Friday, June 23, 2023

Maafisa Elimu Wakumbushwa Kutembelea Miradi ya Ujenzi wa Madarasa Mkoani Singida


Maafisa Elimu mkoani Singida wametakiwa kutoka ofisini kwao na kwenda kuwasaidia Walimu wakuu ambao wanatekeleza miradi ya ujenzi wa vyumba vya madarasa kupitia mradi wa Boost ili kushauriana namna ya kuharakisha umaliziaji wa ujenzi huo kabla ya tarehe 30 Juni, 2023.

Akiongea wakati wa ziara yake iliyofanyika leo (Juni 23, 2023) katika Manispaa ya Singida Katibu Tawala Mkoa wa Singida Dkt. Fatuma Mganga, amesema Maafisa Elimu wanatakiwa kushirikiana kwa karibu na walimu wanaosimamia ujenzi ili kusaidia kutatua changamoto ndogo zinazotokea katika shule hizo. 

Amesema ipo miradi mingine imekamilika na vifaa vya ujenzi vimebaki wakati huo yapo madarasa ambayo kwa sababu moja au nyingine wamepungukiwa na baadhi ya vifaa jambo ambalo Afisa Elimu angeweza kuwasiliana ili kubadilishana vifaa hivyo.

"Maafisa elimu msikae tu ofisini tembeleeni miradi yenu ili muweze kushauri hata kama shule nyingine wamepingukiwa vifaa unaweza kufanya mawasiliano baina ya shule na shule wabadilishane vifaa, mfano simenti, kokotoa hata tofali" Fatuma Mganga. 

Akiwa katika shule ya Sekondari Mungumaji ambapo kulikuwa na ujenzi wa bweni la wavulana amesema haridhishwi na usimamizi unaofanywa na maofisa elimu sekondari kwa kuwa inaoneka mafundi hawakusimamiwa vizuri hasa katika umaliziaji na uwekaji wa milango.

Aidha pamoja na changamoto hizo Katibu Tawala huyo amewapongeza viongozi wa Halmashauri ya Manispaa Singida kwa kuikamilisha miradi ya boost kwa asilimia zaidi ya 95 miradi ambayo imegharimu jumla ya Tsh.Bilioni 1.37

MATUKIO MBALIMBALI WAKATI WA ZIARA


Katibu Tawala Mkoa wa Singida Dkt. Fatuma Mganga akisisitiza jambo wakati wa ziara hiyo.






















No comments:

Post a Comment