Thursday, November 03, 2022

Waliomkataa Mwenyekiti wa Kijiji wakutana na Serukamba

Wananchi wa Kijiji cha Choda Kata ya Mkiwa Wilayani Ikungi Mkoa wa Singida hivi karibuni wameeleza nia yao ya kumkataa Mwenyekiti wa Kijiji hicho kwa tuhuma mbalimbali zikiwemo za kutofanya mikutano ya kuzungumzia maendeleo ya Kijiji chao.

Maelezo hayo wameyatoa mbele ya Mkuu wa Mkoa huo Peter Serukamba wakimuomba kuingilia kati mgogoro huo wa uongozi ambao umekuwa wa muda mrefu.

Akiwa katika mkutano huo wa hadhara wananchi hao walieleza kutoridhishwa na uongozi wa kijiiji kwa kuwa hauitishi mikutano na kutowasomea wananchi mapato na matumizi ya Kijiji chao.

Kutokana na malalamiko hayo RC Serukamba alihoji Halmashauri ya Kijiji hicho kuhusiana na tuhuma hizo ambapo Mwenyekiti wa Kijiji hicho alieleza kwamba wapo wananchi ambao kutokana na itikadi zao hawajitokezi kwenye mikutano inapoitishwa hivyo kukosa uelewa wa kutosha kuhusiana na mapato na matumizi ya Kijiji hicho.

Aidha baadhi ya wananchi walipoulizwa kama waliowahi kuhudhuria mikutano iliyoishwa na Halmashauri hiyo pamoja na viongozi mbalimbali wa vijiji walieleza kwamba hawakuhudhuria.

Akizungumza na viongozi hao Rc Serukamba amesema kwa mujibu wa maelezo aliyoyapata kutoka kwa viongozi wa Halmashauri ya Kijiji, pamoja na viongozi wa CCM wa tawi na Kata amebaini tuhuma zinazotolewa dhidi ya Mwenyekiti wa Kijiji hicho hazina mashiko ya kumuondoa katika nafasi yake.

Awali Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Mhe. Jerry Muro akitoa taarifa ya jinsi walivyoshughulikia mgogoro huo amesema walilazimika kufanya vikao vitatu vya kutatua changamoto hiyo ambapo katika kikao cha mwisho mwezi October Dc. Muro aliwataka kufuata utaratibu endapo wanaona tuhuma za kumtoa Mwenyekiti wa Kijiji zina ukweli jambo ambalo baadhi ya viongozi hawakufanya hivyo.

RC Serukamba mbali na kupongeza jitihada za awali za Wilaya katika kutatua mgogoro huo amewataka wajumbe wa Halmashauri ya Kijiji na viongozi wa CCM tawi kufanya kazi na Mwenyekiti huyo na kumpa ushirikiano ili atekeleze majukumu yake ipasavyo na kuwaonya baadhi ya wajumbe kuacha kuweka maslahi yao binafsi.

Mkutano na Wananchi ukiendelea.

No comments:

Post a Comment