Tuesday, September 06, 2022

RC Serukamba awahubiria Madiwani Mkoani Singida uadilifu na ushirikiano.

Mkuu wa Mkoa wa Singida Peter Serukamba akizungumza na Madiwa wa Manispaa ya Singida (hawapo pichani) wakati wa kikao cha Baraza lililofanyika leo katika ukumbi wa mikutani katika shule ya Sekondari Mwenge Septemba 6, 2022.

Madiwani wa Halmashauri za Wilaya zote za Mkoa wa Singida wametakiwa kufanya kazi kwa uadilifu na kushirikiana hasa katika miradi ya maendeleo inayoendelea kutekelezwa maeneo mbalimbali Mkoani hapo ili kuimarisha usimamizi wa watendaji katika Halmashauri zao.

Akiongea katika mabaraza mbalimbali ya Madiwani aliyohudhuria leo Mkoani hapo yakiwemo Manispaa ya Singida, Singida Vijijini, na Mkalama kama sehemu ya kujitambulisha, Mkuu wa Mkoa wa Singida Peter Serukamba ameonya tabia ya baadhi ya Madiwani kuwa wakusanya kodi na watoa misamaha ya ushuru katika mageti mbalimbali ya kukagua mazao na kuwataka kusimamia majukumu yao ya msingi ya kuwasimamia watendaji.

Serukamba amesema vitendo ambavyo sio vya kiadilifu vikifanywa na viongozi kama Madiwani vitasabisha kiongozi huyo kushindwa kuwasimamia watendaji wa kazi hata kama watakuwa na makosa katika kazi zao.

"Ukimuomba Mhandisi akupe mifuko miwili ya saruji yeye atachukua mitano na hutaweza kumuuliza, ukikusanya kodi wewe watendaji hawataweza kukuuliza na Diwani hutaweza kumsimamia mwingine ambaye alikusanya kodi pasipo kupeleka benki”. Alisema Serukamba

Akiongelea kuhusu msimu wa kilimo RC Serukamba  ameelekeza kwamba  Madiwani wahakikishe kwamba wakulima wanaongeza eneo la kilimo ikilinganishwa na mwaka jana kwa kuwa Serikali imeendelea kutoa ruzuku za pembejeo za kilimo ikiwemo mbegu na mbolea.

Aidha Serukamba amewataka wakulima mkoani hapo kuanza maandalizi ya mashamba mapema ili mvua za kwanza zitumike kwa kupandia kwa kuwa uzoefu wa msimu uliopita ulionesha kwamba waliowahi kupanda walipata mazao ikilinganishwa na waliochelewa kupanda.

Hata hivyo RC amesema kwamba Serikali inatumia kiasi kikubwa cha fedha kuagiza mafuta ya kupikia kutoka nchi za nje ambapo ameeleza kwamba Mkoa wa Singida una uwezo mkubwa kuondoa pengo hilo kwa kuongeza eneo la uzalishaji na matumizi ya mbegu bora za kilimo.

Mkuu wa MKoa wa Singida Peter Serukamba akizungumza na Madiwani pamoja na Watendaja wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama wakati wa kikao cha baraza lililofanyika katika ukumbi wa mikutani wa Halmashauri hiyo.

Akiwa Mkalama Mkuu wa Mkoa amewataka viongozi wa eneo hilo kuhakikisha kunajengwa soko la vitunguu ili kuondokana na changamoto ya walanguzi kuwafuata wakulima mashambani.

Aidha amesema kwa kuwaacha walanguzi kuingia mashambani kumesababisha wakulima kutopata faida inayotokana na kazi yao kwa sababu ya ulanguzi unaofanywa huko shambani.

Hata hivyo Serukba ameendeleza kampeni yake ya kuhakisha kila kaya inakuwa na BIMA ya Afya ya CHF iliyoboreshwa ambapo amewataka Madiwani kusaidia zoezi hilo kwamba hata mwananchi ambaye hatakuwa na uwezo kulipa 30,000 watatoa mifugo kwa ajili ya kupata bima hiyo.

Mkuu wa Wilaya ya Singida Mhandisi Paskasi Muragili akizungumza wakati wa kikao cha Baraza la Madiwani.

Mkuu wa Wilaya ya Mkalama Sophia Kizigo akizungumza wakati wa kikao cha Baraza la Madiwani.

Mstahiki Meya wa Manispaa ya Singida Yagi Kiaratu akizungumza wakati wa kikao cha Baraza la Madiwani.

Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya Singida Vijijini Elia Digha akizungumza wakati wa kikao cha Baraza la Madiwani.

Sehemu ya Waheshimiwa Madiwani wa Halmashauri ya Singida Vijijini

No comments:

Post a Comment