Monday, October 27, 2025

SERIKALI YAMWAGA MABILIONI UJENZI WA OFISI NA NYUMBA ZA MAKAZI SINGIDA


Sekretarieti ya Mkoa wa Singida imepokea zaidi ya shilingi bilioni tatu kutoka Serikali Kuu kwa ajili ya ujenzi wa majengo mbalimbali ya viongozi wa serikali mkoani humo.

Fedha hizo ni sehemu ya utekelezaji wa mpango wa serikali wa kuboresha miundombinu ya ofisi na makazi ya viongozi katika ngazi za mikoa na wilaya. Kupitia mpango huo, ofisi tatu za wakuu wa wilaya zitajengwa katika Wilaya za Iramba, Manyoni na Singida, ambapo kila moja imetengewa bajeti ya shilingi bilioni moja (1,000,000,000).

Aidha, serikali imetenga kiasi cha takribani shilingi milioni 454 kwa kila nyumba ya makazi ya Wakuu wa Wilaya za Manyoni na Iramba, sambamba na bajeti ya shilingi milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa nyumba ya Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida.

Akizungumza leo Oktoba 27, 2025, wakati wa ziara yake katika Wilaya ya Iramba, Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe.Halima Dendego amefika katika eneo lililopendekezwa kwa ajili ya ujenzi wa ofisi mpya ya Mkuu wa Wilaya ya Iramba na nyumba ya makazi ya Mkuu wa Wilaya hiyo, ambapo alijadiliana na viongozi wa eneo hilo kuhusu maandalizi ya utekelezaji wa mradi huo.

Kupatikana kwa majengo hayo mapya kutaboresha kwa kiasi kikubwa mazingira ya kazi na utendaji wa viongozi wa serikali, kuongeza ufanisi wa utoaji wa huduma kwa wananchi, pamoja na kuimarisha usimamizi wa shughuli za maendeleo katika wilaya na mkoa kwa ujumla. 

Vilevile, ujenzi huo utachochea fursa za ajira za muda mfupi kwa wananchi wa maeneo husika na kuchangia ukuaji wa uchumi wa Mkoa wa Singida.









 


Saturday, October 25, 2025

RC DENDEGO ATETA NA WATUMISHI USHIRIKI UCHAGUZI


 Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mhe. Halima Dendego, ameongoza kikao na wakuu wa taasisi pamoja na watumishi wote wa Serikali wa Mkoa wa Singida leo, Oktoba 25, 2025, chenye lengo la kuwahamasisha kushiriki kikamilifu katika Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Jumatano ijayo, Oktoba 29, 2025.


Akizungumza katika kikao hicho, Mhe. Dendego amewakumbusha watumishi na wakuu wa taasisi kuzingatia maelekezo ya kisera yaliyotolewa kuelekea Uchaguzi Mkuu, 

Akiwakumbusha maelekezo yake ya kisera kuelekea Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025, Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mhe. Halima Dendego, amewataka watumishi wote wa umma kuhakikisha wanakuwa na vitambulisho halali vya wapigakura na kufika mapema katika vituo vyao vya kupigia kura kabla ya muda wa kufungwa. Amesisitiza kuwa watumishi wanapaswa kuwa mfano wa utii kwa sheria kwa kufuata kikamilifu maelekezo ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) pamoja na viongozi wa usalama, ili kuhakikisha mchakato mzima wa uchaguzi unafanyika kwa amani, utulivu na uwazi.

Aidha, amekemea vikali vitendo vinavyoweza kuashiria upendeleo wa kisiasa, akiwataka watumishi kuepuka kuvaa mavazi au kubeba nembo za vyama vya siasa, pamoja na kujiepusha na matamshi, maandiko au mienendo yoyote inayoweza kuchochea chuki, vurugu au ubaguzi katika jamii. Ameongeza kuwa watumishi wanapaswa kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa weledi na uwajibikaji, bila kuegemea upande wowote wa kisiasa, ili kudumisha heshima ya utumishi wa umma na kuonesha mfano bora wa uadilifu katika kipindi chote cha uchaguzi.

Kwa upande wake, Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida, Dkt. Fatuma Mganga, amewataka watumishi wote kujiepusha na matumizi mabaya ya mitandao ya kijamii, hasa katika kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi, na badala yake kutumia mitandao hiyo kwa elimu, uhamasishaji chanya na kuimarisha umoja wa kitaifa.

Aidha, Dkt. Mganga ametoa wito wa kujilinda binafsi na kulinda familia, kwa kuepuka kutembea katika maeneo hatarishi hasa nyakati za usiku, na kufanya majukumu yao mapema ili kuepuka usumbufu wowote siku za uchaguzi.

Nao wakuu wa taasisi mbalimbali mkoani Singida, wameahidi kujitokeza mapema ifikapo saa moja asubuhi siku ya uchaguzi, kuhakikisha wanatekeleza haki yao ya kikatiba ya kupiga kura, na kuwa mfano bora kwa watumishi na wananchi kwa ujumla.








Monday, October 20, 2025

SOKO JIPYA LA VITUNGUU,WAFANYABIASHARA KUPINDUA MEZA KIUCHUMI


 Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mhe. Halima Dendego, ameagiza viongozi wa Halmashauri kutoa ushirikiano wa kutosha kwa wakandarasi wanaotekeleza ujenzi wa Soko jipya la Vitunguu lililopo Kititimo, ili kuhakikisha mradi huo unakamilika kwa wakati uliopangwa na kwa viwango vya juu.

Akizungumza katika kikao kilichofanyika eneo jipya la ujenzi wa soko hilo, Mhe. Dendego amesema Serikali ina dhamira njema ya kuboresha mazingira ya wafanyabiashara na kuhakikisha Singida inakuwa kitovu cha biashara ya vitunguu nchini.

“Singida tunakwenda kipindua meza, tunakwenda kuweka historia ya kipekee kwa mradi huu mkubwa na wa kipekee. Hii ni moja ya sababu ya kwenda kuuweka mkoa wa Singida kwenye ramani ya kuwa Jiji la Singida. Na hili linawezekana kwa utekelezaji wa miradi hii mikubwa. Tutegemee mwezi Septemba 2026 kukata keki ya mafanikio baada ya kukamilika kwa mradi huu wa TACTIC,” amesema Mhe. Dendego.

Kadhalika, amemtaka mkandarasi kuhakikisha maeneo muhimu yanazingatiwa katika ujenzi wa soko hilo ikiwemo maeneo ya zahanati, michezo, mapumziko, kumbi za mikutano pamoja na maeneo ya sekta binafsi kuwekeza katika huduma za kifedha. Amesisitiza pia kazi kufanyika kwa ubora ili gharama kubwa za ujenzi ziendane na thamani ya fedha zilizotolewa na Serikali.

Awali, Mkuu wa Wilaya ya Singida, Mhe. Godwin Gondwe, aliwataka wajumbe wa kikao hicho kufikisha salamu za Serikali kwa wananchi na wafanyabiashara wa Soko la Vitunguu juu ya nia njema ya kuhamishia soko hilo maeneo mapya. Amesema eneo hilo jipya litakuwa rafiki zaidi kwa wafanyabiashara na litakidhi idadi kubwa ya wajasiriamali kuliko soko la sasa, hivyo kuongeza faida maradufu.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Soko la Vitunguu-Misuna, Bw. Iddi Mwanja, amesema wafanyabiashara wamepokea kwa mikono miwili na kwa furaha kubwa mradi wa soko jipya kwa kuwa utawanufaisha kwa kiasi kikubwa sambamba na kufanya kazi zao kwa uhuru katika mazingira bora na rafiki kwa wote.

“Serikali yetu tunaiamini, tuiache ifanye kazi yake. Tutafuata utaratibu tunaopewa kwa sababu ina nia njema kwetu sisi wananchi,” amesema Bw. Mwanja.

Naye Katibu wa Soko la Vitunguu, Bw. Mshujaa Salum Mwacha, amesema hawana hofu kwani viongozi wamekuwa wakiwasikiliza na kuwashirikisha vizuri katika kila hatua ya maandalizi ya mradi huo. Ameongeza kuwa wamefurahia kuona soko jipya limewapa kipaumbele watu wenye mahitaji maalum sambamba na akinamama wanaonyonyesha.

Mkandarasi anayehusika na ujenzi huo ameahidi kuhakikisha ujenzi unakuwa wa viwango vya juu na unakamilika kwa wakati, akisisitiza kuwa wananchi wa Singida wajiandae kupokea soko zuri la kisasa lenye mazingira rafiki kwa kazi zao za kila siku.Amesema kuwa ukubwa wa soko hilo ni mita za mraba 32,547.

Kikao hicho kilihudhuriwa na Mkuu wa Wilaya ya Singida, Mkurugenzi wa Manispaa ya Singida, Katibu Tawala wa Wilaya, Wajumbe wa Soko la Vitunguu, Afisa Mazingira, Afisa Maendeleo ya Jamii, Mtaalam wa Ardhi, wataalam kutoka TARURA, wakandarasi na wadau wengine wa maendeleo.

Mradi huu wa ujenzi wa Soko jipya la Vitunguu unatarajiwa kuleta mageuzi makubwa katika sekta ya biashara mkoani Singida kwa kuboresha mazingira ya wafanyabiashara, kuongeza mapato ya Serikali, kutoa ajira kwa wananchi, pamoja na kuongeza thamani ya zao la vitunguu linalolimwa kwa wingi katika mkoa huo. Soko hilo pia litakuwa na miundombinu rafiki kwa watu wote, likiwa na huduma muhimu kama zahanati, maeneo ya mapumziko, michezo na huduma za kifedha, hivyo kuchochea ukuaji wa uchumi wa Mkoa wa Singida na kuchangia utekelezaji wa mpango wa kuifanya Singida kuwa Jiji la kisasa.





























Saturday, October 18, 2025

WANANCHI WAHAKIKISHIWA USALAMA WAO KUELEKEA UCHAGUZI MKUU