Thursday, June 13, 2019

RC SINGIDA APONGEZA HALMASHAURI ZA MKOA WA SINGIDA KWA KUPATA HATI SAFI KWA MWAKA WA FEDHA 2017/2018.

Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt. Rehema Nchimbi pamoja na Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida Dkt. Angelina Lutambi wakiwa na Viongozi wa Mkoa na Wilaya pamoja na Baraza la Madiwani wa halmashauri ya Wilaya ya Manyoni wakati walipotembelea mradi wa kilimo cha Korosho (Masigati) 12 June, 2019.

MKUU wa Mkoa wa Singida Dkt. Rehema Nchimbi amezipongeza Halmashauri zote za mkoa wa Singida kwa kupata hati safi, kutoka kwa Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG).

Dkt. Nchimbi, ametoa pongezi hizo wakati akizungumza katika kikao Maalum cha Baraza la Madiwani cha hoja za ukaguzi kilichofanyika katika ukumbi wa zamani wa Halmashauri ya Wilaya ya Iramba mkoani Singida.

Amesema, Watumishi na Watendaji  ni waajiriwa wa Serikali  iliyoko madarakani, ni lazima wawe waaminifu na waadilifu kwani ndiyo inayowalipa mshahara.

‘’Ukiona mahali kuna hoja za ukaguzi, ujue kiwanda cha kuzalisha  hoja ni watumishi na watendaji,  sisi watumishi na watendaji tukikaa vizuri hakutakuwa  na hoja, ninyi ambao hamkuwepo wakati hoja za ukaguzi zilipokuwa zinazalishwa na watendaji waliopita onyesheni mfano basi msiwe na dhana ya kukariri, kunakilishwa halafu ninyi wenyewe hamuonyeshi mabadiliko, hivyo inawapasa kuonyesha kwamba sisi hatuna hoja ndipo hapo tutakapokutana na kujipongeza kwamba tumepata hati safi’’ Dkt. Nchimbi

Amesema, ni lazima watumishi na watendaji wazingatie hasa kwa utumishi wa awamu ya tano, awamu ambayo si ya maslahi binafsi bali ni ya  kutekeleza   agenda za kitaifa.

‘’Sisi sote ni wasaidizi wa Mheshimiwa. Dkt. John Pombe Magufuli, Rais ambaye hafanyi kazi kwa maslahi yake, hivyo inawapasa kuwa makini sana katika utendaji  wenu”. Amesisitiza Dkt. Nchimbi

Aidha, Mkuu huyo wa Mkoa wa Singida amezipongeza kwa dhati Halmashauri zote za Mkoa wa Singida kwa kupata hati na kuwataka kuendelea kufanya kazi kwa bidii katika kuwatumikia Wananchi na Taifa kwa ujumla.

Kwa upande wake, Katibu Tawala wa Mkoa wa Mkoa wa Singida Dkt. Angelina Lutambi, amesema kuwa kuna hoja zingine  hazikuwa za lazima bali ni uzembe wa watendaji  ambao hawakuwa makini  katika kutekeleza majukumu yao.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya wilaya ya Iramba Bw. Linno Mwageni, aliwasilisha hoja za ukaguzi 64  na kutoa taarifa ya Halmashauri hiyo kupata hati safi kwa mwaka wa fedha 2017/2018. 

MATUKIO KATIKA PICHA 
WAKATI WA ZIARA YA MKUU WA MKOA WA SINGIDA KUTEMBELEA MASHAMBA YA KILIMO CHA KOROSHO, WILAYANI MANYONI.





IMETOLEWA NA,
KITENGO CHA HABARI NA MAWASILIANO,
OFISI YA MKUU WA MKOA
SINGIDA

No comments:

Post a Comment