Thursday, August 25, 2022

Serukamba: Makarani ongezeni juhudi kuhesabu watu tumalize kwa wakati.

 

Makarani wa Sensa Mkoani Singida wametakiwa kuongeza juhudi za kuhesabu watu katika Kaya ili kuweza kukamilisha zoezi hilo kwa wakati.

Akiongea na wajumbe wa sensa wa Mkoa huo leo katika ukumbi wa mikutano wa ofisi ya Mkoa huo, Mkuu wa Mkoa Peter Serukamba amezitaja Halmashauri za Itigi na Manyoni kwamba tokea zoezi limeanza tarehe 23 mpaka leo asubuhi ya tarehe 25 bado walikuwa hawajavuka asilimia 30 wakati Wilaya nyingine za Mkoa huo zikiwa zimefikia asilimia  zaidi ya 40.

Aidha RC Serukamba amemuagiza Mratibu wa sensa Mkoa wa Singida Naing'oya Kipuyo kuangalia uwezekano wa kuongeza  timu ya Makarani ndani ya Wilaya ambao tayari wamemaliza kuhesabu Kaya walizopangiwa kutoa msaada kwa wenzao ambao bado hawajamaliza, lengo likiwa ni kuhakikisha zoezi linakamilika kwa wakati.

Hata hivyo amewapongeza Makarani wa Wilaya ya Mkalama, Singida DC na Manispaa ya Singida ambapo ndani ya siku mbili wameweza kufikia asilimia zaidi ya 40.

Hata hivyo amewataka kuongeza juhudi ili ikiwezekana zoezi likamilike kabla ya siku ya mwisho kwa sababu jnawezekana. Alieleza RC Serukamba.

Naye Katibu Tawala Mkoa wa Singida Mwl. Dorothy Mwaluko ameeleza kwamba wametoa vyombo vya usafiri kama pikipiki za Maafisa Tarafa, Maafisa mifugo na kilimo pamoja na magari ili kusaidia zoezi la Sensa katika Halmashauri ya Manyoni na Itigi kwa kuwa jographia yake imetawanyika kwa kiasi kikubwa.

Amesema maeneo mengi ya Halmashauri hizo umbali kutoka nyumba moja kwenda nyingine ni mkubwa ambapo isingekuwa uwepo wa vyombo hivyo zoezi lingekuwa gumu.

Naye Mratibu wa sensa Mkoa wa Singida Naing'oya Kipuyo amesema Serikali imeendelea kutatua changamoto zinazojitokeza katika zoezi la sensa ambapo pamoja na kutoa power benk ambazo zimekabidhiwa kwa Makarani kwa maeneo yenye changamoto za Umeme bado imetoa idhini ya kupatikana kwa huduma ya majenereta ambayo yatawekwa katika mashule ili vishikwambi vitakavyopata changamoto ya kuishiwa chaji viweze kuchajiwa.

No comments:

Post a Comment