Wednesday, June 25, 2025

WCF YAWASHIKA MKONO WENYE MAHITAJI MAALUM SINGIDA

 Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mhe. Halima Dendego, ametoa shukrani za dhati kwa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi - WCF (Worker's Compensation Fund) kwa kuonesha moyo wa huruma kwa watu wa Singida, hususan wenye mahitaji maalum. 

Ameyasema hayo leo Juni 25,2025 wakati wa hafla ya makabidhiano ya Vifaa saidizi kwa  wanafunzi wenye mahitaji maalumu katika Chuo cha Ufundi Stadi na Marekebisho kwa Watu Wenye Ulemavu Sabasaba mkoani Singida, 

Hafla hiyo imefanyika ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya miaka 10 ya WCF ambapo jumla ya viti mwendo 100 (viti maalum 10 na vya kawaida 90), fimbo nyeupe 154 na limu paper maalumu 200 vilikabidhiwa kwa uongozi wa chuo hicho.

Mhe.Dendego Ameongeza kuwa kitendo cha kuifanya Singida kuwa sehemu ya program hiyo ya WCF kwa watu wenye ulemavu kinaonesha upendo wa kweli, na kuongeza kuwa ofisi yake itaendelea kufuatilia na kushughulikia changamoto zote zilizotolewa na uongozi wa chuo hicho.

Katika salamu zake, Mhe. Dendego pia amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuendelea kumuamini kuiongoza Singida, akiahidi kuendeleza juhudi za kuhakikisha kila mwananchi ananufaika na fursa mbalimbali za maendeleo. Akikiri kuwa mchango wa taasisi kama WCF unathibitisha kuwa sekta ya hifadhi ya jamii ni mshirika halisi wa maendeleo ya mkoa.

Hata hivyo Mkurugenzi Mkuu wa WCF, Dkt. John Mduma, akitoa salaam zake ameeleza kuwa kuelekea kuadhimisha miaka 10 ya Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi - WCF (Worker's Compensation Fund) kwa kuwasaidia watu wenye ulemavu unatokana na mafanikio makubwa ya mfuko huo tangu kuanzishwa kwake huku akiahidi kuwa WCF itaendelea kuwekeza katika jamii kupitia sera yao ya kurudisha kwa jamii, ili kuhakikisha Watanzania wote, bila kujali hali zao, wananufaika na uwepo wa taasisi hiyo.

Kwa upande wake Mkuu wa Chuo hicho, Bi. Fatuma Malenga, ameeleza kuwa Taasisi hiyo ambayo inatoa mafunzo ya ushonaji, umeme na huduma za utengemano, kwa kupitia  msaada huo utasaidia wanafunzi kuwa na mazingira rafiki ya kujifunzia. Kadhalika ameahidi kuwa vifaa vilivyotolewa vitasimamiwa kwa weledi ili kutoa matokeo yanayotarajiwa kwa vijana hao.

Nao Wanafunzi wenye mahitaji maalum, wameonesha shukrani zao kwa WCF kwa msaada huo muhimu akiwemo Amina Mshana, mwanafunzi mwenye ulemavu wa miguu, amesema kiti mwendo alichopokea kitamrahisishia usafiri wa kila siku akiwa chuoni. Kadhalika Isack Edward, mwenye ulemavu wa macho, amepongeza upatikanaji wa fimbo nyeupe akisema sasa ataweza kusafiri kwa usalama zaidi. 

Zoezi hilo limeongozwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Mhe. Ridhiwani Kikwete  hafla ya makabidhiano ya vifaa saidizi ambaye ameeleza kuwa msaada huo utasaidia wanafunzi kujifunza kwa ufanisi na kujitegemea, huku akiwasihi walimu na watendaji wa chuo kuhakikisha vifaa hivyo vinatumika kwa malengo yaliyokusudiwa ili kutoa matokeo chanya kwa jamii.

Hafla hiyo imeonesha kwa vitendo namna taasisi za hifadhi ya jamii zinavyoweza kushiriki kikamilifu katika ujenzi wa jamii jumuishi na yenye usawa.

No comments:

Post a Comment