Thursday, August 24, 2017

PROFESA MKUMBO AELEKEZA MAMLAKA ZA MAJI KUBUNI VYANZO VYA MAPATO.


Katika kile kinachoonekana kutekeleza dhana ya 'hapa kazi tu', Katibu Mkuu Wizara  ya Maji Profesa Kitila Mkumbo akipanda juu ya tanki kuchungulia maji katika vyanzo vya maji kijiji cha Mwankoko Manispaa ya Singida.

Katibu Mkuu Wizara  ya Maji Profesa Kitila Mkumbo akiambatana na Katibu Tawala Mkoa wa Singida Dkt Angelina M Lutambi(katikati) na Mhandisi wa maji SUWASA Robert Sunday (kushoto), wakikangua vyanzo vya maji kijiji cha Mwankoko Mnispaa ya Singida.

Katibu Mkuu Wizara ya Maji Profesa Kitila Mkumbo (wa pili kulia) akipewa ufafanuzi wa mashine ya kupampu maji katika chanzo cha maji cha kijiji cha Mwankoko Manispaa ya Singida na Mhandisi wa SUWASA Patrick Nzamba.

Katibu Mkuu Wizara ya Maji, Profesa Kitila Mkumbo amezihimiza mamlaka za maji na mabonde ya maji kubuni vyanzo vipya vya mapato vitakavyosaidia kujiendesha vyenyewe  bila kutegemea serikali kuu.

Profesa Mkumbo ametoa wito huo wakati akizungumza na watumishi wa mamlaka ya maji Singida (SUWASA), Bonde la maji kanda ya kati na maabara, mjini hapa mjini .

Amesema Serikali haina fedha za kukidhi mahitaji yote ya mamlaka za maji na mabonde nchini hivyo ni vema vikaweka mikakati ya kujitengemea kimapato.

“Duniani kote hata Marekani haitoi fedha kwa taasisi kama hizi zenu. Tumieni kalamu na akili zenu kwa ajili ya kuandika maandiko yatakayowasaidia kupata fedha za kujiendesha bila kutegemea serikali au wafadhili”, amesisitiza.

Akisisitiza zaidi, kwa kusema umefika wakati sasa mamlaka na mabonde ya maji, zifikirie kuwekeza na kujiwekea mipango thabiti ya kuongeza mapato yao.

Aidha, Katibu Mkuu huyo amewataka watumishi wa SUWASA, kutoa huduma bora itakayovutia wananchi wengi zaidi kupata huduma ya maji katika mamlaka hiyo.

“Wateja wa maji ndio wanaowalipa ninyi mishahara na stahiki zingine. SUWASA ikiwa na wateja wachache kwa vyo vyote uendeshaji wake utakuwa mgumu na hivyo hivyo upatikanaji wa mishahara yenu nao utakuwa mgumu”, amesema Profesa Mkumbo.

Ameongeza kuwa SUWASA na mamlaka nyingine za maji nchini ni lazima ziwe na mkakati wa kupanua wigo wa wateja.

“Utamaduni wa kutoa huduma bora unamfurahisha mteja na atapenda kuendelea kuwa mteja wa SUWASA wakati wote. Pia itawavutia watu wengi kukimbilia huduma bora zinazotolewa na SUWASA”,alisema.  

Katika hatua nyingine, Profesa Mkumbo ametumia nafasi hiyo kusisitiza utaratibu wa kulipia kwanza (pree paid) maji kabla ya kupata  huduma ya maji.

 Amesema  utaratibu huo utasaidia kuepukana na wateja wakorofi ambao huzalisha madeni sugu na kusababisha mamlaka kushindwa kutoa huduma zinazokidhi mahitaji ya wateja.

“Kupitia utaratibu huu mteja husika ni lazima ajue matumizi yake ya maji kwa kipindi cha mwezi. Baada ya hapo analipia kiwango hicho cha maji halafu ndipo apewe maji ya kiwango alicholipia”, amesema katibu mkuu huyo.

Awali Afisa Maji bonde la kati Benard Chikarabhani amesema wameanza utekelezaji wa ujenzi wa bwawa la Farkwa kwa lengo la kuongeza usambazaji wa maji katika mji wa Dodoma, Bahi, Chamwino na halmashauri ya wilaya Chemba.

“Bwawa hilo linatarajiwa kuwa na kiasi cha maji cha mita za ujazo 470,000,000 na litachukua eneo la kilometa za mraba 68 pia bwawa litatumika kuboresha kilimo cha umwangiliaji katika mradi wa umwangilaji Bahi”, amesema Chikarabhani.

Wakati huo huo, Chikarabhani amesema bodi ya maji bonde la kati inatarajia kutumia zaidi ya shilingi bilioni 2.4 kugharamia ujenzi wa ofisi makao makuu mjini hapa.

“Fedha hizo zitagharamia pia ukarabati wa ofisi na maabara katika ofisi ndogo ya bodi zilizopo mkoani Shinyanga. Vile vile ujenzi wa ofisi ya jumuiya ya watumijai maji ya Mto wa Mbu”, amesema afisa huyo.
Picha/habari Na Nathaniel Limu


Mhaidrolojia bonde la maji la kati Robert Sunday akichangia hoja kwenye mkutano ulioitishwa kwa ajili ya Katibu Mkuu Wizara ya Maji Profesa Kitila Mkumbo kuzungumza na watumishi wa SUWASA, bonde la maji kati na maabara.
Katibu Mkuu Wizara  ya Maji Profesa Kitila Mkumbo akizungumza na watumishi watumishi wa Mamlaka ya SUWASA, bonde la maji la kati na maabara mjini hapa. Wa kwanza kulia ni Mhandisi SUWASA, Patrick Nzamba.

Picha/habari na Nathaniel Limu.

No comments:

Post a Comment