Thursday, August 11, 2022

RC Serukamba amewataka wakulima waliopewa mashamba kwenye Skimu ya umwagiliaji Itagata kuyaendeleza haraka mashamba hayo.

 

Mkuu wa Mkoa wa Singida Peter Serukamba amewataka wakulima waliopewa mashamba kwenye Skimu ya umwagiliaji Itagata katika Halmashauri ya wilaya ya Itigi mkoani Singida kuyaendeleza  haraka mashamba hayo kwa kuyalima mazao yenye tija kwa mtu binafsi na Serikali vinginevyo Serikali itawanyang'anya na kuwapa watu wengine.

RC Serukamba amesema hayo baada ya kufanya ziara ya kikazi kukagua shughuli za kilimo zinazofanywa na wakulima kwenye skimu hiyo ambayo imeigharimu Serikali bilioni 2.1 hadi kukamilika kwake.

Akiwa katika mashamba ya wakulima kwenye skimu  ya Umwagiliaji Itagata Itigi RC Serukamba amesikitishwa na kilimo kinavyoendelea ambapo kati ya ekari 209 walizogawiwa wakulima ambao ni wananchama wa umoja wa umwagiliaji Itigi ekari 40 tu ndizo walizolima muda wa kiangazi jambo ambalo amesema halitakubalika.

"Serikali imewekeza fedha nyingi sana kwenye mradi huu na mimi nimefika kwenye mashamba haya nimeyaona, watu wengi hawajalima kuna jumla ya ekari 209 lakini ekari zilizolimwa kiangazi hiki ni 40 tu mashamba na maji yapo, sasa hii haikubaliki lazima watu walime ili kuisaidia Serikali kupata mapato, Tume ya umwagiliaji nao wapate tozo zao" alisema Serukamba.

Mkuu wa Mkoa wa Singida Peter Serukamba akiongoza jopo la watendaji wakati wa ukaguzi wa skimu ya kilimo cha umwagiliaji wakati wa ziara yake Agosti 11, 2022 katika halmashauri ya Wilaya ya Itigi wilayani Manyoni.

Aidha Mhe. Serukamba ameongeza kwa kuwataka wananchama wote wa ushirikia kuandaa mkutano ambao  utakuja kubainisha na kuwatambua wakulima waliopewa mashamba, na ambapo wanalima kutumia skimu hiyo.

"Mwezi wa tisa mwenyekiti andaa mkutano na wanachama wako ili tuje tujue nani analima na nani halimi ili wale ambao hawalimi tuwaondolee mashamba tuwape wengine ambao watalima na kuipa Serikali mapato pamoja na Tume ya umwagiliaji" Aliongeza Mkuu huyo wa Mkoa Singida

Mkuu huyo wa Mkoa alisisitiza kuwa faida atakayoipata mkulima kupitia kilimo kwenye skimu hiyo itamrahishia maisha kiuchumi ataweza kuhudumia familia, kulipa bima ya afya  pamoja na kuchangia maendeleo ya taifa lake.

Akizungumza mbele ya Mkuu wa Mkoa mkulima anayejulikana kama Chacha Marwa alisema kuwa changamoto mojawapo inayopelekea  wakulima wengi kutolima ni kushindwa kutambua aina ya udongo  pamoja na baadhi ya Wanachama  wa umoja huo wa umwagiliaji waliopewa mashamba kuyakodisha kwa watu wengine.

"Mhe. Mkuu wa Mkoa sisi huu udongo unatuchanganya sana tunashindwa kuelewa tulime mbegu gani tunaomba mtusaidie kutupimia udongo wetu" Alisema Chacha.

Aliongeza kuwa baadhi ya wasimamizi wa skimu hiyo sio waaminifu kwa wanachama wao jambo linalopelekea washindwe kufanya shughuli za kilimo cha umwagiliaji akisema kuwa baadhi wamekuwa wakikodisha mashamba na kuwanyima fursa wengine.

Akisoma taarifa ya mradi huo Mwenyekiti wa Umoja wa umwagiliaji Itagata Stephen Mbonge alisema kuwa mashamba yenye ukubwa wa Ekari 209 yaligawiwa kwa wanachama 321 ekari 106 ziligawiwa kipindi cha masika mbunga ekari 73 na kutoa tani 105.7 na mazao mengine ekari 33 ambazo zimetoa tani 28.19 lakini kipindi hiki cha kiangazi ekari 40 tu ndizo zimelimwa zikiwa na mazao mchanganyiko na hazijavunwa.

Baada kusomewa taarifa ya mradi wa Skimu ya Umwagiliaji Mkuu wa Mkoa Serukamba akafika  kuzungumza na wananchi wa kijiji cha Itagata msisitizo wake ukiwa katika kuendeleza mashamba yaliyopo kwenye skimu hiyo, kushiriki kwenye zoezi la Sensa Agosti 23 mwaka huu na kuwataka wananchi wa kijiji chicho kukata Bima ya afya ambayo imekuwa ndio wimbo wake tangu aanze majukumu yake Mkoani Singida.

MATUKIO KATIKA PICHA

Kilimo kikiendelea katika eneo la skimu ya kilimo ya umwagiliaji.

Sehemu ya kilimo cha mahindi na kitunguu katika skimu hiyo.

Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Manyoni Suleiman Mwenda akizungumza wakati wa kumkaribisha Mkuu wa Mkoa wa Singida kuzungumza na Wananchi wa kijiji cha Itagata. 

Baadhi ya Wananchi wa kijiji cha Itagata waliojitokeza wakati wa mkutano kumsikiliza Mkuu wa Mkoa wa Singida Peter Serukamba alipotembelea Skimu ya kilimo cha umwagiliaji kijijini hapo Agosti 11, 2022

Mkuu wa Mkoa wa Singida (kushoto) akimsikiliza mwananchi wa kijiji cha Itagata wakati wa ziara yake kujionea hali ya wanufaika wa mradi wa skimu ya umwagiliaji Itagata.

Mkuu wa Mkoa wa Singida (kushoto) akizungumza na wananchi wa Itagata wakati wa ziara yake kujionea hali ya wanufaika wa mradi wa skimu ya umwagiliaji Itagata.


No comments:

Post a Comment