Monday, July 17, 2023

WATAALAM WA BOMBA LA MAFUTA GHAFI WAANZA KAZI RASMI MKOANI SINGIDA, RC SERUKAMBA AWATAKA KUFANYA KAZI KWA WELEDI.

Mkuu wa Mkoa wa Singida Peter Serukamba amewataka Wataalam wa kazi ya upimaji wa Mkuza wa Bomba la mafuta ghafi (EACOP) kutoka Kabaale Hoima nchini Uganda hadi Chongoleani Tanga nchini Tanzania kufanya kwa weledi ili kukamilisha kwa wakati na kupata matokeo chanya.

Serukamba ameyasema hayo leo katika ukumbi wa mikutano wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa huyo wakati wa ufunguzi wa kikao maalum cha wataalam walioweka kambi mkoani humo kwa ajili ya maandalizi ya kazi ya upimaji wa Mkuza wa bomba hilo lenye urefu wa kilomita 1,443 ikiwa kilomita 2,247 kwa upande wa Tanzania na kilometa 296 kwa upande wa Uganda.

Amesema, Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imedhamiria kuhakikisha miradi yote ya kimkakati inakamilika kwa muda uliopangwa na hili linajidhihirishia kwa wataalam hao ambao wameonekana kuwa na nia na ari itakayowapa msukumo wa kukamilisha kazi hiyo.

“Nina imani mnatambua umuhimu wa mradi huu kwa taifa letu, hivyo katika mikoa linapopita bomba hili na kwa wananchi mmoja mmoja ni toe rai kuwa na moyo wakizalendo tunapoenda kufanya kazi hii ili kuruhusu mradi kutekelezeka pasipo na vikwazo vyovyote hasa vya ardhi” Serukamba

Ameeleza kuwa kwa upande wa Tanzania bomba hilo litapita katika mikoa nane (8) Wilaya 24 na Kata 134 hivyo amesema mradi huo ni wa kipekee katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati na unajumuisha ujenzi wa vituo (PS) sita vya kusukuma mafuta ambapo vituo 4 vitakuwa Tanzania na viwili Uganda.

Ameongeza kuwa vituo viwili vya kupunga msukumo (PRS) vitakuwa kwa upande wa Tanzania, Matanki manne yakuhifadhia mafuta yatakayojengwa katika eneo la Chongoleani yenye ujazo wa mapipa laki tano kwa kila moja sambamba na gata la kupakia mafuta ghafi kwenye meli.

Aidha, amefafanua kwamba kutokana na aina ya mafuta (mafuta mazito), bomba litakuwa na mfumo wa upashaji joto kuwezesha mafuta kutiririka kwa urahisi.

Akimalizia hotuba yake Serukamba amesema, bomba hilo ndilo litakalokuwa refu zaidi duniani lenye mfumo wa upashaji joto na huo ndio upekee wake ambapo litajengwa kwa kipindi cha miaka mitatu (3) na uendeshaji wake utachukua takribani miaka ishirini na tano (25) kulingana na kiasi cha mafuta yatakayozalishwa.

Hata hivyo Mkuu huyo wa Mkoa amewahakikishia timu ya wataalam hao ulinzi na usalama wa afya zao na vifaa vya utekelezaji wa mradi huo kwa kipindi chote hadi kukamilisha kazi hiyo huku akiwasihi wananchi mkoani humo kutumia fursa la mradi huo katika kujikwamua kiuchumi.

Timu ya Wataalam imeanza kutekeleza rasmi kazi mkoani Singida Julai 14, 2023. imefanikiwa kupima vituo vya kusukuma mafuta, kupunguza kasi ya mafuta na barabara zinazoingia katika vituo hivyo katika mikoa ya Kagera Geita Tabora Singida Manyara na Tanga. Utekelezaji wa upimaji wa njia ya Bomba la mafuta la Afrika Mashariki ni ishara ya kuanza uwekezaji katika uchumi wa nchi na upatikanaji wa ajira.

Kikao maalum cha wataalam kwa ajili ya maandalizi ya kazi ya upimaji wa Mkuza wa bomba la mafuta ghafi (EACOP) kilihusisha Makamisha wa Ardhi wasaidizi kutoka mikoa ya Kagera, Geita, Shinyanga, Tabora, Dodoma, Manyara na Tanga pamoja na mratibu wa mradi EACOP kutoka TPDC na wawakilishi kutoka Wizara ya Nishati.

No comments:

Post a Comment