Thursday, May 25, 2023

RAS Dkt. Fatma atembelea kambi ya Mashindano ya UMITASHUMTA, Mwenge Singida

Katibu Tawala Mkoa wa Singida Dkt. Fatma Mganga hivi karibuni ametembelea kambi ya vijana wa shule ya msingi iliyopo shule ya Sekondari Mwenge ambapo wanaendelea na mashindano ya UMITASHUMTA yanayoshirikisha michezo ya mpira wa miguu kwa wanawake na wanaume, kikapu mpira wa Pete, riadha, kwaya, ngoma na mingineyo.

Akiwa uwanjani hapo RAS amewataka viongozi, wahudumu wa afya na makocha wa timu hizo kuendelea kuwasimamia wanafunzi hao waweze kufanya vizuri katika michezo na kuweza kuwakilisha vyema katika mikoa mingine watakapo chaguliwa.

Aidha ameahidi kwa wale watakaochaguliwa kuendelea na mashindano kwa hatua za mbele kwamba Serikali ya Mkoa wa Singida itaendelea kutoa ushirikiano mkubwa huku akiwakumbusha kwamba wahakikishe wanashinda michezo yote.

"Serikali itaendelea kuwaunga mkono na kuhakikisha ina vilea na kuviendeleza vipaji mlivyo navyo, muhimu ni kujitahidi mtakao tuwakilisha huko mikoa mingine mrudi na ushindi mkubwa”Dkt. Mganga


Kwa upande wake Afisa michezo wa Mkoa, Amani Mwaipaja katika taarifa yake amesema mashindano  yanayoendelea katika viwanja vya shule ya Sekondari Mwenge iliyopo Singida mjini yalianza ambayo tarehe 23 hadi 26 Mei, 2023 na kambi ya mkoa itaendelea kwa muda wa siku 6 kuanzia tarehe 26 hadi 31 Mei, 2023.

Hata hivyo Afisa Michezo huyo ameeleza kwamba kwa sasa wanaendelea kujipanga na safari ya kuelekea Tabora ambapo mashindano ngazi ya Taifa yatafanyika kuanzia tarehe 2 Juni, hadi 13, 2023.

Aidha alifafanua kwamba kutakuwa na mashindano ya UMISSETA yatakayoanza Juni 6, hadi Juni 9, na kambi ya mkoa tarehe 10 hadi 13 Juni, safari ya kuelekea Tabora itakuwa 14 Juni, na mashindano ngazi ya Taifa yataanza tarehe 15 Juni hadi tarehe 26 Juni, 2023 na kurejea tarehe 27 Juni.

Mashindano haya kwa mwaka huu yanaongozwa na kauli mbiu isemayo “Uimarishaji wa Miundombinu ya Elimu Nchini ni chachu ya Maendeleo ya Taaluma, Sanaa na Michezo”.




No comments:

Post a Comment