Friday, April 28, 2023

RC Serukamba azindua Kamati ya Mkoa ya Watu wenye Ulemavu, akerwa na wanaowatumia Walemavu kujipatia vipato.

 

Wakuu wa Wilaya Mkoani Singida wameagizwa kuwachukulia hatua wote wanaowatumia watu wenye ulemavu kama chanzo cha kujipatia vipato kwa kuwatumia kwenda kuomba na baadae kuwasilisha fedha hizo kwa waliowatuma.

Agizo hilo limetolewa leo tarehe 28.04.2023 na Mkuu wa Mkoa huo, Peter Serukamba wakati akizindua Kamati ya Watu wenye ulemavu ya Mkoa iliyofanyika katika ukumbi mdogo wa Mikutano wa Ofisi hiyo.

RC Serukamba amewaagiza wakuu hao wa Wilaya kufanya zoezi la kuwabaini watu wenye ulemavu ambao wanajihusisha kuombaomba na kufanya ufuatiliaji kwa kina na kuwachukulia hatua wote wanojihusisha katika kuwatumia watu wenye ulemavu katika kuomba.

Aidha RC Serukamba ametoa rai kwa viongozi wote wa Serikali na taasisi binafsi waone umuhimu wa kuwekeza katika kundi hilo na kutenga bajeti toshelevu kwa ajili ya wenye ulemavu ikiwemo utoaji wa mikopo isiyo na riba na kuwaunganisha katika fursa mbalimbali za kiuchumi.

Kwa upande wake Katibu Tawala Mkoa wa Singida Dkt. Fatma Mganga ameipongeza kamati hiyo ambayo ameeleza kwamba itasaidia mkoa kupata taarifa za watu wenye ulemavu wa Mkoa huo.

Hata hivyo RAS ameeleza kwamba Ofisi ya Mkoa itatoa Ushirikiano na kamati hiyo ikiwa ni pamoja na kuzibaini fursa za watu wenye ulemavu Mkoani hapo.


No comments:

Post a Comment