Monday, June 09, 2014

TUME YA HAKI ZA BINADAMU NA UTAWALA BORA YAWAFUNDA WAKUU WA IDARA NA VITENGO JUU YA HAKI ZA BINADAMU.



"Suala la uwajibikaji kwa watumishi wa umma wakiwemo wa Halmashauri ni changamoto kubwa kutokana na  baadhi yao kutozingatia maadili ya kazi zao, kuendekeza rushwa, kutoa huduma zisizokidhi matarajio ya wananchi na hivyo kusababisha malalamiko ya wananchi dhidi ya serikali".

Katibu Tawala Mkoa wa Singida Liana Hassan ameyasema hayo leo asubuhi katika ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wakati akifungua mafunzo ya Mpango kazi wa Kitaifa wa haki za Binadamu kwa wakuu wa idara na vitengo 60 kutoka Mikoa ya Dodoma na Singida.

Katibu Tawala Mkoa wa Singida Liana Hassan akisoma hotuba wakati wa kufungua mafunzo kwa Wakuu wa Idara na vitengo kutoka Mkoa wa Dodoma na Singida ya Mpango kazi wa Haki za Binadamu.

Liana amesema ipo haja kubwa ya kueneneza elimu ya haki za binadamu na misingi ya utawala bora katika jamii ili haki hizo ambazo zimeaninishwa katika Katiba ya nchi, sheria na mikataba ya haki za binadamu itambuliwe na kuheshimiwa na watu wote.

Ameongeza kuwa hivi karibuni vyombo vya habari vimekuwa vikitoa taarifa za uvunjifu wa haki za binadamu hali inayoonesha kuwa bado kuna uelewa mdogo wa haki za binadamu na misingi ya utawala bora katika jamii.

Baadhi ya washiriki wa Mafunzo ya Mpango kazi Haki za Binadamu wakifuatilia mafunzo hayo.

Liana amesisitiza kwa kutoa mifano ya taarifa za ukatili dhidi ya watoto, matukio mbalimbali ya wananchi kujichukulia sheria mikononi dhidi ya watuhumiwa wa uhalifu, ukatili dhidi ya wanawake na utumikishwaji wa watoto kuwa yamekuwa yakijitokeza kwa wingi.

Tume ya haki za Binadamu inatoa mafunzo ya siku nne kwa wakuu wa Idara na Vitengo 60 kutoka Mikoa ya Dodoma na Singida juu ya Mpango kazi wa Kitaifa wa Haki za binadamu wa mwaka 2013/2017.

Mafunzo hayo yatajikita katika kutambua makundi mbalimbali ya haki za binadamu ambayo ni haki ya kiraia na kisiasa, haki za kiuchumi, kijamii na kiutamaduni, haki za makundi na misingi ya utwala bora.
 



Washiriki wa mafunzo kutoka Mkoa wa Singida wakiwa katika picha ya Pamoja na Katibu Tawala Mkoa wa Singida Liana Hassan.

Washiriki wa mafunzo kutoka Mkoa wa Dodoma wakiwa katika picha ya Pamoja na Katibu Tawala Mkoa wa Singida Liana Hassan.

No comments:

Post a Comment