Mkuu wa Mkoa wa
Singida Dkt Rehema Nchimbi akishiriki kupunguza nyasi katika uwanja wa Namfua
ambapo mechi kati ya Singida United na Yanga itachezwa jumamosi hii.
Mkuu wa Wilaya ya
Singida Elias Tarimo (katikati) akimueleza jambo Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt
Rehema Nchimbi (kushoto) alipotembea uwanja wa Namfua ambapo mechi kati ya
Singida United na Yanga itachezwa jumamosi hii, mwanzoni kulia ni Katibu wa
Timu ya Singida United Abdulrahman Sima.
Baadhi ya Vijana
waliojitokeza kusaidia ukarabati wa uwanja Namfua kwa kupaka rangi ambapo mechi
kati ya Singida United na Yanga itachezwa jumamosi hii.
Hii ni Sehemu ya
uwanja wa Namfua ambapo mechi kati ya Singida United na Yanga itachezwa
jumamosi hii.
Mkuu wa Mkoa wa
Singida Dkt Rehema Nchimbi ameitahadharisha timu ya Yanga kuwa ijiandane
kupambana na timu ya Singida United itakayocheza uwanja wa nyumbani ikiwa imara
na tayari kwa ushindi kwa kuwa timu hiyo imeingia ligi kuu kushinda na sio
kushiriki.
Dkt Rehema Nchimbi
ameyasema hayo mara baada ya kukagua uwanja wa Namfua Stadium ambao mechi kati
timu ya Singida United na Yanga itachezwa uwanjani hapo jumamosi hii huku akisisitiza
kuwa timu ya Singida United imeingia Ligi kuu kushinda na sio kushiriki wala
kufanya mazoezi.
"Yanga ijiandae
kufungwa, kwetu ushindi ni muhimu kwakuwa tumejipanga sawasawa kwa ajili ya
ushindi, hatujaingia Ligi kuu kushiriki au kufanya mazoezi, sisi tumeingia
kushinda na Yanga walitambue hilo", amesisitiza Dkt Nchimbi.
Ameongeza kuwa ana
uhakika wa ushindi kwa timu ya Singida United kutokana ana ubora na maandalizi
mazuri ya timu pamoja na kuchezea uwanja wa nyumba wa Namfua ambao umeboreshwa
kwa viwango vya hali ya juu.
"Kwa mara ya kwanza
baada ya miaka kumi na saba timu yetu itacheza mechi ya ligi kuu katika uwanja
wa nyumbani, Uwanja huu ambao ni mali ya Chama cha Mapinduzi umekarabatiwa na
uko katika hali bora sana", ameeleza Dkt Nchimbi.
Aidha amewataka
mashabiki wote wa Singida United waliopo mkoani Singida na mikoa ya Jirani
kujitokeza kwa wingi ili kutoa hamasa na kuishangilia timu yao pamoja na
kushuhudia ikifanya vizuri.
Ameongeza kuwa katika
mechi hiyo kutakuwa na fursa za kufanya biashara mbalimbali hivyo amewataka
wafanyabiashara wote kupeleka bidhaa bora ambazo zitautangaza vema mkoa wa
Singida.
Kwa upande wake
Katibu wa Timu ya Singida United Abdulrahman Sima amesema timu hiyo
imeshawasili mkoani Singida kwa ajili ya mechi ya jumamosi huku wakitarajia
ushindi kutokana na mazoezi pamoja na hamasa ya mashabiki wake watakaojitokeza
katika uwanja wa Namfua.
Sima amesema kuwa
maandalizi yote yako tayari huku ukarabati wa uwanja, vyoo na vyumba vya wachezaji
vikiwa katika hali nzuri, mageti yote yako imara na pia shirikisho la Mpira wa
miguu nchini (TFF) wameshafanya ukaguzi wa uwanja huo.
No comments:
Post a Comment