Sunday, September 29, 2024

RC SINGIDA, Apongeza Wawekezaji wa Ndani Kuimarisha Sekta ya Viwanda vya Mafuta, Pamba na Kuleta Ajira kwa Vijana.

Mkuu wa Mkoa wa Singida, Halima Dendego, amewapongeza wawekezaji wa ndani hasa katika sekta ya viwanda vya mafuta ya kupikia, Mount Meru Mellers LTD, Singida Fresh Oil Mill na kiwanda cha Pamba cha Biosustain vilivyopo mkoani Singida akisema uwepo wa uwekezaji huo unaipunguzia Serikali mzigo wa kuagiza mafuta ya kupikia kutoka nje na kuleta ajira kwa vijana.


RC Dendego, ametoa pongezi hizo Septemba 28, 2024 katika ziara yake ya kutembelea viwanda katika halmashauri ya Manispaa ya Singida ambapo amesema, uwekezaji katika viwanda vya mafuta utasaidia serikali katika kutimiza lengo lake la kuzalisha mafuta ndani ya nchi.

Akizungumzia kiwanda cha Singida Fresh Oil Mill, Dendego amekiri kupokea taarifa ya kuwa asilimia 95 ya ukamilishaji mradi huo tayari umefikiwa na zaidi ya watu 200 wanatarajiwa watapata ajira, hii ni kuunga mkono serikali katika juhudi za kuleta maendeleo katika mkoa wa Singida na taifa kwa ujumla.

Mkurugezi Mkuu wa Kiwanda cha kukamua mafuta cha Singida Fresh Oil Mills Khalid Omary (kulia) akimweleza jambo Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe. Halima Dendego (mwenye kilemba) wakati wa ziara ya kutembelea viwanda katika Manispaa ya Singida. kushoto ni Mkuu wa Wilaya ya Singida Godwin Gondwe.

"Sisi Serikali ya mkoa wa Singida tutahakikisha tunawezesha mazingira mazuri kwa wawekezaji na changamoto zenu tunazishughulikia. Pia nimefurahishwa jinsi wageni wanavyokuja na teknolojia mpya na kuwaachia ujuzi huo utawasaidia vijana kupata ajira". RC Dendego

Aidha, Mkuu huyo wa Mkoa amesema kuwa Mkoa wa Singida ni miongoni mwa wazalishaji wakubwa wa mazao ya kilimo, hususan mbegu za mafuta ya alizeti hivyo ametoa wito kwa wakulima mkoani humo kuzalisha kwa wingi ili kukidhi mahitaji.

Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe. Halima Dendego akizungumza na uongozi wa kiwanda cha Singida Fress Oil Mill (hawapo pichani) mara baada ya kutembelea kiwanda hicho.

Pia RC Dendego,, ameahidi kuwa serikali ya mkoa itahakikisha malighafi zinapatikana ili mafuta yazalishwe kwa wingi huku akiwataka wawekezaji wa viwanda vidogo kuhakikisha wanazalisha mafuta safi na salama kwa matumizi ya binadamu.

Hata hivyo, Dendego amewashukuru wawekezaji hao wa viwanda kwa ushirikiano kwa serikali na jamii kwa kuwa unaleta manufaa makubwa ikiwa ni pamoja na upatikanaji wa maji safi, ujenzi wa shule, na msaada katika kukabiliana na majanga.

Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe. Halima Dendego (wapili kutoka kushoto) akizungumza na Mkurugenzi wa Kiwanda cha kukamua mafuta ya Alizeti Mount Meru Millers kilichopo Singida mjini wakati wa kutembelea kiwanda hicho.

Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe. Halima Dendego akionyesha moja ya bidhaa ya sabuni inayozalishwa na kiwanda cha kukamua mafuta ya alizeti Mount Meru Millers wakati alipotembelea kiwanda hicho. 
kulia ni Mkuu wa Wilaya ya Singida Godwin Gondwe.




Ziara ikiendelea katika kiwanda cha kukamua mafuta ya alizeti SINGIDA FRESH OIL MILL kilichopo Singida Mjini.

Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe. Halima Dendego akipokea maelezo mafupi kutoka kwa viongozi wa kiwanda cha Pamba Biosustain kuhusu mchakato wa uzalishaji wakati alipotembelea katika kiwanda hicho kilichopo Singida Mjini, Septemba 28, 2024.


Muonekano wa magunia ya Pamba ambayo imezalishwa na kiwanda cha biosustain tayari kwa ajili ya kusafirisha.

No comments:

Post a Comment