Wednesday, May 31, 2023

Singida Press Club yakutana na RAS Singida

Waandishi wa Habari Mkoani Singida wameshauriwa kutangaza fursa zinazopatikana katika Mkoa huo ikiwemo kilimo ufugaji na utalii ambazo zitasaidia kuongeza uwekezaji na kuinua uchumi wa mtu mmoja mmoja na Taifa kwa ujumla.

Ushauri huo umetolewa leo na Katibu Tawala  Mkoa huo Dkt. Fatma Mganga alipokutana na viongozi mbambali  wa chama cha waandishi wa habari mkoani Singida (Singida Press Club) kwa lengo la  kujitambulisha na kujadili namna ya kuboresha ufikishwaji wa taarifa kwa jamii.

Amesema Mkoa wa Singida una vivutio vingi vya kitalii ambavyo vikitangazwa vinaweza kuongeza idadi ya watalii na wananchi kuongeza maslahi kwa wananchi.

Aidha RAS Fatma ameeleza nafasi ya waandishi wa habari Mkoani hapo katika kukuza viwango vya ufaulu kwa kufanya mahojiano baina ya shule zinazofanya vizuri na zinazofanya vibaya hasa katika kipindi hiki ambacho wanafunzi walioripoti shule ni asilimia 87  mkoa mzima.

Hata hivyo amewapongeza kwa namna waandishi hao wanavyoshirikiana na Serikali kupeleka taarifa kwa wananchi huku akiwakumbusha kufuata maadili ya kazi yao ili kuleta tija kwa jamii.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa chama hicho Elisante John amesema chama kinahitaji kufanya kazi kwa karibu na Serikali ili kuweza kuwafikishia habari wananchi huku akieleza kwamba wanajipanga kuadhimisha miaka 20 tangu kuazishwa ifikapo Oktoba, 2023.

Aidha mwenyekiti huyo alimumba Katibu Tawala kuona uwezekano wa kuongeza ushirikiano na chama hicho ambacho kina mpango wa kuanzisha miradi yake hivi karibuni.


No comments:

Post a Comment