Wednesday, November 16, 2022

Singida yaweka mikakati ya kufuta daraja sifuri katika shule za Sekondari

 

Mkoa wa Singida umeweka mikakati ya kuboresha elimu ya Sekondari ili kuhakikisha kwamba wanafuta daraja la mwisho (division zero) kuanzia mwaka huu 2022.

Kauli hiyo imetolewa leo na Mkuu wa Mkoa huo Peter Serukamba wakati akihitimisha Mkutano wa Kamati ya Ushauri ya Mkoa (RCC) uliofanyika katika ukumbi wa mikutano Chuo cha Uhasibu Mkoani hapo.

Amesema Serikali ya Mkoa imedhamiria kuinua kiwango cha elimu kwa kuhakikisha wanaanza kufuta daraja sifuri na hatimaye watafikia daraja la tatu.

Amesema ili kufanikiwa katika zoezi hilo ni lazima wazazi, walimu, wanafunzi na viongozi wa Dini na jamii kwa ujumla washirikiane na viongozi wa Serikali kuandaa na kutekeleza mkakati huo ili ulete matunda.

Kwa upande wake Katibu Tawala Mkoa wa Singida Mwl. Dororthy Mwaluko amesema tayari ameshafanya kikao na Walimu wakuu wote na Maafisa elimu kata ambapo waliandaa viwango vya kuwapima kwa kila kata na kila kila shule.

Aidha amesema jumla ya shule za Sekondari 146 kati ya shule 168 za Serikali zimeandaliwa kutoa chakula cha mchana ili kuwavutia wanafunzi kuja shule na kupata nguvu ya kusoma.

Katibu Tawala Mkoa wa Singida Mwl. Dororthy Mwaluko, akizungumza wakati wa kikao cha Kamati ya Ushauri ya Mkoa Novemba 16, 2022

RAS ameendelea kusema kwamba mpango huo utaendelea kutekelezwa katika shule za Sekondari huku akibainisha kwamba kwa upande wa shule za msingi bado zoezi halijakaa sawa ambapo jumla ya shule 187 kati ya shule 609 ndizo zinazopata chakula.

Hata hivyo Mwaluko ameeleza kwamba jitihada nyengine walizofanya ni kuteua Wakuu wa shule katika shule mpya zilizojengwa na kufanya uhamisho wa walimu waliopo ili kukidhi haja ya upungufu wa walimu.

Akimalizia hotuba yake Mwaluko ameeleza kwamba Mkoa wa Singida umeanzisha mpango ujulikanao "Singida Digital Class" ambapo wanafunzi hutumia video za masomo yaliyorekodiwa ili kujifunzia hasa katika shule ambazo hazina walimu wa masomo husika.

Katibu Tawala Msaidizi  Mipango na Uratibu Mkoa wa Singida Beatrice Mwinuka, akizungumza wakati wa kikao cha Kamati ya Ushauri ya Mkoa Novemba 16, 2022





Kikao kikiendelea

No comments:

Post a Comment