Saturday, August 06, 2022

WAZIRI MKUU AHITIMISHA ZIARA MKOANI SINGIDA, AWAAGIZA WAKUU WA WILAYA KUSIMAMIA FEDHA ZA MAKUSANYO

 

WAZIRI Mkuu, Kassim Majaliwa, amewaagiza Wakuu wa Wilaya kuhakikisha wanasimamia Watumishi wote katika Halmashauri za Mkoa wa Singida ambao walikusanya fedha za mapato lakini hawakuzipeleka benki wanazirudisha haraka.

Ametoa agizo hilo leo kwenye kikao cha majumuisho ya ziara yake ya siku mbili mkoani hapa wakati akizungumza na Watumishi wa Halmashauri za Wilaya ya Singida, Ikungi na Halmashauri ya Manispaa ya Singida.

Alisema kumekuwa na tatizo kubwa kwenye Halmashauri nyingi nchini katika ukusanyaji wa mapato ya ndani ambapo baadhi ya Watumishi wanapokusanya fedha haziingizwi kwenye mfumo wa Serikali jambo ambalo limekuwa kero kubwa.

"Wakuu wa Wilaya hakikisheni Watumishi wanaodaiwa fedha wazirudishe haraka, Iramba, Manyoni na hata Ilongero (Halmashauri ya Wilaya ya Singida) nimepewa orodha ya Watumishi ambao wanadaiwa fedha za makusanyo," alisema.

Majaliwa alisema Rais Samia Suluhu Hassan amekuwa akisisitiza suala la ukusanyaji wa mapato na hata majuzi wakati anawaapisha wakuu wa mikoa lakini cha kushangaza baadhi ya Watumishi wa umma wamegeuka kuwa wabadhirifu.

Alisema ujanja unaofanywa na baadhi ya Watumishi kufuja fedha za makusanyo ni kwamba wanapokusanya fedha hasa wanapobaini ni nyingi wanazima mashine ili zisiingie kwenye mfumo wa Serikali.

Aidha, Waziri Mkuu amewataka Watumishi kuacha urasimu katika utendaji wa kazi kwani mambo hayo ndio yanakaribisha vitendo vya rushwa chini.

Kuhusu idara za manunuzi, alisema limekuwa ni tatizo kubwa ambapo Idara hizo zimekuwa zikiweka makadirio makubwa ya bei za manunuzi ya vifaa vya ujenzi kwenye miradi hususani inayotumia 'force account'.

Aliongeza kuwa kwenye Halmashauri kumekuwa na tatizo kubwa la usimamizi wa miradi inayotekelezwa na kwamba kuna umuhimu kwa Watumishi kuhakikisha suala hili linapewa umuhimu wa juu.

Alisisitiza suala la mahusiano kwa Watumishi wa Umma mahali pa kazi kwani kufanya hivyo kutaboresha utendaji kazi na kuleta ufanisi mkubwa katika kuwatumikia wananchi.

Aidha, alizitaka Halmashauri kuratibu vizuri suala la wafanyabiashara wadogo maarufu wamachinga ili wapewe maeneo ya kufanyia biashara zao bila usumbufu.

Awali Waziri Mkuu aliweka jiwe la msingi la ujenzi wa jengo la Ofisi ya Halmashauri ya Wilaya ya Singida linalojengwa Ilongero katika kijiji cha Mwahango kwa thamani ya Sh. 2.7 bilioni.

Akizungumza na wananchi wa eneo hilo, alimwagiza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Singida, Ester Chaula, kuisimamia idara ya manunuzi ili ujenzi wa jengo hilo uweze kukamilika na kuanza kutumika.

"Nimeridhishwa na ujenzi unavyoendelea, DED (Mkurugenzi wa Halmashauri) isimamie idara ya manunuzi, wasikuvuruge, mkandarasi alipwe fedha zake, " alisema.

Akiwa katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Singida inayojengwa kwa Sh. bilioni 19.5 Waziri Mkuu, alisema ujenzi wa hospitali hiyo itakuwa mkombozi mkubwa kwa wananchi wa mkoa huu na mikoa jirani.

MATUKIO MBALIMBALI WAKATI WA ZIARA

WAZIRI Mkuu, Kassim Majaliwa, akikagua ujenzi wa jengo la Ofisi ya Halmashauri ya Wilaya ya Singida linalojengwa Ilongero katika kijiji cha Mwahango.

WAZIRI Mkuu, Kassim Majaliwa (kushoto) akiweka jiwe la msingi katika jengo la Ofisi ya Halmashauri ya Wilaya ya Singida.

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa (kushoto) akipeana mkono wa pongezi na Mwenyekiti wa CCM Mkoa Alhaji Jumanne Kilimba mara baada ya kuweka jiwe la msingi katika jengo la Ofisi ya Halmashauri ya Wilaya ya Singida.


Mkuu wa Mkoa wa Singida Peter Serukamba akizungumza na wananchi (hawapo pichani) waliojitokeza katika hafla ya uwekaji wa jiwe la msingi jengo la Ofisi ya Halmashauri ya Wilaya ya Singida. 

Baadhi ya waananchi waliojitokeza kushuhudia uwekaji wa jiwe la msingi jengo la Ofisi ya Halmashauri ya Wilaya ya Singida uliofanywa na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa wakati wa ziara yake wilayani Singida vijijini mkoani Singida. 

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa (kulia) akizungumza jambo kwa furaha na Mbunge wa Viti Maalum Nusrat Hanje (mwenye kilemba chukundu) wakati wa salamu za Wabunge wa mkoa huo.




Muonekano wa jengo la Ofisi ya Halmashauri ya Wilaya ya Singida linalojengwa Ilongero katika kijiji cha Mwahango kwa thamani ya Sh. 2.7 bilioni.

Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Singida Jumanne Kilimba akitoa salamu za chama wakati wa ziara hiyo.

Mkuu wa Mkoa wa Singida Peter Serukamba akimkaribisha Waziri Mkuu Kassim Majaliwa wakati wa kukagua ujenzi wa Hospitali ya Rufaa Mkoa mkoani humo.








No comments:

Post a Comment