Friday, September 22, 2023

Mwenge wa Uhuru kuzindua miradi ya Bilioni 224 Singida

MKUU wa Mkoa wa Singida, Peter Serukamba amesema Mwenge wa Uhuru ambao umekabidhiwa leo tarehe 22 Septemba, mwaka huu mkoani humo kutokea Tabora, unatarajiwa kutembelea kuzindua pamoja na uwekaji wa mawe ya msingida miradi yenye thamani ya zaidi ya Sh 224 bilioni ambayo imetekelezwa katika kipindi cha kuanzia Julai 2022 hadi Septemba, 2023.

Miradi itahusu sekta ya elimu, afya, maji, nishati, kilimo, uchumi, miradi ya utunzaji wa mazingira na miundombinu.

Serukamba ametoa kauli hiyo leo tarehe 22 Septemba mwaka huu wilayani Iramba mkoani Singida wakati akipokea Mwenge wa Uhuru kutoka kwa Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Balozi Batlida Briani.

Amesema lengo kubwa la kuupokea Mwenge huo ni kufanya uchechemuzi wa miradi pamoja kuhamasisha upendo, amani na ushirikiano.

Akizungumzia sekta ya elimu amesema jumla ya Sh. 34.08 bilioni zimetolewa kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mbalimbali ya miundombinu ya elimu hususani ujenzi wa shule mpya za BOOST na shule mpya za Sekondari kupitia mradi wa SEQUIP pamoja na utoaji wa elimu bila malipo kutoka shule ya msingi hadi kidato cha nne.

Kwa upande wa kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Taifa, Abdalla Shaib Kaim amesema lengo la kukagua miradi hiyo ni kuhakikisha miradi inayotekelezwa inaendana na thamani ya fedha.


 

No comments:

Post a Comment