhamasisha jamii kulima na kutunza bustani za mboga majumbani. Haya yote yanaimarisha lishe kwa wananchi,” alisema Bi. Sinde.

Kwa upande wa sekta ya elimu, Bi. Sarah Mkumbo amewasilisha hali ya uvunaji wa chakula mashuleni ambapo ameeleza kuwa kiwango cha upandaji na uvunaji kimepungua mwaka huu kutokana na mabadiliko ya hali ya hewa.

“Hata hivyo mashule yetu bado yanapanda mazao ya chakula chenye lishe kwa watoto ikiwemo mahindi, mtama, mpunga, alizeti, karanga, maharage na kunde. Tunapambana kuhakikisha kila mwanafunzi anapata chakula chenye virutubishi,” alisema Bi. Mkumbo.

Mwenyekiti wa kikao hicho Bw.Pancras Stephen akiongoza kikao hicho kwa niaba ya Katibu Tawala wa Mkoa,Ka yake,  ameaziagiza Halmashauri zote za Mkoa wa Singida kuhakikisha fedha zote zilizotengwa kwa ajili ya lishe zinawasilishwa na kutumika kwa malengo yaliyopangwa.

“Ni lazima tuwe na uwajibikaji mkubwa. Fedha za lishe zisicheleweshwe wala kutumika kinyume na makusudi yake. Vilevile idara mtambuka zinapaswa kutoa mrejesho wa utekelezaji wa shughuli za lishe mara kwa mara, huku tukiimarisha ushirikiano na wadau na kuongeza mashine za kuongeza virutubishi kila kata,” amesema Bw. Pancras.

Kikao hicho kimehitimishwa kwa makubaliano kuwa kila sekta na kila mtaalamu atashirikiana kikamilifu ili kuimarisha hali ya lishe mkoani Singida. Lengo ni kuhakikisha watoto wanakua na afya bora, watu wazima wanabaki na nguvu kazi imara, na Singida inachangia vyema katika kupunguza changamoto za lishe kitaifa.

Friday, August 15, 2025

SINGIDA YAJA NA MIPANGO KABAMBE YA KUFIKIA VIWANGO VYA JUU VYA USAFI WA MAZINGIRA

 

Posted on: August 15th, 2025

 Viongozi na wataalamu wa afya wametakiwa  kusimamia kwa umakini utekelezaji wa Mradi Endelevu wa Usambazaji Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (SRWSSP) ili kufanikisha lengo la kuwa na mkoa wenye viwango vya juu vya usafi ifikapo mwaka 2025.

Akifungua kikao cha tathmini ya utekelezaji wa mradi huo leo (15 Agosti 2025),   Katibu Tawala Msaidizi wa Sehemu ya Mipango na Uratibu Mkoa wa Singida Ndg.Nesphory Bwana, akizungumza kwa niaba ya Katibu Tawala wa Mkoa, amesema mpango huo, unaotekelezwa kwa mfumo wa Malipo kwa Ufanisi (Result Based Financing), umewezesha mkoa kupokea zaidi ya shilingi bilioni 6.42 katika kipindi cha miaka mitano, na kuboresha miundombinu ya maji na usafi katika vituo 154 vya kutolea huduma za afya.

Kwa upande wake, Mganga Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt.Victorina Ludovick amesema miradi ya usafi wa mazingira na uboreshaji wa miundombinu ya maji imekuwa chanzo muhimu cha mapato kwa mkoa, na kufafanua kuwa mwaka 2021 ulipokelewa mtaji wa kuanzia wa shilingi milioni 262.87, lakini hadi kufikia mwaka wa fedha 2024/2025 zaidi ya shilingi bilioni 6 zimepokelewa. Fedha hizo zimetumika kujenga vyoo, vichomea taka, kuboresha maeneo ya huduma za mama na mtoto na miundombinu ya maji safi na salama.

Aidha, amesema kikao hicho pia kinajadili ushirikiano na Shirika la Viwango Tanzania (TBS) kwa ukaguzi na usajili wa maeneo ya biashara, ambapo asilimia 40 ya mapato yatabaki halmashauri na asilimia 10 kuingia mkoani, hatua ambayo itaimarisha mapato.

Naye Afisa Afya Mkoa wa Singida, Bw. Mgeta Sebastian, ameeleza kuwa huduma za WASH zimeboreshwa na kuwafikia makundi maalumu, hususan wenye ulemavu na afya ya mama na mtoto huku Idadi ya kaya zenye vyoo bora ikiongezeka kutoka asilimia 60 mwaka 2020 hadi 75.9 mwaka 2025, kadhalika vifaa vya kunawia mikono vikiongezeka kutoka asilimia 16 hadi 46 katika kipindi hicho. Amesema pia uelewa wa wananchi kuhusu usafi wa mazingira na ujenzi wa vyoo jumuishi umeimarika.

Bw. Mgeta ameongeza kuwa mkoa umefanikisha ufuatiliaji wa karibu wa utekelezaji wa miradi, kuhamasisha jamii kutumia vyoo bora, na kuimarisha ushirikiano wa kisiasa, kijamii na kidini katika kutekeleza sheria za mazingira.

Kikao hicho kimeazimia kuendelea kusimamia kwa ufanisi miradi ya maji na usafi wa mazingira, ili Singida ibaki kinara wa afya bora na mazingira safi nchini.



Kwa undani zaidi wa yaliyojiri katika kikao hicho tafadhali fatilia kiungo kifuatacho kuona Video ya kikao hicho

https://youtu.be/AuKmMZfwCgU

                                    👇👇👇👇👇



Thursday, August 14, 2025

WAZAZI WASIOPELEKA WATOTO WENYE MAHITAJI MAALUM SHULENI KUCHUKULIWA HATUA


Posted on: August 14th, 2025

Viongozi wa elimu na wadau mkoani Singida wametoa wito wa mshikamano na ushirikiano katika kusimamia fedha na miradi ya elimu ili kuhakikisha ubora wa shule na mazingira salama ya kujifunzia kwa wanafunzi wote sambamba na kuhakikisha watoto wote wanapelekwa shuleni kupata elimu bila kuwaacha nyuma wale wenye mahitaji maalum wakiwemo walemavu wa viungo ili kuhakikisha makundi yote yanapata elimu iliyo bora.

Hayo yamejiri katika kikao cha tathimini ya mradi wa Shule bora kwa mwaka 2024/25 Mkoani Singida katika ukumbi wa Mkuu wa Mkoa wa Singida leo Agosti 14,2025 ambacho kimehusisha Wakurugenzi wa Halmashauri,Wadhibiti ubora wa Shule,Maafisa elimu,wahasibu na Maafisa mipango kutoka Halmashauri za Mkoa wa Singida.

Akizungumza kwenye kikao cha tathmini ya utekelezaji wa programu ya Shule Bora, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni Bi.Anastazia Tutuba amewataka wakurugenzi wenzake kushirikiana na wataalamu wa elimu, wahasibu, na wadhibiti ubora ili kuhakikisha fedha zinazotolewa zinapangiwa mpango kazi wenye vipaumbele na kutekelezwa kwa wakati. Amesisitiza kuwa kila mtoto ana haki ya kupata elimu bora katika mazingira salama, na kwamba mpango wa Shule Bora hauwezi kubagua jinsia wala changamoto za kimaumbile.

Kwa upande wake, Afisa Elimu wa Mkoa wa Singida Dkt.Elpidius Baganda ametoa wito kwa wazazi wenye watoto wenye mahitaji maalumu kuhakikisha wanawapeleka shule ili wapate haki yao ya msingi ya elimu. Amesema kuwa kuwatenga au kuwafungia ndani watoto hao ni kosa la jinai na hatua za kisheria zitachukuliwa kwa watakaokiuka. Amesisitiza pia kuwa shule zimeboreshwa ili kuwa rafiki kwa watoto wenye mahitaji maalumu kwa kujengwa madarasa yanayokidhi mahitaji yao.

Aidha, alieleza kuwa vipaumbele vya Mpango wa Maendeleo ya Sekta ya Elimu chini ya utekelezaji wa Shule Bora ni pamoja na kuimarisha uandikishaji wa wanafunzi, kuongeza idadi ya wanafunzi wanaomaliza elimu ya msingi, kuimarisha ufundishaji wa Kusoma, Kuandika na Kuhesabu (KKK), kuongeza idadi ya wanafunzi wanaoingia sekondari, kuimarisha mbinu za ufundishaji na ujifunzaji, pamoja na kusaidia serikali kufikia vigezo vya EPforR II ili kupata fedha za motisha kutoka kwa wahisani wa maendeleo.

Awali akiwasilisha mada katika kikao hicho,mratibu wa Shule Bora Mkoa wa Singida Bw. Fredrick Ndahani amewasilisha baadhi ya  matokeo ya muda mfupi yaliyokusudiwa na mradi wa Shule Bora ikiwa  ni pamoja na wazazi na jamii kushiriki kikamilifu katika kuboresha ujifunzaji, walimu kusaidiwa kufundisha elimu bora, jumuishi na katika mazingira salama, shule kusimamiwa kwa uwajibikaji kwa wadau, tawala za mikoa na mitaa kusimamia shule vizuri, pamoja na taasisi za kitaifa kusimamia utoaji wa elimu bora kwa ufanisi.

Bw. Ndahani alihitimisha kwa kusisitiza kuwa utekelezaji wa Shule Bora mkoani Singida unaendelea kuleta mabadiliko chanya katika elimu, huku akiwataka wadau wote kuendelea kushirikiana ili kuhakikisha malengo yaliyowekwa yanafikiwa.

Nae Mdau wa elimu, Bi. Zipora Semwanza, amesema matarajio baada ya kikao hicho ni kufanya maboresho pale ambapo hapakuwa na ufanisi na kuimarisha maeneo yanayoendelea vizuri huku akiahidi kuwa kutakuwa na maboresho ya miundombinu ya elimu, kuimarishwa kwa stadi za Kusoma, Kuandika na Kuhesabu (KKK), pamoja na mafunzo kwa walimu ili kuongeza ujuzi, ubunifu na mshikamano wa kiutendaji.

 Shule Bora ni programu ya kitaifa inayolenga kuboresha ubora wa elimu, ushirikishwaji, na kuhakikisha mazingira salama ya ujifunzaji kwa wanafunzi wa shule za msingi za serikali nchini Tanzania. Programu hii inafadhiliwa na Shirika la Misaada la Uingereza (UKAID) kwa idhini ya Serikali ya Uingereza na inatekelezwa katika mikoa tisa ya Tanzania Bara ikiwemo Mkoa wa Singida kwa kushirikiana na mashirika ya Cambridge Education, ADD International, International Rescue Committee (IRC) na Plan International.Kadhalika mradi huo pia unaunga mkono utekelezaji wa mpango wa Elimu wa Kitaifa wa Lipa Kulingana na Matokeo (EPforR II).


Sunday, July 06, 2025

AJALI YA MOTO SOKO KUU SINGIDA YATAFUTIWA UFUMBUZI


Posted on: July 6th, 2025

Serikali ya Mkoa wa Singida imeunda kamati ya kuchunguza na kufanya tathimini tukio la kuungua moto soko kuu la mjini Singida ili wafanyabishara waliopata janga hilo iangalie namna ya kuwasaidia.

Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mhe.Halima Dendego, akizungumza na wananchi na wafanyabishara leo baada ya kutembelea kukagua eneo la tukio, amesema kamati hiyo ifanya kazi hiyo kwa muda wa siku saba kuanzia leo.

Amesema kamati aliyoiunda itawajumuisha wafanyakazi wa serikali, Kamati ya Usalama ya Mkoa na mameneja wa benki zote zilizopo mkoani hapa na kwamba baada ya tathimini hiyo kazi ya kurejesha miundombinu ya soko hilo itaanza mara moja.

“Ndani ya kamati hizi kutakuwa na wataalam wa fedha,wataalamu wa biashara na wataalam wa afya pia kwani wenzetu wamepata mshtuko lazima tuwajue mmoja mmoja wapo wapi ili warejee katika hali salama na kazi hiyo inaanza leo na tumewapa siku saba wamalize kazi hiyo na sisi tutaanza kusafisha eneo hilo kwa ajili ya kujenga kwa haraka,” amesema.

“Naomba nitoe salamu za pole kutoka kwa Mhe.Rais Samia Suluhu Hassan,  tulimpa taarifa za awali na amenituma tukae mimi na kamati yangu kuweka kambi hapa ili tumjulishe uharibifu uliotokea hapa, lakini pia Waziri wa Tamisemi, Mhe.Mohamed Mchengerwa anawapa pole,” alisema Dendego.

Aidha,Dendego amekipongeza Kiwanda cha Pamba cha Biousastain na kiwanda cha Meru ambavyo vimeweza kusaidia kutoa vitendea kazi katika kufanikisha kazi ya kuzima moto.

Naye Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Singida, Martha Mlata, amewapa pole wafanyabiashara kwa janga hilo na kuwaahidi kwamba ana imani kubwa kuwa Serikali itarejesha miundombinu ya soko hilo ili shughuli za biashara ziendelee kama kawaida.

Kadhalika,Mlata amelipongeza Jeshi la Zimamoto na Ukoaji, Jeshi la Polisi na wananchi kwa jinsi walivyoweza kushirikia katika zoezi la uokoaji ambapo hakukuweza kutokea tukio la kupora mali za waathirika.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Singida, Godwin Gondwe, alisema ulinzi utaendelea kuimarishwa katika soko hilo ili uporaji woowote usiweze kufanyika.

Mwenyekiti wa Soko Kuu la Singida, Hassan Mboroo, alisema moto katika soko hilo ulianza kuwaka  saa 3:40 usiku wa kuamkia leo katika duka la kuuza vifaa vya ujenzi baadaye kuenea katika maduka mengine.

Amesema zoezi la kuuzima lilianza kufanyika muda huo na kufanikiwa kuuzima hapo baadae ambapo jumla ya maduka 15 yameteketea kwa moto zikiwamo bidhaa zilizokuwemo na kusababisha hasara kubwa kwa wafanyabiashara.

Mboroo alisema kufuatia tukio hilo kuna haja kwa serikali kuliboresha soko hilo kwa kuweka katika mpangilio mzuri ili kunapotokea majanga kama haya ya moto magari ya kuzimia moto yaweze kupita kwa urahisi kufanya kazi ya uokozi.

Monday, June 30, 2025

MAAFISA MAENDELEO KIKAANGONI,WAASWA KUJIPIMA KWA MATOKEO NA SIO IDADI YA VIKAO.


Posted on: June 30th, 2025

Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mhe. Halima Dendego, amesema kuwa Maafisa Maendeleo ya Jamii lazima wajipime kwa matokeo wanayoyaleta kwa wananchi na si kwa idadi yao au vikao wanavyohudhuria, akisisitiza kwamba kazi yao kuu ni kuifikia jamii na kuleta mabadiliko chanya.

Akizungumza katika kikao kazi cha Maafisa Maendeleo kutoka wilaya zote za Mkoa wa Singida kilichofanyika katika ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Mhe. Dendego amesema amefurahi kukutana nao kwa sababu ndiyo msingi mkubwa wa mafanikio ya wananchi katika ngazi ya jamii.

“Nimefurahi kukutana nanyi kwa sababu tuna mambo mengi ya kuyajadili ili kuhakikisha tunatekeleza mipango mbalimbali ya serikali na huduma zinawafikia wananchi. Tuhakikishe tunawafikia wananchi na tunawaelimisha, kwani haitakuwa na maana huduma hizi hazitawafikia,” amesema RC Dendego.

Ameeleza kuwa Maafisa Maendeleo wanapaswa kujitathmini kama kweli wanatekeleza wajibu wao ipasavyo na kuleta tija, badala ya kukaa maofisini wakisubiri wananchi wawafuate. “Ukiitwa Afisa Maendeleo, kila eneo linakuhusu. Tupimane kwa malengo yetu ili tulete tija kwa wananchi wetu,” amesisitiza.

Pia,Mkuu wa Mkoa amesema anaifahamu vyema taaluma hiyo kwa kuwa yeye mwenyewe ni mwana sayansi wa jamii, hivyo anajua namna ilivyo na jukumu kubwa katika kubadilisha tabia na ustawi wa wananchi. 

“Sisi tunahusika moja kwa moja na kurekebisha tabia za jamii, tunawajenga raia wema wa taifa hili,” amesema.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa Maafisa Maendeleo kuviunda vikundi, kuvisimamia, kuvilea na kuvifikisha kwenye taasisi za fedha, ili wanawake, vijana na watu wenye ulemavu waweze kupata mikopo na kujikwamua kiuchumi. “Tija sio uwingi wetu, tija ni namna tunavyoipeleka jamii mbele kwa vitendo,” amesema.

Ametumia kikao hicho kuwataka Maafisa Maendeleo waamke na waone kama wanatimiza malengo ya serikali.

 “Tupate ndoto ya kuwatoa wananchi wa Singida hapa walipo, tusibaki kusema hiki ni kikao kazi bila vitendo. Hiki ni kikao cha operation, kama kumponya mgonjwa, tupate suluhisho. Swali kubwa ni: namna gani mnaifikia jamii? Tuache kukaa tu ofisini, tufike field.”

Kadhalika Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida Daktari Fatuma Mganga amesema kuwa kikao hicho pia kina maazimio kadhaa cha kuhakikisha wanakwenda kujitathimini juu ya kwamba ni namna gani wameweza kuwafikia wananch na yapi ni matokeo ya wao kuwepo maeneo hayo ikiwa ni kuhakikisha wananchi wanaishi mazingira bora ikiwemo kuwa na vyoo bora,ukatili dhidi ya wanawake na watoto,mikopo ya wanawake na walemavu,fursa mbalimbali za wananchi kuwekeza,kadhalika dawati la huduma za msaada wa kisheria  ikiwa ni kwa namna gani wanatumia jukwaa hilo kuhakikisha wanashighulikia kero za wananchi na mengineyo mengi.

"Tunalo jukumu kubwa la kuhakikisha kuwa yale ambayo tumekasimiwa na Mhe.Rais,Wakurugenzi na viongozi wengine katika ngazi ya  Wilaya tunayafanyia kazi na yanaleta matokeo ili nasisi tuonekane kuwa tunafanya kazi yenye matokeo chanya katika jamii"amesema Daktari Mganga.

Kadhalika amesema kuwa moja ya azimio la kikao hicho ni kuhakikisha Maafisa hao wanakwenda kushuhulikia suala la marejesho ya fedha zote ambazo vikundi mbali mbali vilikopa ikiwemo mikopo ya asilimia kumi kwa lengo la kuhakikisha inawafikia wengine ambao hawajapata kadhalika kusimamia vema vikundi vilivyopo ili kupiga hatua kubwa zaidi za kiuchumi.

Kauli hizo zimekuja wakati Maafisa Maendeleo wakiwa kwenye mkutano wa pamoja kujadili changamoto zilizopo katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo, ikiwemo mikopo kwa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu, mikataba ya vikundi pamoja na namna ya kuhakikisha wanavifikia vikundi vyote vya jamii kwa usawa.

Ni katika majadiliano yao, Maafisa Maendeleo wamejadili changamoto zinazohusu utekelezaji wa kanuni mbalimbali ikiwemo mikopo kwa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu, pamoja na mikataba ya vikundi vya kukopeshwa ili kuhakikisha malengo ya serikali ya kuwainua kiuchumi makundi haya muhimu yanafanikiwa ipasavyo.

Kikao hicho kimetoa fursa kwa Maafisa Maendeleo kubadilishana uzoefu na kuja na mikakati ya pamoja itakayosaidia kuharakisha maendeleo katika jamii za Mkoa wa Singida.