Wednesday, June 07, 2023

Peter Serukamba asherehekea kumbukizi ya kuzaliwa kwake kwa kukagua miradi ya maendeleo.

Mkuu wa Mkoa wa Singida Peter Serukamba ametumia tafrija ya kusherehekea kumbukizi ya siku yake ya kuzaliwa kuipongeza Halmashauri ya Wilaya ya Ikungi kwa kuharakishaa utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo ikilinganishwa na Halmashauri nyingine.

RC Serukamba ameeleza kufurahishwa kwake na Halmashauri hiyo baada ya kutembelea miradi mbalimbali kwa muda wa siku mbili yenye thamani ya Tsh. zaidi ya Bilioni Tatu kwa Wilaya nzima ambapo miradi mingi imekaribia kukamilika na ambayo haijakamilika ilikuwa na idadi kubwa ya mafundi ikilinganishwa na Halmashauri nyingine alizotembelea mwishoni mwa wiki iliyopita.

Mkuu wa Mkoa wa Singida Peter Serukamba (kulia) akifunua kitambaa kuashiria uwekaji wa jiwe la msingi ujenzi wa mabweni mawili na bwalo katika shule ya msingi Ikungi (kushoto) ni Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Thomas Apson.

Akiwa katika ukumbi wa mikutano ambapo alikutana na baadhi ya watumishi wa Halmashauri hiyo kufanya majumuisho baada ya kumaliza ziara yake, Serukamba alitoa pongezi hizo kwa viongozi na watumishi kwa namna walivyojipanga kusimamia miradi ndipo walimstukiza kwa kumuimbia wimbo maarufu wa kumbukizi ya kuzaliwa "happy Birth day to you RC Serukamba"

Mkuu wa Mkoa wa Singida Peter Serukamba (kulia) akilishwa keki na Mkuu wa Wilaya ya Ikungi kama sehemi ya kusherehekea siku ya kuzaliwa kwake.

"Nimetembelea miradi mbalimbali katika Halmashauri Sita lakini Halmashauri hii ya Ikungi mmefanya kazi vizuri sana, kwa kweli mmenifariji"

Aidha amemshukru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania  Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuleta fedha nyingi Mkoani hapo ambapo amesema kila Tarafa ina Mradi wa kutekeleza.

RC  Serukamba amefafanua kwamba  mafanikio ya Wilaya ya Ikungi yametokana na ushirikiano mzuri baina ya viongozi jambo ambalo amesema linafaa kuigwa na Halmashauri zote Mkoani hapo.

Hata hivyo  Menejimenti na watumishi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Singida wakiongozwa na Katibu Tawala wa Mkoa huo wametuma pongezi kwa kiongozi huyo na kumtakia Maisha marefu yenye baraka tele.

Mkuu wa Mkoa wa Singida akikagua mradi wa barabara wakati wa ziara hiyo wilayani Ikungi

Ukaguzi wa miradi ukiendelea




No comments:

Post a Comment