Thursday, June 01, 2023

Watakao chelewesha miradi ya maendeleo Singida kukiona - Serukamba

Siku tatu baada ya Katibu Tawala Mkoa wa Singida Dkt. Fatma Mganga kutoa maagizo kwa Mkandarasi anayejenga wodi mbili na nyumba ya kuhifadhia Maiti Wilayani Manyoni ya kuwalipa staahiki zao mafundi na vibarua leo Mkuu wa Mkoa huo, Peter Serukamba naye ametembelea eneo hilo na kumuagiza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manyoni kulipa fedha za Mkandarasi huyo na kuwalipa mafundi pamoja na vibarua ili kazi iweze kukamilika kwa wakati.

RC Serukamba ametoa maagizo hayo baada ya kupewa taarifa na Mhandisi wa Wilaya hiyo, Gabriel Mayaya kwamba, kazi ya ujenzi inachelewa kwa sababu Mkandarasi haonekani eneo la kazi na vibarua  hawajalipwa fedha zao jambo ambalo huchangia kusuasua kwa kazi hiyo ndipo alipotoa maelekezo fedha hizo kukatwa na kuwalipa vibarua na mafundi huku akimtaka Mhandisi huyo kuongeza usimamizi ili kazi ikamilike kwa wakati.

"Huwezi kuacha kuwalipa vibarua halafu utegemee kazi itamalizika, Mhandisi kaa na Mkurungezi chukueni fedha za Mkandarasi lipeni vibarua wake kwa kuwa inafahamika kiasi wanacholipwa kwa kazi walizofanya" Serukamba

Aidha amemuagiza Mhandisi Mayaya kuongeza mafundi wengine kwa kuwa sehemu ya ujenzi iliyobaki ni kubwa na mafundi ni wachache huku muda ukiwa ni mdogo uliobaki.

"Hatuwezi kumsubiri mtu ambaye hata ‘site’ haonekani, fedha zake walipeni hao vibarua na tafuteni mafundi wengine ili kazi ikamilike kwa wakati".

Hata hivyo RC Serukamba amebainisha kwamba mtumishi yeyote atakayeshindwa kusimamia miradi ya maendeleo Mkoani Singida na akasababisha fedha kurudi hazina watakuwa wamehatarisha vibarua vyao.

Hata hivyo akiongea kwa niaba ya Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manyoni, Elias Moleli (Afisa Maendeleo ya Jamii) Wilayani hapo amemuahidi Mkuu wa Mkoa kwamba wataongeza mafundi na watahakikisha kazi inafanyika usiku na mchana na kwa viwango vinavyotakiwa.

Aidha Moleli amesema tayari wamenunua vifaa vyote muhimu vikiwemo mabati nondo na madirisha na mbao kwa ajili kukamilisha kazi hiyo.

MATUKIO KATIKA PICHA WAKATI WA ZIARA







Mkuu wa Mkoa wa Singida Peter Serukamba akisisitiza jambo kwa Mhandisi wa Wilaya ya Manyoni, Gabriel Mayaya mara baada ya kujionea hali ya ujenzi.










No comments:

Post a Comment