Monday, September 25, 2023

MIRADI YA HALMASHAURI YA MANISAPAA YA SINGIDA YAMKOSHA KIONGOZI WA MBIO ZA MWENGE KITAIFA 2023

Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa mwaka 2023, Abdalla Shaib Kaim amesema kuwa miradi ya maendeleo iliyokaguliwa na Mbio za Mwenge wa Uhuru mwaka huu katika Halmashauri ya Manispaa ya Singida imetekelezwa kwa viwango vinavyokubalika na kutekelezwa kizalendo.

Kaim ametoa kauli hiyo leo tarehe 25 Septemba, 2023 wakati wa ziara ya ukaguzi, uzinduzi na uwekaji wa jiwe la msingi katika miradi mbalimbali ya maendeleo katika Halmashauri ya Manispaa ya Singida.

Kaim akiweka jiwe la msingi katika Kituo cha Afya Mtipa, amesema kuwa miradi mingi imetekelezwa kwa viwango vinavyokubalika na kuzingatia ubora na thamani ya fedha.

Akizungumzia mradi wa Kituo cha afya cha Mtipa, Kaim amesema kuwa mradi huo umejengwa kwa kiwango na ubora sambamba na uwepo umakini katika nyaraka mbalimbalimbali za manunuzi na utekelezaji wa mradi.

Hata hivyo amewataka Wakandarasi wanaofanikiwa kupata tenda za kujenga miradi mbalimbali ya Serikali wanatakiwa kuwa wazalendo kwa kuhakikisha wanajenga miradi hiyo kwa viwango ubora  unaokubaliwa na Serikali.

Aidha amewataka wakandarasi kuhakikisha wanamaliza miradi yao kwa wakati ili iweze kutumika kwa malengo yaliyokusudiwa na si vinginevyo.

Katika hatua nyingine Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa mwaka 2023 ametembelea na kukagua mradi wa uboreshaji wa huduma wa usafi wa mazingira katika Manispaa ya Singida.

Sambamba na hilo amewataka wananchi wa Singida Mjini kuhakikisha wanatunza mazingira kwa kupanda miti na kuitunza. Aidha amewataka wasimamizi wa miradi hiyo kuhakikisha changamoto zote zilizotolewa maelekezo yanafanyiwa kazi kwa wakati.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Singida Mhandisi Paskas Muragili amesema miradi iliyozinduliwa na Mbio za Mwenge wa Uhuru mwaka huu pamoja na kukaguliwa na kuwekwa jiwe la msingi itatunzwa na kulindwa na ile ambayo haijakamilika itakamilishwa kwa wakati.

Sambamba na hilo Mhandisi Muragili, amesema miradi inayotekelezwa inalenga kuwanufaisha wananchi na kuhakikisha fedha zinazotolewa na Serikali zinatumiwa kwa malengo yaliyokubalika.

Jumla ya sh. Bilioni 3.113 zimetumika kujenga miradi mbalimbali ya maendeleo katika Halmashauri ya Manispaa ya Singida. Katika ujenzi wa miradi hiyo imewashirikisha wananchi, wadau (wahisani) pesa za ndani kwa maana ya vyanzo vya mapato kutoka Halmashauri ya Manispaa ya Singida na fedha kutoka Serikali Kuu.

Kwenye utekelezaji wa miradi hiyo wanachi wamechangia kiasi cha fedha Milioni moja, wahisani Bilioni 1.7, Manispaa shilingi Milioni 511 na Serikali Kuu imechangia kiasi cha Shilingi Milioni 870.4 na kufanya jumla ya sh Bilioni 3.113




No comments:

Post a Comment